JUMAPILI
YA TAREHE 30/11/2014
MCHUNGAJI
KIONGOZI JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO:
MIKONO YA KICHAWI/KISHETANI
Mchungaji kiongozi Josephat Gwajima. |
Biblia inasema;
“Mungu ni Roho, nao wamwabuduo
yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” Yohana 4:24
Lakini pamoja na kuwa
Mungu ni roho, Mungu anayo mikono na vidole pia.
“Na mche ule
ulioupanda Kwa mkono wako wa kuume; Na tawi lile ulilolifanya Kuwa imara kwa
nafsi yako.” Zaburi 80:15
“Miongoni mwao
waliokufa nimetupwa, Kama waliouawa walalao makaburini. Hao ambao Wewe
huwakumbuki tena, Wametengwa mbali na mkono wako.” Zaburi 88:5
“Lakini, ikiwa mimi
natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha kuwajilia.” Luka11:20
Mkono wa Bwana
hutumika kuokoa, kubariki na kuponya wanadamu.
“Bwana atawapa watu wake
nguvu; Bwana atawabariki watu wake kwa amani.” Zaburi 29:11
Yesu alipokuwa akiwaambia
wanafunzi wake anatoa pepo kwa kutumia kidole cha Mungu alikuwa anamaanisha anatoa pepo kwa uwezo wa Roho
mtakatifu. Roho Mtakatifu ndiye kidole
cha Mungu. Leo hii Mungu hutenda kazi kupitia mikono ya mawakala wake duniani
ambao ni wachungaji na watumishi wengine wa Mungu aliye hai. Ndio maana watu
wengi wanapomwabudu Mungu huimba wakisema, “Mungu niguse, niguse Bwana.” Watu
hawa huguswa na Mungu kupitia watumishi wa Mungu waliojaa nguvu za Roho
Mtakatifu.
Kama ambavyo Mungu
ana mikono na vidole; shetani naye ana mkono wake na kidole chake.
“Kisha Bwana
akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana
mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu
na kuepukana na uovu. Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Je! Huyo Ayubu
yuamcha Bwana bure? Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba
yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali
yake imeongezeka katika nchi. Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote
aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako. Bwana akamwambia Shetani,
Tazama, yote aliyo nayo yamo katika uwezo wako; lakini usinyoshe mkono wako juu
yake yeye mwenyewe. Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana. Ilitukia siku
moja hao wanawe na binti zake walipokuwa wakila na kunywa divai katika nyumba
ya ndugu yao mkubwa, mjumbe akamfikilia
Ayubu na kumwambia, Hao ng'ombe walikuwa wakilima, na punda walikuwa wakilisha
karibu nao; mara Waseba wakawashambulia,
wakawachukua wakaenda nao; naam, wamewaua hao watumishi kwa makali ya upanga,
mimi peke yangu nimepona, mimi tu, kukuletea habari. Huyo alipokuwa akali akinena, akatokea na
mwingine, na kusema, Moto wa Mungu umeanguka kutoka mbinguni na kuwateketeza
kondoo, na wale watumishi, na kuwaangamiza; mimi peke yangu nimepona, mimi tu,
kukuletea habari. Huyo alipokuwa akali
akinena, akatokea na mwingine, na kusema, Wakaldayo walifanya vikosi vitatu,
wakawaangukia ngamia, wakaenda nao, naam, wamewaua wale watumishi kwa makali ya
upanga; mimi peke yangu nimepona, mimi tu, kukuletea habari. Huyo alipokuwa akali akinena, akatokea na
mwingine, na kusema, Wanao na binti zako walikuwa wakila na kunywa divai katika
nyumba ya ndugu yao mkubwa; mara,
tazama, upepo wenye nguvu ukatoka pande za jangwani, ukaipiga hiyo nyumba pembe
zake nne, nayo ikawaangukia hao vijana, nao wamekufa; na mimi peke yangu
nimepona, mimi tu, kukuletea habari. Ndipo Ayubu akainuka, akalirarua joho
lake, kisha akanyoa kichwa chake, na kuanguka chini, na kusujudia; akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu
nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; Bwana alitoa, na Bwana
ametwaa; jina la Bwana na libarikiwe.” Ayubu
1:8-21
Tunajifunza hapa kuwa
mtu anayependwa na Mungu ni yule mtu mkamilifu, mwelekevu, mweye kumcha Mungu
na mwenye kuepuka uovu. Mungu hujivunia mtu wa namna hii.
