google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

PATA MAARIFA YA NAMNA YA KURUDISHA AKILI YAKO ILIYOIBWA NA WACHAWI.


JUMAPILI YA TAREHE 14/09/2014

NA MCHUNGAJI KIONGOZI: JOSEPHAT GWAJIMA

SOMO: AKILI ILIYOLOGWA

NENO LA MSINGI: Wagalatia 3:1

Mchungaji kiongozi Josephat Gwajima.
1 Enyi Wagalatia msio na akili, ni nani aliyewaloga, ninyi ambao Yesu Kristo aliwekwa wazi mbele ya macho yenu ya kuwa amesulibiwa? 

Kumbe inawezekana mtu akalogwa akili yake bila kujua.

Musa alipotaka kutengeneza hema ya kukutania Mungu alimwelekeza kwa mtu mwenye akili  ya kuitengeneza hiyo hema.

Kutoka 35

30 Kisha Musa akawaambia wana wa Israeli, Angalieni, Bwana amemwita kwa jina lake Bezaleli mwana wa Uri, mwana wa Huri, wa kabila ya Yuda;
31 naye amemjaza roho ya Mungu, katika hekima, na akili, na ujuzi, na kazi ya ustadi kila aina;
32 na kuvumbua kazi za werevu, na kufanya kazi ya dhahabu, na fedha, na shaba,
33 na kukata vito vya kutilia, na kuchora miti, atumike katika kazi za werevu kila aina.
34 Naye amemtilia moyoni mwake ili apate kufundisha, yeye, na Oholiabu mwana wa Ahisamaki, wa kabila ya Dani.
35 Amewajaza watu hao akili za moyoni, ili watumike katika kazi kila aina, ya mwenye kuchora mawe, na kazi ya werevu, na ya mwenye kutia taraza, katika nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na nyekundu, na kitani nzuri, na ya mwenye kufuma nguo; ya hao wafanyao kazi yo yote, na ya wenye kuvumbua kazi za werevu.

Mchungaji mwandamizi Grace Gwajima
Maandiko matakatifu yanaonyesha kuwa akili za Mungu hazichunguziki na watu waliookoka kama watoto wa Mungu wanatakiwa watumie akili zao. Maandiko pia yanasema Mungu ni Mungu mwenye nguvu msifuni kwa akili; kumbe hata kumsifu Mungu kunahitaji  akili. Leo Mungu afungue akili yako  ili maisha yako pia yafunguke kwa kuwa kuna baadhi ya majibu kuhusu maisha yako yamo kwenye akili zako.

Wachawi wanatuonea wivu kwamba tuna akili ambayo ndani yake tunapata baadhi ya majibu kuhusu maisha yetu. Hatuhitaji kumuomba Mungu kwa habari ya mambo hayo wala kumtegemea mtu mwingine.  Ukimtegemea mtu utakufa masikini ndio maana Paulo anawaandikia wagalatia kwamba enyi wagalatia msio na akili ninani aliyewaloga? Akili zilizorogwa pia zinaitwa akili zilizotiwa giza.

Waefeso 4

17 Basi nasema neno hili, tena nashuhudia katika Bwana, tangu sasa msienende kama Mataifa waenendavyo, katika ubatili wa nia zao;
18 ambao; akili zao zimetiwa giza, nao wamefarikishwa na uzima wa Mungu, kwa sababu ya ujinga uliomo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao;
19 ambao wakiisha kufa ganzi wanajitia katika mambo ya ufisadi wapate kufanyiza kila namna ya uchafu kwa kutamani.
20 Bali ninyi, sivyo mlivyojifunza Kristo; 


 
 

Mungu alipomuumba mtu alimuumba katika vipande vitatu;

1.Roho

2.Mwlili

3.Nafsi  kuna kitengo cha nia ambapo mtu anajaza elimu. Pia kuna eneo la hisia na  utashi. Pia kuna eneo la akili. Ndio maana unaweza kukuta  ambaye hajasoma lakini ana mafanikio makubwa.

 Farao alipotaka kushindana na Musa aliwaita watu wenye akili, wachawi na waganga. Hii inatuonyesha kwamba kumbe wenye akili ni tofauti na wachawi na waganga. Nebukadreza naye alikuwa anaita wenye akili, wachawi, na waganga sababu alikuwa anajua akili inaweza kutumika kama uchawi utashindwa. Kila mtu unayemwona amepewa akili na Mungu, wapo watu ambao hutuma mashetani ili kufunga akili za watu wengine. Hapo ndio unakuta mtu anashindwa kufanya jambo kwasababu akili zake zimefungwa.  Akili  ni jambo la muhimu sana kwenye maisha ya mtu. Mungu amekupa akili za kumtosha mkeo na familia  yako. Zinapokuwa nyingi kulitosha taifa ndipo unapofaa kuwa kiongozi. Leo kuna viongozi ambao wana akili zisizowatosha hata wao wenyewe.

