Na Mch. Maximillian Machumu 10.03.2013
Mchungaji Maximillian Machumu (RP) akihubiri jumapili hii |
KWANINI NDUGU WALIMFUNGA: kama tulivyosoma katika kitabu cha Waamuzi 15:9-16, ndugu zake ndio
waliohusika kumfunga Samsoni. Hapa tunajifunza kuwa mara nyingi adui (shetani)
anapotaka kumfunga mtu hupitia kwa watu wake au wanaomjua mtu huyo vizuri. Kifungo
kinachotokana na watu wako wa karibu ni kibaya zaidi kwasababu wanaujua udhaifu
wako; muda gani unaomba na muda gani huombi.
Ndio maana hata Mtume Paulo
aliwahi kutegeshewa nyoka kwenye kuni (Matendo
ya Mitume 28:3). Nyoka ni yule mtu wa karibu anayejua siri na mambo
unayoyafanya, kwasababu hiyo inakuwa rahisi kwa shetani kuwatumia kukuangamiza.
Nyoka hakuonekana mwanzoni kwa Paulo kwasababu alijifanya kama kuni, na watu wa
karibu ni vivyohivyo huwezi kuwatambua kwa urahisi. Furaha ni kuwa Mungu
hakuruhusu yule nyoka kumwangamiza Mtume Paulo.
KWANINI WALITUMIA KAMBA MBILI: Ndugu wa Samsoni walikuwa elfu tatu
lakini jambo la ajabu ni kuwa walibeba kamba mbili tu; Utajiuliza nini siri ya
hizi kamba mbili?. Yesu mwenyewe aliainisha kamba mbili kuu ambazo shetani
anazitumia kuwaangamiza na kuwafunga watu duniani. Ukisoma katika Ufunuo 1:18 “na aliye hai; nami nalikuwa
nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti,
na za kuzimu.” Kumbe zile kamba mbili zina maana ya mauti na kuzimu. Kuzimu
inaleta magonjwa na matatizo mbalimbali lakini mauti inaleta kifo. Kamba mbili
mpya ni mauti na kuzimu. Kwa kuzimu na mauti shetani amekuwa akiwaangamiza na
kuwatesa watu wa Mungu. Inawezekana na wewe ni mmoja wa watu wanaoteseka kwasababu
ya kamba hizi leo kuna habari njema kuwa Yesu aweza kukata kamba hizo.
MATOKEO YA KIFUNGO CHA SAMSONI: baada ya kumfunga, ndugu zake wakamkabidhisha
kwa wafilisti yaani adui zake. Jambo la ajabu likatokea, mara baada ya
kukabidhiwa. Imeandikwa, “Alipofika
Lehi, Wafilisti wakapiga kelele walipokutana naye; ndipo roho ya Bwana ikamjia
kwa nguvu, na zile kamba zilizokuwa juu ya mikono yake zikawa kama kitani
iliyoteketezwa kwa moto, na vile vifungo vyake vikaanguka mikononi mwake.”
Waamuzi 15:14 kupitia kifungo kile Mungu akamtumia Samsoni kuwaangamiza
wafilisti wote. Kumbe waweza upo katika kifungo ambacho Mungu alikiruhusu ili
upate ushindi ulio mkamilifu.
MUNGU ANAWEZA KUKATA KAMBA ZILIZO KATIKA MAISHA YAKO: Wachawi na
waganga wanaweza kuwa wajanja mbele ya macho yetu lakini Bwana anawaona, na
kamba zao zinaonekana mbele ya macho ya BWANA. Hata mfalme Daudi aliwahi kuwa
katika kamba hizo ukisoma katika Zaburi 119:61
“Kamba za wasio haki zimenifunga, Sikuisahau sheria yako.” Upo uwezekano wa
mtu kufungwa, Mwilini unajiona ni mtu asiye na mafanikio au asiye na mwelekeo
lakini rohoni unakuwa umefungwa na kamba kabisa. Zaburi 18:1->… “…Kamba za mauti zilinizunguka, Mafuriko ya
uovu yakanitia hofu. Kamba za kuzimu zilinizunguka, Mitego ya mauti
ikanikabili. Katika shida yangu nalimwita Bwana, Na kumlalamikia Mungu wangu.
Akaisikia sauti yangu hekaluni mwake, Kilio changu kikaingia masikioni mwake…”
Mungu anaweza kukutoa katika kamba za matatizo unayopitia. Daudi alipokuwa
katika kamba hizo aliliitia jina la BWANA.
Yesu alipofufuka akatangaza kuwa
anazo funguo za mauti na kuzimu, Hata kama aliyekufunga awe mtu wa karibu kiasi
gani lakini zipo funguo za kufungua kamba zilizokufunga. Kama alivyofanya kwa
Samsoni; baada ya kukufungua kinachofuata ni kipigo kwa wale wote walioshiriki
kukufunga. Mungu anaweza kukutofautisha; shida na mateso yote unayopitia si kitu
mbele za Mungu wetu kwasababu yeye anaweza kukuweka huru. Mpokee Yesu upate
uhuru mkamilifu, kwasababu dunia ya leo haipo salama kama haupo ndani ya Yesu.
0 Comments