Shetani anamwambia
Mungu kwamba Ayubu anamcha kwasababu amembariki na kumwekea ulinzi. Mungu
akampa ruhusa shetani anyooshe mkono wake juu ya vyote alivyo navyo Ayubu
lakini asiuguse uhai wake. Shetani pia kama ambavyo Mungu alivyo na mawakala
duniani; yeye pia anao. Hawa ndio wachawi na waganga. Hivyo shetani anapotaka
kukugusa atakugusa kupitia wao.
Kuna watu ambao wana
matatizo kwasababu wameguswa na mkono wa kichawi bila wao kujua. Kama ambavyo
Ayubu alianza kupatwa na matukio baada ya shetani kupata kibali cha kumgusa
ndivyo inavyokuwa kwa mtu anayeguswa na mikono ya kichawi leo. Shetani
aliponyoosha mkono wake tu, wakatokea waseba (wezi) wakaiba mifugo na kuondoka
nao. Ayubu hakuwa peke yake mwenye mifugo lakini wengine hawakuibiwa ila yeye.
Kwa nini? Mkono wa shetani umemgusa. Baada ya kuguswa kila eneo la maisha yake Ayubu
alianza kuchanganyikiwa. Kumbe unapoguswa na mkono wa shetani unaanza
kuchanganyikiwa pia. Ayubu akaishia kumshukuru Mungu akisema Bwana alitoa Bwana
ametwaa jina lake libarikiwe. Lakini mimi ni wewe ni mashahidi leo kuwa ni
kweli Bwana alitoa kwa Ayubu lakini si kweli alitwaa tena alivyotoa.
Aliyevitwaa alikuwa shetani. Kumbe yawezekana kabisa kuwa ulipewa vitu na Bwana
lakini mkono wa kichawi ukavigusa na kuvitwaa.
Lakini lihimidiwe jina la Bwana
kwa kuwa ipo mikono ya watumishi wa Mungu wa kweli itumikayo kugusa na
kurudisha vyote ambavyo waseba walikuwa wameiba.Imeandikwa
“watashika
nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono
yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.” Marko 16:18
Sisi tunaomtumikia
Mungu tumepewa mamlaka ya kuweka miono yetu juu ya wagonjwa, walioibiwa,
walioteswa na kuwarudishia afya zao na vyote walivyoibiwa na yule aliyekuja
kuiba na kuharibu yaani shetani.
Inawezekana leo
unapitia balaa na mikosi mbalimbali kwenye maisha yako ambayo chanzo chake ni
kushikwa na mikono ya kichawi. Yamkini hawakuweza kukushika wewe lakini walishika
nguo yako au kiatu chako au kitu chako chochote; na kwa kadri ambavyo
unaendelea kukaa na kile kitu nyumbani kwako kinakuwa kiunganishi kati yako na
ile laana au mkosi. Ni lazima ukate kile kinachokuungamanisha na yale matatizo
yatokanayo na ile mikono ya kichawi..
Kila unapoamka,
unapoomba unatakiwa uombe damu ya Yesu itakase mikono yako, uso wako na mwili
wako kwa ujumla. Haupaswi kuwaogopa na
kuwakwepa, unatakiwa upambane nao kwa jina la Yesu. Kila aliyegusa nguo yako
kwenye ulimwengu wa roho leo mrudishie vyote alivyokuwekea kwa jina la Yesu.
