Na Mch. Kiongozi Josephat Gwajima 22.4.2013 Kitabu cha Petro ni waraka wake kwa watu wote; ukisoma, 2 Petro 1:3 “kwa
kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa kwa
kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe” ukisoma kwa
haraka waweza usijue siri iliyopo katika andiko hili. Andiko hili linamaanisha
kuwa uweza wa Mungu umetupatia vitu vyote, kwa kumjua yeye.Kumbe hapa tunapata kujua kuwa ni mapenzi ya
Mungu tuwe na vitu vyote, na uweza huo wa Kiungu umeshatupa tayari “has given us” kila kitu kitupasacho kuishi. Maana ya andiko hilo ni kuwa hapo kabla ya maisha yetu kuanza Mungu alikuwa
ameshatukirimia mambo yote. Twaweza pata ufahamu mzuri zaidi kutoka kwenye
habari ya Yeremia; Ukisoma “Yeremia 1:4-…” andiko linaanza kwa kusema “kisha
neno la Mungu likamjia Yeremia…” Biblia inapotaja neno inamaanisha “Mungu”
kwasababu katika (Yohana 1:1-5) Biblia inathibitisha kuwa neno hilo ni Mungu
mwenyewe. Yesu Kristo ndio neno lililokuwa linawajia manabii hapo kabla, na
ndio maana mara zote Yesu alipokuwa duniani alitumia maneno kama “Amini amini
nawambia” au “Musa alisema hivi na mimi nasema hivi” Yesu alikuwa na mamlaka
hiyo kwasababu yeye ndiye neno lenyewe haijaandikwa popote kuwa neno la Mungu
likamjia Yesu, bali yeye alitamka neno kwa kuwa ndiye neno mwenyewe. Hivyo kwa
habari ya Yeremia, biblia inapotaja “neno” inamaanisha Yesu mwenyewe alimjia
Yeremia. Yesu alipomjia Yeremia akamwambia, (Yeremia 1:5) “kabla sijakuumba
katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa;” Kumbe Yesu
alimjua Yeremia kabla ya kuumbwa tumboni. Kimsingi, Hakuna mtu ambaye anaweza
kukumbuka kipindi yupo tumboni wala kabla ya kuwa tumboni, lakini Mungu
alikujua kabla ya kuwepo tumboni na alikukirimia vitu vyote. Swali la kujiuliza
kama Mungu alikujua tangu huko mwanzo, na alikukirimia kila kitu; kwanini maisha
yako yapo hivyo? Jibu la swali hilo litatoka katika ujumbe wangu wa leo “KESHO
ILIYOPINDISHWA”. Tukirudi kwa habari ya Yeremia, Mungu aliongea na Yeremia
akiwa kijana mdogo tu kuwa yeye amewekwa kuwa nabii wa mataifa (Yeremia 1:5).
Kumbe kabla hujazaliwa Mungu alikwishakuweka katika njia njema ya maisha yako
kama Yeremia; Jiulize nini kimetokea hadi leo upo kwenye njia nyingine? Mungu
alikuwekea mafanikio tangu mwanzo, lakini jiulize nini kimetokea hadi leo upo
katika hali hiyo mbaya? Yawezekana wewe ni maskini leo, lakini unatakiwa ujue pia Mungu hakuiti
kwa jina la umaskini bali anakuita kwa jina ambalo ndio kusidi lako. Warumi
8:29-30 “maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe
na mfano wa mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwa kwanza miongoni mwa ndugu
wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita na wale aliowaita; na wale
aliowaita, hao akawahesabia haki, hao akawatukuza” kumbe tunaona kuwa Mungu
amekwisha kuchagua tangu asili na tangu asili unatajwa kuwa mshindi. Na
ukifanikiwa kupekuwa kwenye mipango ya Mungu juu yako, hutaona kuwa unatakiwa
kuharibu mimba, au matatizo ya ndoa, au mateso ya umaskini, au kutokufanikiwa
au magonjwa ambayo yanayokusumbua sasa. Naweza fananisha jambo hili na mfano wa Treni na reli, mara zote treni
hutembea katika reli yake. Vivyo hivyo maisha yako ni sawa na Treni, yana reli
au njia ya Kiungu ya mafanikio yako, tatizo ni kuwa haupo kwenye reli na wewe
wafikiri upo kwenye reli; kwasababu hata Treni isipopita kwenye reli yake
itatembea kwa tabu baadaye itakwama; ndivyo ulivyo sasa unavyodhania kuwa
maisha yako ndivyo yalivyo sivyo, unajiona na gari moja sio sahihi ulitakiwa
uwe na kampuni! Kwasababu kama ungeona kusudi la Mungu katika maisha yako
usingeishi maisha unayoishi sasa. Kuna mtu anasoma ujumbe huu akiwa kijijini
lakini kumbe mpango wa Mungu, ulitakiwa uwe Uingeleza sasa hivi. Kuna mambo makuu na makubwa ambayo Mungu anakuwazia katika maisha yako lakini
hayajamilika kwasababu njia uliyotakiwa kupita imepindishwa (Waefeso 3:20).
