Mch. Josephat Gwajima (SNP)
UTANGULIZI:
Warumi 8:1-2 “Sasa,
basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwa sababu
sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na
sheria ya dhambi na mauti.” Katika huu mstari wa pili tunaona
sheria tatu ambazo Biblia inazitaja, kwanza sheria ya uzima, sheria ya dhambi
na sheria ya mauti. Dunia hii inaongozwa na sheria (principles) na ndio maana
kuna katika ulimwengu wa kawaida kuna sheria mbalimbali. Mfano sheria ya
mvutano (gravitation force) na ndio maana ukichukua jiwe ukalirusha juu
litakwenda lakini baada ya muda litarudi chini tena. Na kimsingi huwezi
kubishana na sheria hiyo, na ukitaka kuibishia jaribu kwenda gorofani ujirushe
lazima utaanguka chini sio kwasababu huna upako bali ni kwasababu ya sheria ya
mvutano inayovuta vitu kuja chini.
DUNIA YA KAWAIDA NA
SHERIA ZILIZOPO:
Kwa kawaida sheria huwa hazibadiliki, kwa mfano sheria
inayosema unavyopanda kwenda juu baridi linaongezeka, hii sheria haibadiliki na
ndio maana katika mlima kuna baridi zaidi kwasababu ya sheria ambazo zipo. Na
vilevile sheria tulizoziona katika Biblia (warumi 8:2) ni bayana yaani
hazitanguki. Na kwa maana hiyo hata nchi ili iwe na amani ni lazima ziwepo
sheria na kanuni. Na ili watu wafuate sheria wamewekwa polisi, mahakama na
magereza kwaajili ya kuhakikisha zile sheria zinafuatwa.
Unapofanya kosa lolote, unaingia kwenye matatizo kwasababu
ya sheria iliyopo, kwa namna hiyo polisi watakukamata na kukupeleka mahakamani
unapogundulika una makosa unafungwa, hii yote ni kwasababu ya sheria iliyopo.
MAISHA YA KIROHO NA
SHERIA YA UZIMA, DHAMBI NA MAUTI:
Kama tulivyoona sheria za nchi zinazosimamia maisha ya
wananchi ndivyo sheria hizi za rohoni zinavyotenda kazi. Kimsingi unapovunja
sheria ile sheria inakushusha chini bila ya wewe kujua. Na ndio maana biblia
inasema “kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti bali karama ya Mungu ni uzima wa
milele” Kuna tofauti kati ya mshahara na zawadi, kwasababu unapotenda kazi ni
lazima upokee mshahara wake, upende usipende na ulieusilie.
Kimsingi, wewe unaweza ukawa unatenda vitu na hakuna
anayekuona, unaweza ukawa umeokoka lakini unatenda mambo mabaya au dhambi
katika ulimwengu wa siri. Siku utakayopokea mshahara kila mtu atajua isipokuwa
hatojua umepokea hilo kutoka katika kazi dhambi gani uliyotenda. Unaweza
kumuona mtu alikuwa wa Mungu lakini akafa ghaflaghafla watu wakasikitika na
kumbe umepewa mshahara wa matendo yake ya sirini. Maisha yako ya sirini ni
muhimu sana.
SHERIA YA DHAMBI:
Warumi 6:23: “Kwa
maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele
katika Kristo Yesu Bwana wetu.”
Ezekieli 18:4:
“Tazama, roho zote ni mali yangu; kama vile roho ya baba ni mali yangu, ndivyo
ilivyo roho ya mwana mali yangu; roho ile itendayo dhambi itakufa.”
Nini maana ya maneno haya?; hapo mwanzo sheria alikuwa
mbinguni, akifikia kipindi akafanya yaliyomaovu na kuasi hivyo akafukuzwa
mbinguni. Na alipotupwa duniani akaanzisha utawala wake katika kila mtaa
wa dunia hii ili kutenda kazi kila mahali. Haya majeshi ya pepo
wabaya yapo kwaajili ya kuwapa watu mishahara ya matendo mabaya wanayoyatenda.
Kwasababu shetani alikuwa mbinguni, anaifahamu biblia anajua
kanuni za Mungu, hivyo, unavyotenda lililoovu shatani anajua kuwa umekosea na
amekaa tayari kugawa mshahara. Kumbe mshahara huu hautoki kwa Mungu bali
shetani ndiye alipaye. (Yohana
10:10) yaani shetani hatendi kazi isipokuwa kuharibu, kuchinja na
kuharibu. Unapotenda uovu kwa siri, mashetani hukaa mahali ili kugawa mshahara
wa uovu ile. Na kwa muda ambao mashtaka yapo na hayajakanushwa kwa kutubu, mtu
huyo atajikuta anafia dhambini. Kwa namna hiyo watu wengi wanaishi kwenye
magonjwa na matatizo yanayotokana na maisha yao ya sirini ambayo hakuna
anayejua.
Kiukweli hakuna dhambi ndogo wala kubwa, hivyo dhambi
iliyondogo sana yaweza kumpeleka mtu Jehanamu. Dhambi ambazo watu huzidharau na
kuziita ndogo ndizo zipelekazo watu Jehanamu bila hata ya wao kujua. Jifunze
kutubu kila unapojikuta unamkosea Mungu.
Ni muhimu kutafuta mahali ulipouacha upendo wako wa kwanza,
uhurudie na ukatubu. Mungu ni mwenye rehema atakusamehe kabisa na hatoyakumbuka
makosa yako tena. Tengeneza maisha yako ya rohoni.
0 Comments