google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

VITA YA KUMILIKI YALE ULIYOPEWA NA MUNGU.

UFUFUO NA UZIMA UBUNGO CATHEDRAL 
IBADA YA JUMAPILI 2 APRILI 2023 
ASKOFU BARAKA THOMAS TEGGE 
SOMO: VITA YA KUMILIKI YALE ULIYOPEWA NA MUNGU.

Usipofahamu namna ya kumiliki yale ambayo Mungu amekupa kamwe hutawezi kuyapata. Mungu alishakupa mambo yote yakukufikisha kwenye hatima yako na Mungu huwa hadanganyi. Mungu anapokuahidi jambo kuna kuwa na agano kati yake na aliyemuahidi na kila upande kwenye agano kuna sehemu lazima itimize. Mungu anakupa kila kitu lakini kuna sehemu lazima uifanye wewe la sivyo hutaweza kupata yale uliyopewa. Mungu alivyokuwa anawaongoza wana wa Israeli kuna mataifa mengine alikuwa anawaambia waacheni kwa kuwa hajawapa, ila kuna nchi na mataifa ambayo Mungu aliwapa. 

“Ikawa baada ya kufa kwake Musa, mtumishi wa BWANA, BWANA akamwambia Yoshua, mwana wa Nuni, mtumishi wa Musa, akasema, Musa mtumishi wangu amekufa; haya basi, ondoka, vuka mto huu wa Yordani; wewe na watu hawa wote, mkaende hata nchi niwapayo wana wa Israeli. Kila mahali zitakapopakanyaga nyayo za miguu yenu, nimewapa ninyi, kama nilivyomwapia Musa. Tangu jangwa hili na mlima huu, Lebanoni, mpaka mto ule mkubwa, mto wa Frati, nchi yote ya Wahiti, tena mpaka bahari ile kubwa upande wa machweo ya jua, hapo ndipo patakapokuwa mpaka wenu. Hapatakuwa mtu ye yote atakayeweza kusimama mbele yako siku zote za maisha yako; kama nilivyokuwa pamoja na Musa, ndivyo nitakavyokuwa pamoja na wewe; sitakupungukia wala sitakuacha.” Yoshua 1:1-5.

Lazima kuwe na mtu wa kukurithisha yale ambayo Mungu amekupa, Yoshua alikuwa na kazi ya kuwarithisha wana wa Israeli nchi ya ahadi, ambayo Mungu aliyowaapia Baba zao. Wana wa Israeli walikuwa ni kana kwamba wanahama hama ila kuna nchi waliyokuwa wanaiendea ambayo Mungu aliwapa. Vivyo hivyo pia kuna mtu anaweza kuonekana kana kwamba hana kitu, ana madeni, tabu n.k ila anakuwa njiani kuelekea pale ambapo Mungu kamuandalia. 

Pamoja na ahadi waliyopewa na Mungu ya kumiliki nchi ya ahadi, wana wa Israeli waliacha sehemu kubwa sana ambayo hawakuwa wameimiliki. Ahadi ya Mungu ni kweli na hakika lakini kama usipopigana Mungu hana la kukusaidia.

“Basi Yoshua alipokuwa mzee, na kwendelea sana miaka yake, BWANA akamwambia, Wewe umekuwa mzee na kwendelea sana miaka yako, kisha inasalia nchi nyingi sana bado kumilikiwa.” Yoshua 13:1.

Kuna nchi kubwa sana ilisalia bila kumilikiwa na wana wa Israeli, baadhi ya makabila wakawa wanakaa kwenye nchi za wenzao. Ulegevu ulipelekea haya yote kutokea.

“Kisha mkutano mzima wa wana wa Israeli walikutana pamoja hapo Shilo, wakasimamisha hema ya kukutania kuko; nayo nchi ilikuwa imeshindwa mbele zao. Zilisalia katika wana wa Israeli kabila saba ambazo hazijagawanyiwa bado urithi wao. Yoshua akawauliza wana wa Israeli, akasema, Je! Hata lini mtakuwa walegevu katika kuingia kwenu na kuimiliki hiyo nchi, ambayo yeye BWANA, Mungu wa baba zenu, amewapa?” Yoshua 18:1-3.

Ilibidi wawaendee waliokuwa wamekaa kwenye nchi ya ahadi na kupigana nao ili wamiliki nchi ambayo Bwana aliwapatia. Yoshua hakwenda kuwapigania, walienda wenyewe kupigana. Wale unaodhani watakuja kukupigana, huo ulegevu utakufanya ushindwe kuimiliki.

