Na Mch. Josephat Gwajima (SNP) | GCTC; Dar es Salaam,
Tanzania; 23.08.2013
UTANGULIZI:
Kwa asili, Mungu ni Mungu wa
hatua kwa hatua, yeye huwapa watu hatua baada ya hatua. Na pia, kwa desturi;
maisha ni hatua kwa hatua; siku kwa siku; na ndio maana mafanikio ya mtu hayapo
katika kuokota almasi au kubahatisha tu bali ni hatua kwa hatua kuelekea katika
utele. Katika hali kama hiyo, upo uwezekano hatua ya mtu ya kimaisha
kucheleweshwa na kujikuta yupo kwenye hatua ambayo Mungu hakumkusudia kuwa
tangu mwanzo.
Mwanzo 15:13, Hapa tunaona kuwa Mungu aliongea na Abrahamu kwamba,
uzao wake (wana wa Israeli) watakaa utumwani kwa muda wa miaka mia nne. Lakini
jambo la kushangaza ni kuwa, wana wa Isarel wakakaa katika nchi ya utumwa,
Misri kwa muda wa miaka mia nne na thelathini (Kutoka 12:40-41) hapo tunapata kujua kuwa mafanikio ya mtu ya
rohoni au mwili yanaweza kucheleweshwa na mambo fulani iwapo hajaamua au
hajapata ufahamu wa kuyachukulia hatua.
MAANA YA HATUA:
Ili uweze kuelewa maana ya Hatua,
naweza kutumia mfano huu kuwa; katika maisha tunayoishi inawezekana mtu akaanza
katika kipato cha chini, kumtosha yeye peke yake, lakini baada ya muda mtu huyo
anapata kazi nyingine yenye kipato zaidi na baadaye kupanda cheo, anafikia kujenga
nyumba ya kwanza, ya pili na baadaye kupata safari za nje na kujenga magorofa
n.k. Hizo ni hatua ambazo Mungu amewapa watu wazipitie kwa kadri wanavyoendelea
kuishi. Kwa mfano huyo sasa tunajua kuwa, HATUA
ni maisha ya mtu ya kimaendeleo ambayo Mungu alimwekea kuyaishi duniani.
Ni muhimu kujua Mungu amemwekea
kila mtu hatua ambayo kwa hiyo, atafikia maendeleo na mafanikio katika maisha
yake. Ndio maana Mfalme Daudi alisema kuwa, “Uzielekeze hatua zangu kwa neno lako, uovu usije ukanimiliki” Zaburi
119:133; Mfalme Daud alijua kuwa Mungu hutoa hatua kwa kila mtu na upo
uwezekano wa hatua hizo kucheleweshwa.
UWEZEKANO WA HATUA YA MTU KUCHELEWESHWA:
Ukisoma katika Yeremia 25:11-12 “…nayo mataifa haya
watamtumikia mfalme wa Babeli kwa miaka sabini…” kutoka hapo tunaona kuwa
Mungu aliwaambia wana wa Israeli kuwa kipimo cha kuishi utumwani ni miaka
sabini lakini swali ni kuwa, je walikaa utumwani kwa miaka sabini? Jibu
tunalipata hapa, Danieli 9:2; Biblia inasema, Daniel kwa kusoma vitabu akagundua
kuwa muda wa kukaa utumwani umeisha. Na baada ya kugundua, Danieli alichukua
hatua ya kufunga na kuomba. Vivyo hivyo maisha ya mtu yaweza kucheleweshwa ili
asifikie katika hatma yake njema; ndio maana mtu aweza kuitwa aliyefanikiwa
katika miaka ishirini na mwingine miaka sabani; kimsingi wote wamefanikiwa
lakini mmoja amecheleweshwa.
Upo uwezekano wa Mtu, Tabia au
shetani kuchelewesha hatua au maendeleo ya mtu ya kimaisha. Ndio maana hata
wana wa Israeli walipokuwa wakitoka Israel, walikuwa na uchaguzi wa njia ama
fupi na njia ndefu. Lakini wana wa Israel walipitishwa njia ndefu ya miaka
arobaini jangwani kwasababu ya kukwepa vita. Maisha ya wana wa Israeli ni
kivuli cha maisha yetu ya rohoni; yaani waweza kufanikiwa baada ya miaka mingi
kwasababu ya kukwepa kuvipiga vita vya rohoni. Ndio maana mtu aweza kuolewa
lakini akiwa na miaka sitini au umejenga nyumba ukiwa na miaka sabini hata muda
wa kuikaa kwenye hiyo nyumba haupo, kwasababu tu shetani au tabia
kukuchelewesha.
