IBADA YA JUMAPILI 21 APRIL 2024
ASKOFU DKT JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO: KUSUDI LA MUNGU KATIKA KIZAZI CHAKO
Kila mtu unayemuona
anaisha duniani lipo kusudi la Mungu katika maisha yake, na kusudi la Mungu
haliwezi kuzuiwa na mtu, kila juhudi ya kuzuia kusudi la Mungu kwenye maisha
yako hiyo ndiyo hatua ya kuliwahisha, na litatokea kwa wepesi zaidi kuliko
lilivvyokusudiwa.
“Mna hila nyingi moyoni mwa mtu; Lakini shauri la BWANA ndilo litakalosimama.” mithali 19:21
Mahali popote ulipo liko shauri la Mungu nalo litasimama.
"Kwa maana Daudi, akiisha kulitumikia shauri la Mungu katika kizazi chake, alilala, akawekwa pamoja na baba zake, akaona uharibifu." Matendo 13:36
Mungu
ni Mungu wa makusudi na kila alichokiumba kina makusudi, Mungu ameweka kusudi
juu ya kila mtu, na mtu kwa kadri anavyoishi anazidi kulitumikia kusudi, kusudi
lako likiisha unalala, kama kusudi halijaisha hauwezi kufa. Kila aluiyezaliwa ana kusudi la Mungu na
anayeshindana na wewe anashindana na kusudi la Mungu na ashindanaye na Bwana
atapondwa kabisa.
“Washindanao
na BWANA watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; BWANA
ataihukumu miisho ya dunia; Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe
ya masihi wake.” 1 samweli 2:10
Kusudi huwa haliondoki hata kama umekosea, Mungu akikupa amekupa na ndio maana unaona wanamuziki wa ki-dunia wanaimba kwenye ufalme wa shetani ila Mungu hawezi kuwanyang`anya atakutana nao siku ya wisho.
Mungu akikupa amekupa, wanadamu wakikupa ukiwaletea matatizo wanakunyang`anya, unapokwenda na mtu angalia kusudi la Mungu kwanza kwa maana kusudi la Mungu haliwezi kuzuiwa na mtu.
Kuna watu leo unaona hawafai kumbe Mungu ameweka kusudi ndani yao, kuna muda utafika wale uliowanenea mabaya utaona wapo juu ya Mlima.
“na
Salmoni akamzaa Boazi; na Boazi akamzaa Obedi; 22na Obedi akamzaa Yese; na Yese
akamzaa Daudi.” Ruthi 4:21
“Kitabu
cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu. Ibrahimu alimzaa
Isaka; Isaka akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yuda na ndugu zake; Yuda akamzaa
Peresi na Zera kwa Tamari; Peresi akamzaa Esromu; Esromu akamzaa Aramu; Aramu
akamzaa Aminadabu; Aminadabu akamzaa Nashoni; Nashoni akamzaa Salmoni; 5Salmoni
akamzaa Boazi kwa Rahabu; Boazi akamzaa Obedi kwa Ruthu; Obedi akamzaa Yese; Yese
akamzaa mfalme Daudi. Daudi akamzaa Sulemani kwa yule mke wa Uria.” Mathayo 1:1-6
Unaweza kuwa hapa namna yako ya kuzaliwa ilikuwa ya ajabu ajabu lakini kusudi la Mungu kwako halibadiliki.
“na Yese akamzaa Eliabu, mzaliwa wake wa kwanza, na wa pili Abinadabu, na wa tatu Shama; na wa nne Nethaneli, na wa tano Radai; na wa sita Ozemu, na wa saba Daudi;” 1 Nyakati 2:13-15
Mungu
anapokuitia jambo, anakupaka mafuta kwenye jambo hilo, hata kama unaona muda
umeisha lakini litatimia, kuna watu wako
hapa ila si wa hapa yani wewe kuna nyumba yako Canada mahali lakini wewe hujijui, kazi yako
iko Uingereza mahali.
Yule unayemuona hayuko sawa ndio kusudi la Mungu linawekwa ndani yake, kwenye familia yako muangalie sana asiyependwa, anaweza kuwa na kitu, Mungu ana kawaida akikuchagua anaruhusu udharauliwe ili ukifanikiwa watu washangae, kuna hatua polopole zitaanza za kusababisha uingie kwenye kusudi mahali unapotakiwa kuingia, kuna ufunguo uko mbele yako, Mungu akiwa na kusudi na wewe anakupa vifaa vya kuvitumia kwenye kusudi lako.