Ndio maana malaika alipomtokea Gideoni alimwita kwa jina la “shujaa”. Japokuwa
Gideoni alikuwa mtu wa kawaida kwa
wakati ule bado kumbe tangu tumboni aliitwa shujaa na alitakiwa kuwa shujaa.
Tatizo ni maisha yaliyomzunguka yalimfanya asiujue ukweli huu kuwa yeye ni
shujaa. Pamoja na yote jina lile halikubadilika mbele za Mungu kuwa yeye katika
ulimwengu wa roho anaitwa shujaa. Je wajua kuwa kabla ya kuzaliwa ulikuwa
kwenye mapafu ya Mungu yaani ulikuwa pumzi ya Mungu, ulikuwa pamoja na Mungu
ndio maana biblia inakuita “mwana wa miungu” (Zaburi 82:6), hiyo ndio asili yako. Rudi kwenye asili yako leo,
asili yako sio uzinzi na uasherati, sio madeni, sio magonjwa, sio kushindwa.
Amua kurudi kwenye asili yako kwasababu tupo duniani na kusudi la Mungu
“mission” huwezi kufa ukiwa kwenye njia ya Mungu mpaka mission yako ikamilike,
wakunyweshe sumu wakuloge hutokufa mpaka ukamilishe mission yako. Kuna watu, kwasababu ya maisha wanayopitia wamejikuta wakijiuliza kuwa
Mungu yupo kweli? Unawaza kama Mungu angekuwepo usingepitia kwenye mateso yako?
Ni muhimu kujua Mungu alishakukirimia vitu vyote tatizo ni kwamba watu wengi
hawapo katika asili yao. Biblia inasema Mungu ametukirimia vyote kwa kumjua
yeye, sasa unachotakiwa kufanya ni kurudi katika njia, kwa kuanza kusoma neno,
kufanya maombi yaani unatakiwa ubadilishe staili yako ya maombi na uhamie
kwenye maombi ya kushindana ili kurudisha asili ya maisha yako. Kuna mashetani
na wachawi ambao wapo katika ulimwengu wa roho ili kubadili njia yako ambayo
Mungu alikuwekea ili uiishi. Inawezekana Mungu alikuweka kuwa kiongozi mkubwa
na mwenye kukubalika lakini wachawi na mashetani waweza kukuhamisha kutoka
katika njia ya Mungu aliyokuitia. Amua kurudi katika njia yako ambayo Mungu alikuita
kwayo. Warumi 8:19-21 Yaani hata viumbe vinavyoishi duniani vimetiishwa chini
ya uharibifu yaani vimehamishwa kutoka katika asili yao. Viumbe navyo vyajua
kuwa havipo katika asili yake, ndio maana navyo vinatarajia kufunuliwa kwake
Kristo Yesu ili virudi katika asili yao. Hata Hana aliposumbuka miaka mingi
pasipo kupata mtoto alimwomba BWANA akasema ukinipa mtoto atakuwa mjakazi wako,
hapo ndipo Mungu alipomuingiza nabii Samweli kwenye tumbo la Hana. (1Samweli
1:11) Nabii Samweli ni nabii aliyekuwa na nguvu za Mungu, ambaye Mungu
alimtumia sana; kumbe asili yake ni ile iliyotajwa na Hana akiwa kwenye maombi
kabla hata ya Samweli kuzaliwa. Amini usiamini maisha unayoishi, sio ambayo
Mungu alikupangia wewe uishi; hata wewe mwenyewe ni shahidi kuwa maisha hayo
siyo uliyotaka kuishi. Kuna mashetani wamepindisha asili yako na kukupa maisha
mengine na bahati mbaya zaidi umekubali maneno ya watu kukwambia “vumilia
vumilia”. Kuna muda unatakiwa uamue kuchukua hatua ya kupambana ili urudi
kwenye asili yako. Ndio maana watu ambao hawachukui hatua ya kuomba maombi ya
kushindana wanajikuta wanahama kila kanisa bila mafanikio kumbe unatakiwa
ufanye maamuzi ya kushindana na falme za giza. Huu ni wakati wa kuamua kurudi
kwenye asili yako uliyopangiwa na Mungu. Sikuzote shetani hufanya vita na watu ambao tangu asili waliitiwa maisha
mazuri, yeye (shetani) huwa hamisha na kuwafanya wawaze kuwa wanavyoishi ndivyo
Mungu anavyowataka kuishi. Leo amua kurudi katika asili yako, pambana na
mamlaka za giza. Imeandikwa kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama
bali ni juu ya falme na mamlaka za giza. Kataa kuishi maisha hayo na uamue
kurudi kwenye asili yako aliyokupangia Mungu. Mungu hakukupangia mateso hayo
unayopitia, Leo rudisha asili yako ambayo Mungu amekupangia. Mungu na
akurudishie asili ya maisha yako!!!
0 Comments