Shetani sio muumbaji bali yeye huiba na kutumia vibaya vitu alivyoumba Mungu. Hivyo wachawi ambao ni wakala wa shetani wanaweza kuiba akili aliyokuwekea Mungu na kukuwekea jini au pepo kuja kukaa ndani yako. Hapo ndipo utakuta kama wewe ni mwanafunzi ukiingia darasani huelewi.  Akili yako imerogwa.

Zaburi 147

5 Bwana wetu ni mkuu na mwingi wa nguvu, Akili zake hazina mpaka.
6 Bwana huwategemeza wenye upole, Huwaangusha chini wenye jeuri. 

2Samweli 14: 2 Yoabu akatuma watu waende Tekoa, akaleta kutoka huko mwanamke mwenye akili, akamwambia, Nakusihi, ujifanye kama unakaa matanga, ukavae nguo za kufiwa, nakusihi, wala usijitie mafuta, ila ukafanane na mwanamke aliyeomboleza siku nyingi kwa ajili yake aliyefariki;

20 mtumwa wako Yoabu ameyatenda haya ili kubadili uso wa jambo hili; na bwana wangu anayo akili, kama akili ya malaika wa Mungu, hata ajue mambo yote ya duniani.

Yoabu anasema mfalme Daudi anayo akili kama ya malaika wa Mungu kujua mambo. Kumbe hata malaika nao wana akili. Mfalme kabla hajafa akamwambia mwanae Suleiman amtendee kwa akili Yoabu, aliyekuwa mkuu wa majeshi ili aweze kutawala vizuri. Daudi alipofariki Sulemani alishika madaraka akijua kuwa anatakiwa  kumtendea kwa akili Yoabu. Siku moja Suleiman akaagiza aitiwe Yoabu; Yoabu akaogopa akijua  mfalme anataka kumuua akakimbilia hekaluni kushikilia pembe ya madhabahu. Kwa desturi za wayahudi wakati ule kumuua  mtu aliyeshikilia pembe ya madhabahu ni laana. Yoabu akaenda kushika kwenye madhabahu ya Bwana akisema nitafia hapahapa kwenye madhabahu ya bwana.  Mfalme akasema kwa kuwa amesema atafia kwenye madhabahu basi muueni kama alivyosema, Yoabu akala matunda ya kinywa chake.

Yesu akasema, “ mpende bwana Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa akili yako yote.”  Kumbe hata Bwana anapendwa kwa akili zetu. Kina Shedrack, Meshack, na Abednego walichukuliwa ili walishwe vizuri na kulelewa vizuri ili akili zao zitumike. Jambo lilipokuwa likitokea walikuwa wanafuatwa kutoa ufafanuzi kwa akili zao. Biblia inasema mwana wa Adamu amekuja naye ametupa akili.
Maelfu wakiwa wanaita akili zao.

Utakuta mtu anaangalia televisheni kuanzia asubuhi mpaka jioni halafu analalamika serikali haiangalii watu wa chini, akili yake imelogwa. Utakuta mahali mtu kaanzisha biashara kesho mwingine anakuja pembeni yake na kuanzisha biashara ileile na mwingine na mwingine mpaka inafika hatua wote hawana wateja. Hawa watu wana tatizo na tatizo lao liko kwenye akili.

Shetani anapoona una akili na anaamua kuifunga akili yako. Unakutana na mtu anaishi maisha mabaya ukimuuliza anakwambia haina shida bora uzima. Au unakutana na mwanamke ukimuuliza anafanya kazi gani anakujibu ni mama wa nyumbani, ukiuliza kwa muda gani anajibu kwa ujasiri kwa miaka kumi. Ama unaongea na kijana wa miaka 50, hajaoa na haoni shida kusema bado anajipanga. Huyu akili zake zimelogwa.

Kuna wachawi wanaochukua akili ya mtu na kuitumia na mahali pa akili wanabakiza mashetani ambayo yanamfanya anakuwa na laana na mikosi.

 

Mithali 12

8  Mtu atasifiwa kwa kadiri ya akili zake; Bali mwenye moyo wa ukaidi atadharauliwa. 

Mtu anasifiwa kwa jinsi akili yake ilivyo. Mchawi anapochukua  akili  yako vile vitu unavyotakiwa  kuvifanya unashindwa. Utakuta mtu akianza kusoma kichwa kinauma au anasinzia kumbe  akili yake imechukuliwa na inatumiwa mahali fulani. Au  mtu ni mgonjwa lakini chanzo  cha ugonjwa wake ni akili kuchukuliwa.

Kama malaika wana akili na sisi lazima tuwe na akili kama Mungu ana akili na akili zake hazichunguziki kwa nini sisi tulio watoto wake tusiwe na akili? Lazima akili zetu zirudi kwa jina la Yesu.