Ruhusa uguswe na mkono wa Mungu kabla mikono ya kichawi haijakugusa, ukiguswa
na Mungu ile nguvu inaingia mpaka kwenye mifupa
ndani ya mwili wako. Hapo nguvu ya mikono ya kichawi haitoweza
kufanikiwa tena juu yako.
Maombi
Mikono ya wachawi
waliowahi kugusa mikono yangu, nguo zangu, chakula change, mali zangu zote;
kuanzia sasa kwenye ulimwengu wa roho ninafuta alama zao kwa jina la Yesu.
Mikono ya kichawi
iliyogusa vitu vyangu, mwili wangu au kitu chochote ninavifuta kwa jina la
Yesu. Alama za kichawi zilizoachwa ndani ya nguo zangu ninazifuta kwa damu ya
Yesu. Mikono ya kichawi iliyogusa ndoa yangu, familia yangu, kazi yangu ninaiamuru
kwa jina la Yesu ivunjike. Ninanyoosha mkono wa Mungu kuivunja na kuiteketeza
mikono ya kishetani iliyonyooka juu ya maisha yangu; ninaivunja kwa jina la
Yesu Kristo. Imeandikwa
“nao wakamshinda kwa damu ya mwana kondoo” Ufunuo12:11
Kila mchawi aliyenyoosha
mkono wake juu ya mwili wangu, nguo zangu, kichwa changu, kanisa langu, nchi
yangu, ndoa yangu, ninaipoozesha kwa damu ya mwana kondoo.
Kila mkono wa
kishetani ulionyooka ili kuleta maangamizo juu yangu, ninaupoozesha na kuuvunja
kwa jina la Yesu Kristo. Ninatuma polio kwenye mikono yote ya kichawi
iliyojipanga kugusa watoto wangu, biashara yangu, elimu yangu. Ninaipoozesha
kwa damu ya Yesu Kristo, ninaivunja kwa jina la Yesu Kristo. Kila kazi
iliyoanzishwa na mikono ya kishetani ninaibatilisha kwa jina la Yesu Kristo.
Ninaamuru kwa mamlaka ya jina la Yesu, kila mkono wa kichawi ulionyooka kunigusa
mimi na familia yangu upooze kwa damu ya Yesu Kristo. Ninaifyeka kwa jina la
Yesu Kristo.
Mikono inayoleta
utasa ninaivunja kwa jina la Yesu. Ewe mkono ulionyooka kuleta utasa kazini
kwangu, utasa kwenye elimu ninakuvunja kwa jina la Yesu Kristo. Kila mkono wa
kichawi uliotumwa kunigusa mimi na vyote nilivyonavyo leo ninakuvunja kwa jina
la Yesu Kristo. Ewe shetani uliyenyoosha mkono wako kuniletea uoga wakati wa
usiku na hofu wakati wa mchana leo ninakuvunja kwa jina la Yesu Kristo. Kila
mkono ulionyooka juu ya watoto wangu, wazazi wangu, rafiki zangu, na ndugu
zangu wote leo ninaondoa uweza wako wa kudhuru na kukuvika polio upooze, ninakufyeka
kwa jina la Yesu Kristo. Ninaukata mkono ulionyooshwa ili nisiolewe kwa jina la
Yesu. Ninaukata mkono ulionyooshwa ukagusa nguo zangu, mali yangu au chochote nilicho
nacho kwa jina la Yesu; ninaukata mkono ulionyooshwa kugusa ajira yangu kwa
jina la Yesu. Ninaukata mkono wa wachawi ulionyooshwa kugusa mapato yangu kwa
jina ya Yesu. Mchawi mwanaume, mtoto, mwanamke, mzee ninaukata mkono wako
uliounyoosha kunigusa mimi na mali zangu kwa jina la Yesu Kristo. Amina!
0 Comments