Kuchaguliwa na Mungu haimaanishi kwamba watu watakupenda lakini kusudi la Bwana litasimama wapo watu wanapitia magumu wanajiuliza watatokaje, kuna wakati unafika utatoka , yale unayoyaona ni ya muda tu utatoka, kuna mambo Mungu anakuinulia ili uyatandike, ili uweze kungia kwenye nafasi nyingine, Mungu anaweza kuruhusu jambo fulani gumu, usilikwepe tunisha msuli useme hapo ndipo nitakapoinukia, ukiona fitina imezidi, maneno yamezidi, pesa hakuna, ujue unakaribia kupenya hapo, ukimuona Goliathi cheka kwanza maana bila Goliathi Daudi anabakia pale, kama huna Goliathi kwenye maisha yako, mbele yako hakuna kitu.
Goliathi anaweza kuwa madeni, kuna watu wamezima simu si kwa sababu wapo kwenye ibada ila ni kwa sababu wanadaiwa,
mwenye kusudi ndani yake hawezi kukosa madeni lakini si kwamba Mungu amekuacha
anakupeleka mahali alikokupangia, hali yako ya leo haimaanishi ndio hali yako
ya kesho, kila unaloliona lina makusudi
Mungu
akitaka kufanya jambo anasababisha tukio ili akubebe wewe, Mungu anasababisha
tukio ili uanze kwenda.
Nyuma
ya kila kuinuliwa yuko Goliathi, wapo watu ambao hatima yao imeunganishwa na
hatima yako, hatima ya Daudi ilikuwa imeungana na ya Nathaniel. `
Kusudi la Mungu haliwezi kuzuiwa na mtu, ukiwa una tatizo leo haimaanishi kwamba Mungu amekuacha , Mungu anaruhusu shida ili akunoe, Mungu akitaka kukuinua anaweza kusababisha jambo fulani, wanakusingizia jambo kumbe ndio wana kupeleka kwenye hatima yako. Watu wanaweza kukusemea mabaya ipo siku Mungu atakuinua na hali yako hiyo hiyo.
Usishindane
na mtu ambaye kusudi la Mungu liko kwenye maisha yake, ukiwa na wito wa Mungu
wewe hujijui ila tu unakuwa unaona mbona mimi nampenda sana Mungu, kusudi la Mungu
ni la watu wote. Kila jambo linalopangwa yupo mtu amaendaliwa na Mungu
atakuokoa, hauwezi kufa mpaka kile ulichopewa na Mungu kitimie kwenye maisha
yako.
Mtu
unayempenda zaidi, unayemuamini, unayemsaidia ndio atakuwa wa kwanza kukusaliti, lakini
mwisho wao wote watapondwa watasagwasagwa, hatari unazokutana nazo haziondoi
kusudi la Mungu ndani yako, Mungu akikupenda hakupi hela maana zinaweza
zikaisha, hakupi nyumba maana inaweza kuungua, hakupi gari maana linaweza
kupata ajali, Mungu akikupenda anakupa Neno ukilishikilia Neno unapata vyote,
hautakufa mpaka utimize mambo yako yote kwa jina la Yesu.
Mungu
akiwa na mpango na wewe wanaokutafuta ni wengi, ila usiogope Mungu yupo pamoja na
wewe hatakuacha mpaka kusudi lako litakapotimia hakuna hata jambo moja ambalo
halitatimia kwenye maisha yako.
Kila mtu ukimuangalia
unatakiwa ujiulize hivi huyu atakuwa
nani, wangekuwa wanajua Daudi atakuwa Mfalme wangekuwa na urafiki nae, uwe na
uwezo wa kuona rohoni hazina iliyojificha ndani ya watu na uwapende si kwa sababu
ya vitu bali kwa ajili ya hazina iliyoko ndani yao.
Juu yako liko kusudi la Mungu na halitazuiwa na magonjwa, na ajali mpaka liweze kutimia, wako adui zako wanaweza kukuzuia, kusema maneno mabaya juu yako ili usipige hatua, pigana nao uwamalize wakati wa uhai wako, utakayembakiza atakuwa adui wa wanao, Naamuru kuanzia leo kusudi la Mungu lisimame juu yako kwa jina la Yesu.
BONYEZA HAPA KUTAZAMA IBADA NZIMA YA JUMAPILI
0 Comments