Mtu mwingine anasema wameniloga nisipendwe, nisisafiri, nisipate kazi lakini sio kwamba wamekuloga wamechukua akili, mawazo unayowaza ndivyo ulivyo.na Wanafilosofia wanasema angalia sana unachokiwaza kuna siku utakisema. Angalia sana unachokisema kuna siku utakitenda. Angalia sana unachokitenda kuna siku kitakuwa tabia. Angalia sana tabia yako kuna siku itakuwa asili yako. Asili ya mtu hujalisha mwisho wake utakuwaje. Hebu jiulize hapo ulipo una mpango gani wa maendeleo? Utasema labda sina mpango kwa sababu sina mtaji. Lakini kwa kawaida unatakiwa uanze kuwa na mpango halafu ndipo upate mtaji ila kwa sababu akili yako imelogwa ndio maana unasubiri upate mtaji ndio upange mpango.

Akili yako inapolazwa ndio wale tunaowaita usingizi wa kiroho ingawa unaona lakini umelala usingizi kwenye akili. Huu sio wakati wa kushangilia ametajirika ni wakati wa kuwaza ameupata wapi utajiri ule. Si wakati wa kushangilia ameshinda uongozi, ni wakati wa kuwaza ameupata wapi uongozi ule. Lazima turudishe akili zetu zote zilizoibiwa kwa jina la Yesu, ni wakati wa kuanza kuitumia akili yako ili kuinua familia yako,ni wakati wa kutumia akili tuliyopewa na Mungu kutimiza kusudi lake kwenye maisha yetu kwa jina la Yesu

Ndani yako unahisi unaweza kufanya zaidi ya hapo, ni kweli ila kuna mahali wameitafuna akili yako na wamekuloga ili waitumie mahali. Yamkini akili yako inatumika kuzaa watoto wa kijini baharini lakini akili hiyohiyo ingetumika kuwafanya watu waokoke. Wanapoiiba akili yako wanakuvisha akili ya uoga na kuondoa ile akili ya ujasiri uliyoumbiwa. Kataa uoga ulionao kwa jina la Yesu kwa sababu hiyo sio asili yako.

 

MAOMBI:

Kwa jina la Yesu mtu yeyote aliyechukua akili yangu akanifunga na magonjwa ninaamuru rudisha akili yangu kwa jina la Yesu; akili ya biashara, akili ya kusimamia miradi, akili ya kujenga kanisa, akili za kusafiri rudisha kwa jina la Yesu. Umenijia kwa uchawi nakujia kwa jina la Bwana wa majeshi, akili njooo kwa jina la Yesu.

Kwa jina la Yesu wale waliotafuna akili yangu ninawaamuru waitapike akili yangu kwa jina la Yesu . Akili yangu iliyofungiwa shimoni njoo kwa jina la Yesu, naishinda akili ya uoga kwa jina la Yesu. Kwa jina la Yesu naamuru akili yangu njoo, akili ya biashara, akili ya ubunifu, akili ya fedha,njoo kwa jina la Yesu. Mtu yeyote anayetumia akili yangu naamuru achia akili yangu kwa jina la Yesu, akili ya kuanza biashara , akili ya kufanya kazi, akili ya kubuni njoo kwa jina la Yesu. Napokonya akili kwa jina la Yesu, nakunyanganya akili yangu kwa jina la Yesu; uliyemeza akili yangu nakutapisha kwa jina la Yesu. Ewe mkurugenzi uliyemeza masomo yangu nakutapisha kwa jina la Yesu, ewe uliyemeza akili yangu ya ubunifu nakunyanganya kwa kwa jina la Yesu, akili ya kusafiri, akili ya kuongea, akili ya kutenda njoo kwa jina la Yesu. Akili iliyoko mapangoni, mashimoni, baharini njoo kwa jina la Yesu, akili ya miradi, akili ya kuanzisha makampuni, akili ya kumtumikia Mungu njoo kwa jina la Yesu. Rudisha akili yangu kwa jina la Yesu, akili inayotumiwa na majini kutengeneza bacteria na virusi wa magonjwa nashindana nanyi kwa jina la Yesu. Akili ya kubuni miradi akili ya kuita miradi, akili ya kuota kazi njooo kwa jina la Yesu. Akili ya kujua cha kufanya , akili ya kujua cha kutenda njoo kwa jina la Yesu. Ninaifungua akili yangu kwa jina la Yesu, ninawashambulia mashetani wote na wachawi wote mnaoishikiila akili yangu  kwa jina la Yesu, akili yangu inayotumika mahala popote  ninairudisha kwa jina la Yesu. Naondoa akili za kishetani na magonjwa yote yaliyowekwa ndani yangu kwa jina la Yesu, vifungo vya akili ninavifungua kwa jina la Yesu.

Ameni.

 

 

 

Post a Comment

0 Comments