SHETANI ANAVYOCHELEWESHA HATUA:
Kuna visababisho vingi vya kuchelewesha
hatua za mtu, navyo vyaweza kuwa Ndugu wa karibu, Tabia za mtu (mfano, uvivu,
wivu, dhambi n.k) au shetani. Leo tunaanza kwa kuangalia jinsi shetani
anavyoweza kuchelewasha hatua za Mtu. Katika kitabu cha Daniel 10:1-14; Hapa tunaona Daniel aliamua kufunga na kuomba bila
majibu, lakini katika siku ya 21 malaika Gablieli akaja na kumpa taarifa kuwa, “usiogope, Daniel; kwa maana tangu siku ile
ya kwanza ulipotia moyo wako ufahamu, na kujinyenyekeza mbele za Mungu wako, maneno
yako yalisikiwa…” ukiendelea kusoma, utaona malaika anamwambia kuwa majibu
yake yalizuiwa na mkuu wa anga la Uajemi.
Kumbe wapo watu wanamwomba Mungu
lakini bila kujua kuwa kuna shetani yupo mahali naye anazuia wasipokee kile
ambacho Mungu amewaahidia kwa wakati. Mithali
16:9; Mungu ndiye aongozaye hatua za mtu na pasipo yeye shetani aweza
kuchelewesha hatua hizo. Kimsingi Mungu amekuleta duniani na kukupa hatua
ambazo ulipaswa kuzipitia lakini kwasababu ya shetani unajikuta hata maisha
unayoishi sasa si sawa na hatua ambayo Mungu alitaka uwe nayo. Kisoma, Zaburi 73:2 “…hatua zangu zilikuwa karibu
na kuteleza” Biblia inaonyesha kuwa kuna uwezekano wa mtu kuteleza katika
hatua zake. Hizi si hatua za miguu ya kawaida bali ni maisha ya mtu ya kiroho
au kimwili katika kuelekea maendeleo.
MFANO WA ALIYECHELEWESHWA NA SHETANI KATIKA BIBLIA:
Katika biblia kuna mtumishi wa
Mungu mmoja aliyecheleweshwa Marko
5:6-20, Kimsingi, mtu huyu mwenye pepo ndani yake alikuwa na kazi na wito
ya kumtumikia Mungu kwa kuhubiri injili; na ndio maana baada ya kufunguliwa
akaenda kuhubiri injili katika Dekapoli lakini alikaa katika makaburi kwa miaka
mingi ambayo angeweza kuitumia kumtumikia Mungu. Ndio maana leo waweza kuwakuta
watu wana wito wa kumtumikia Mungu, lakini shetani anawaletea mawazo kinyume na
kumtumikia Mungu na mwisho wanakuja kugundua kuwa, wamepoteza miaka mingi
wakiwa wamecheleweshwa.
Hivi ndivyo shetani anavyoweza
kuchelewesha maisha ya mtu katika masomo, biashara, mafanikio, maendeleo,
mahusiano n.k Hii inaweza kutokea pale pepo wachafu wanapomwingia mtu na kuzuia
hatua za mtu za mafanikio na kama mtu huyo akikosa ufahamu kuwa shetani ndiye
anayefunga maisha yake; ataishia kulaumu na kukata tamaa bila mafanikio.
FANYA UCHAGUZI SAHIHI:
Ili kumiliki hatua zako kwa
wakati inabidi uamue mwenyewe kushindana katika ulimwengu wa roho. Ndio maana
kuna watu wameokoka na wengine hawajaokoka ambao waliwahi kutolewa unabii na
kunenewa mambo mengi na watumishi wa Mungu, lakini hadi leo hayajatimia kwao;
hii ni kwasababu ya kutokuamua kupigana katika ulimwengu wa roho. Na ndio maana
Daniel alipogundua kuwa siku za kukaa utumwani zimeisha aliamua kuomba na
kufunga ili kumiliki zile hatua ambazo Mungu amempangia.
Ni muhimu kujua kuwa Mungu
akikuahidia kitu sio lazima kitimie kwa wakati, unaweza ukachelewa maana yupo
azuiaye. Danieli aliomba kwa siku ishirini na moja bila majibu na inawezekana
alianza kumlaumu Mungu kwa kutomjibu maombi yake lakini kumbe tatizo lilikuwa
katika wakuu wa anga. Vivyo hivyo, usipoamua kushindana na wakuu wa anga na
shetani unaweza ukajikuta unapambana katika maisha bila mafanikio. Ni muhimu
kutumia mamlaka ambayo Yesu Kristo alituachia pale msalabani, kumsambaratisha
shetani anayejaribu kuchelewesha mafanikio yako katika Jina la Yesu Kristo.
Information Ministry, GCTC
0 Comments