Na Mch.
Josephat Gwajima.
Mch Kiongozi Josephat Gwajima |
Utangulizi:
Hii ni sehemu
ya pili ya somo la hatua iliyocheleweshwa. Ni muhimu kujua kuwa Mungu ni Mungu
wa makusudi na hakuna kitu anachofanya pasipo kusudi. Mbele za Mungu; Maisha ya
mtu hayaanzi tumboni mwa mama yake bali yanaanza kabla ya mtu kuwa tumboni
yaani Mungu huyaona maisha ya mtu kabla ya kuwa tumboni. Kimsingi, Mungu anajua
kesho ya mtu kabla haijafika; katika ulimwengu wa roho kusudi la maisha ya mtu
laweza kuonekana.
Kwa kuwa
shetani ni roho anaweza kuona kesho ya mtu na pia aweza kuichelewesha; leo
tunaangalia watu waliowahi kucheleweshwa katika Biblia.
Mchungaji aliyecheleweshwa katika Biblia:
Luka 8:26-39; “…akihubiri katika mji
wote” tuangalie pia, habari hiyo katika kitabu cha Marko 5:18-20 “…akaenda kuhubiri katika Dekapoli” maana ya neno
Dekapoli, ni “miji kumi” yaani tafsiri
ya deka ni kumi, polis ni mji. Kumbe
huyu aliyekuwa ameponywa akawa mhubiri katika miji kumi. Na ndio maana baadaye
Yesu naye alienda kuhubiri Dekapili kwasababu alishamtanguliza mtu huyo kule, Marko 7:31. Inawezekana kabisa kuwa Yesu alikuwa anaenda
Dekapoli kumtembelea huyo Mchungaji wa huko.
Mambo yote
ambayo Mchungaji huyu aliyafanya yalikuwa yamecheleweshwa kwa zaidi ya miaka kumi.
Ukisoma katika Marko 5:1-8; tunaona
Mchungaji huyu alihamishwa na shetani kutoka sehemu alipokuwa anaishi na kuishi
makaburini. Pia tunaona kuwa mtu huyu ambaye alikuwa na huduma ya uchungaji na
uwezo wa kuhubiri ndani yake alitupiwa mashetani ili asiweze kumtumikia BWANA. Katika
hili tunapata picha hii kuwa kuna uwezekano wa mtu ambaye Mungu alimpangia kuwa
ama mchungaji, mfanyabiashara maarufu, mwimbaji au kiongozi; kucheleweshwa na
shetani ili asiifikie hatma yake kwa wakati sahihi. Pepo wabaya wanaweza
kumchelewesha mtu asifikie kusudi ambalo Mungu amemwekea mtu. Ndio maana
ukifuatilia maisha ya watumishi wa Mungu wengi walianza tangu wakiwa na umri
mdogo.
Kesho Iliyocheweshwa:
Kama tulivyomuona
huyo mhubiri alivyocheleweshwa; vivyohivyo maisha ya watu wengi yamecheleweshwa
ili wasiishi maisha ambayo BWANA aliwawekea wayaishi. Mashetani wanaweza
kuchelewesha hatma njema ya maisha ya mtu. Unaweza kucheleweshewa utajiri,
watoto, ndoa au kazi; na ndio maana Yesu baada ya kumfungua yule aliyekuwa na
pepo wachafu hakutaka ajiunge naye bali akamwambia aende akahubiri injili
Dekapoli. Kumbe tangu mwanzo Mungu alimwekea kusudi la kuwa mhubiri ndani yake.
Unaweza
ukajiuliza; kwanini shetani anaendelea kukufuatilia ingawa umeshaokoka? Jibu ni
kuwa, una kitu kikubwa cha Mungu ndani yako; hivyo anachoweza kufanya ni
kukuchelewesha usikifikie na kwa njia hii shetani ameteka maisha ya watu wengi.
Mwanamke tajiri aliyecheleweshwa:
Jina Mariamu Magdalene
limetajwa mara nyingi katika Biblia, na huyu ndiye aliyekuwa wa kwanza kukutana
na Yesu baada ya kukufuka. Mwanamke huyu ndiye aliyekwenda kuwapasha habari
mitume kuwa Yesu Kristo amefufuka. Tunafahamu kuwa alikuwa tajiri kwenye kitabu
cha Luka 8:1-3 “…waliokuwa
wakimhudumia Yesu kwa mali zao” inawezekana mtu, alishapewa neema ya kupata
utajiri tangu alipoumbwa; lakini pepo wabaya ambao mtu huyo umetumiwa wanaweza
kuchelewesha utajiri huo. Marko 15:40-41,
Mariamu Magdalene alipotolewa pepo wabaya akapata utajiri na kwa utajiri huo
akamtumikia Mungu.
Marko 16:1-8; Mariamu Magdalene ndiye
aliyeendelea kumhudumia Yesu kwa fedha baada ya kutolewa pepo saba. Kumbe
inawezekana ulipangiwa uwe tajiri wa kuwezesha kazi ya Mungu au wa kuwasaidia
watu lakini shetani amekuchelesha na kukufanya uwe maskini.
Yesu aweza kukuokoa:
Ni kweli kuwa
kuna watu wamecheleweshwa kimasomo, kimaendeleo, kiajira au kimahusiano. Na wengine
wanaishi kwenye matatizo kwasababu ya kucheleweshewa kesho yao lakini ni muhimu
kujua kuwa Yesu Kristo aweza kukuokoa kutoka katika kesho iliyocheleweshwa na
kukuweka huru. Kama vile alivyomwokoa Mariamu Magdalene ndivyo atakavyokuokoa
nawe. Uwe huru katika Jina la Yesu.
Kwa matukio zaidi na Picha bonyeza hapa: Facebook Page
0 Comments