“Wakasema, Haya, inukeni, twende tukapigane nao; kwa maana tumeiona hiyo nchi nayo ni nchi nzuri sana; nanyi, je! Mwanyamaa tu? Msiwe wavivu kwenda, na kuingia, ili mpate kuimiliki nchi hiyo.” Waamuzi 18:9.

Ili umiliki kwenye agano jipya hakuna utofauti sana na agano la kale, ni lazima upigane na majeshi ya shetani kwenye ulimwengu wa roho. Sheria ya kumiliki alichokupa/ kuahidi Mungu ni lazima upigane kila wakati pasipo kuchoka. 

“Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani; zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu. Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu; kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote;” Waefeso 6:10-18.

Mambo ya kuzingatia kuhusu Mungu na kumiliki. 

  • Kuyafahamu mawazo ya Mungu.

Kuna mawazo ambayo Mungu anayo kwa ajili ya kila mtu. Kila mtu kuna hatima kupewa na Mungu. Kuna mawazo ya Mungu kwenye kila hatua na mambo ya maisha yako.

“Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema BWANA, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.” Yeremia 29:11.

  •  Njia za Mungu.

Njia za Mungu ni kwa namna gani mtu apate yale ambayo Mungu amemuwazia (ahadi za Mungu).

  •  Wakati wa Mungu. 

Mungu anawakati wake wakukufanyia jambo fulani, usiposubiri wakati wa Mungu kwa haraka zako utaharibu na kukosea.

“Mdogo atakuwa elfu, Na mnyonge atakuwa taifa hodari; Mimi, BWANA, nitayahimiza hayo wakati wake.” Isaya 60:22.

Mambo haya kuhusu kumiliki, ili wewe uyafahamu lazima roho mtakatifu akuelekeze. 

“Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu. Maana ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu.” 1 Wakorintho 2:10-11.

Vita ya kumiliki ipo kwenye nafsi na utashi maana huo ndio uwanja wa shetani. Roho mtakatifu atakujulisha mawazo, njia na wakati wa Mungu lakini shetani atakuletea vita kwenye mawazo ili ushindwe kuamini yale aliyokuonyesha roho mtakatifu.

Mawazo haya ya shetani yanaweza kuwa kupitia watu wako wa karibu na unaowaamini ambapo shetani atawavuvia na kuwatumia wakushauri kinyume na mawazo, njia na wakati wa Mungu ili ushindwe kuchukua hatua kuelekea hatima uliyopewa na Mungu. Petro alitumika na shetani ili ajaribu kumzuia Yesu kutimiza kusudi lake alipewa na Mungu.

“Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka. Petro akamchukua, akaanza kumkemea, akisema, Hasha, Bwana, hayo hayatakupata. Akageuka, akamwambia Petro, Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.” Mathayo 16:21-23.

Hekima ya kibinadamu ndio mawazo ya shetani, ambayo lazima yawe kinyume na mawazo ya Mungu. Kuna muda hekima ya shetani inaonekana ni bora ila dhumuni lake ni kuzuia kusudi na mawazo ya Mungu juu yako.

“Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani.” Yakobo 3:15. 

Kuna mambo ya Mungu hutafanya kama utasikiliza ushauri wa kila mtu. Paulo anasema injili aliyopewa haikuwa kwa namna ya kibinadamu na wala hakufanya shauri na wanadamu ili ahubiri.

“Kwa maana, ndugu zangu, injili hiyo niliyowahubiri, nawajulisha ya kuwa siyo ya namna ya kibinadamu. Kwa kuwa sikuipokea kwa mwanadamu wala sikufundishwa na mwanadamu, bali kwa ufunuo wa Yesu Kristo.” Wagalatia 1:11-12.

“alipoona vema kumdhihirisha Mwanawe ndani yangu, ili niwahubiri Mataifa habari zake; mara sikufanya shauri na watu wenye mwili na damu;” Wagalatia 1:16.

Na kufuata mawazo na njia za Mungu haimaanishi kwamba umiliki wako utakuwa mwepesi Hapana. Mawazo na njia za Mungu zinaweza kuwa ngumu lakini huko ndipo kwenye umiliki wako na lazima upigane. 

"BONYEZA HAPA KUANGALIA IBADA NZIMA YA JUMAPILI"

Post a Comment

0 Comments