Na Mch. Josephat
Gwajima
04.03.2013
Utangulizi:
Shetani hajabadilika na silaha zake ni zilezile; na jambo
kubwa linaloshangaza watu ni kwamba silaha za shetani ni zilezile lakini bado
zinatenda kazi kwenye maisha ya watu. Moja ya kifungo kinachosumbua watu ni
kifungo cha tabia.
Mara nyingi kupata urafiki au uhusiano ni rahisi lakini ili
uweze kuendelea kuwa karibu na watu hao unatakiwa uwe na tabia nzuri. Hivyo
shetani anaweza kukuacha usonge mbele na kazi ya Mungu lakini akakuzuia kupitia
vifungo vya tabia. Kwasababu hii Roho Mtakatifu ametaka leo tujifunze kuhusu
vifungo vya tabia:
KIPAWA NA TABIA YA MTU:
Kuna vitu kadhaa vya kuangalia kama mtu wa Mungu unayehitaji
kufanikiwa, cha kwanza ni kipawa na pili ni tabia ya mtu.
Mithali 18:16 “zawadi ya mtu humpatia nafasi,
humleta mbele ya watu wakuu; ” hili neno zawadi kwenye Biblia ya kingereza
linaitwa “GIFT” au kwa Kiswahili kipawa. Sasa basi kipawa cha mtu chaweza
kumfikisha mbele za watu wakubwa na kujulikana. Mfano mtu anaweza kuwa na
kipawa cha uwimbaji lakini anakaa kijijini na umaskini, ila kile kipawa chake
kikionekana kinaweza kumleta mtu huyo mjini hii ndio maana ya sehemu ya kwanza
ya andiko hilo. Kwasababu hiyo kila mtu aliyepo duniani amepewa kipawa na Mungu
ambacho kwa hicho anaweza kufika kwenye hatua ya juu zaidi.
Sasa basi kipawa cha mtu humleta mtu kwenye mafanikio yake,
tatizo linakuja pale mtu anapokuwa na kipawa lakini tabia yake si nzuri. Hivyo
tabia ndio ambayo inakubakiza katika sehemu uliyopo. Mtu anaweza kuwa na macho
ya rohoni au upako lakini kama tabia yake ni mbaya hakuna mtu atakayetamani kuwa
karibu naye. Ili Mungu akutumie kwa kiwango cha juu ni muhimu kuanza kwa
kubadili tabia yako.
TABIA ZA KIMUNGU NA
TABIA ZA ASILI:
Biblia imeainisha tabia za aina mbili, yaani tabia ya Kimungu
na tabia ya kiasili au ya mwilini. Katika
1Wakoritho 2:14 “Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho
wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa
yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.” 1Wakorintho
3:1 kuna tabia za rohoni na tabia za mwilini. Hivyo anachosema Mtume Paulo
ni kwamba unapoongea na watu inabidi ujue ama mtu huyo ana tabia za rohoni au
za mwilini. Mfano mtu anaweza kuwa mwimbaji mzuri lakini ana tabia ya uongo;
Mtu mwingine anaweza kuwa na kipawa kitakachomfanya apate mchumba; lakini kama
tabia yake ni mbaya ama uongo, au umbeya au uzinzi inaweza kumfanya kuachwa na
mchumba wake sio kwasababu hapendwi bali kwasababu ya tabia. Tabia ya Kimungu
ni tabia njema na nzuri lakini tabia ya kibinadamu ni tabia mbaya aliyonayo
mtu.
Shetani akitaka kuharibu kipawa cha mtu anaanzia kwenye tabia
yake; kwa maana hiyo tabia ya kibanadamu au ya mwilini ndio hiyohiyo Biblia
inaiita tabia ya kishetani. Ukisoma katika Yakobo
3:15 “Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia
ya kibinadamu, na Shetani.” Unaona kumbe tabia mbaya ya kinadamu ndio hiyo
inaitwa tabia ya kishetani. Mhubiri 10:1
“Mainzi mafu huvundisha marhamu ya mwuza marashi; Kadhalika upumbavu haba ni mzito kuliko
hekima na heshima.” Hili ni neno la hekima la Mfalme Suleimani kusema mainzi
wanaweza kuharibu marhamu nzuri; ikimaanisha unaweza kupata mpenyo katika
maisha lakini tabia mbaya inaweza kukupeleka mbali kabisa na upenyo wako.
Ndio maana waweza kumkuta mtu ni mwombaji au anatenda miujiza
lakini tabia yake ikawa mbaya kwasababu ya asili. Jambo hili ndlo linalosabisha
watu wengine kusema “kama ulokole ndio huu sitaki kuokoka” kumbe mtu huyo aliwahi
kumuona mtu ambaye ameokoka na ananena au anaombea watu lakini ni mwongo au
mzinzi. Katika Biblia, Samson alikuwa mnadhiri wa Mungu na alikuwa amepakwa
mafuta tangu tumboni mwa mamaye. Japokuwa alikuwa mpakwa mafuta lakini alikuwa
na tabia mbaya ya kutaka wasichana wa kifilisti ambao Mungu alikataza tangu
mwanzo. Hii ni sawa na mtu kung’ang’ania kufungwa nira na mtu asiyeamini. Kwa
njia hii Samson akakutana na Delila ambaye lengo lake halikuwa upendo bali ni
kumharibia kipawa chake kwa kuijua siri yake. Vivyohivyo shetani amewaangamiza
watu wa Mungu wengi kwa kuwafanya waoe au kuolewa na watu wasiomjua Kristo na
matokeo yake kile kipawa cha Kimungu kilichokuwa ndani yao kinashindwa
kuonekana tena.
KUBADILI TABIA:
Tabia mbaya ya mtu huondoka kwa kuamua mwenyewe, hata kama
mchungaji akuombee mara zote kama tabia yako ni mbaya kwa asili inakulazimu
kuamua kuibadili mwenyewe. Ni kweli tabia yako inaweza kuwa imeshakupotezea
kibali kwa watu au imeshakupotezea upenyo katika maisha lakini ukiamua kuanza
upya na BWANA na kuacha zile tabia mbaya Mungu wetu ni wa nafasi ya pili. Mungu
wetu anatoa nafasi ya pili biblia inasema, “usifarahi ee adui yangu niangukapo
mimi nitasimama tena”
Leo naongea na watu ambao walikuwa waombaji leo hawaombi
tena, walimuhofu Mungu lakini leo hawana hofu, walikuwa watakatifu lakini leo
ni waovu wakubwa Mungu anayo nafasi ya pili kwaajili yako. Amua kutubu na kuacha
dhambi na tabia hiyo mbaya; Mungu atakuwezesha tena kama alivyomwezesha Samson
kuwaangamiza wafilisti wote. Hivyo uamuzi wa kwanza ni kuamua mwenyewe kuacha
tabia hiyo.
0 Comments