UFUFUO NA UZIMA
CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI
29.03.2026
ASKOFU DKT GERSHOM
MWAKILA
SOMO: MATUKIO KATIKA DAMU KWENYE
FAMILIA
![]() |
Familia ni kundi dogo ndani ya
jamii ambalo linatengeneza ukoo. Familia tofauti za damu moja zinatengeneza
ukoo, na koo tofauti tofauti zikikusanyika zinatengeneza makabila ambayo kwa
pamoja tunapata taifa.
Kila familia ina roho za familia
ambazo zinaweza kufanana au kutofautiana kati ya famila moja na familia nyingine.
Mfano wa roho za familia ni; roho za kukosa ndoa, roho za ugomvi, roho za damu,
n.k. kuna wataalamu kabisa wanaojihusisha na damu katika familia.
Kuna familia ambazo, kwa sababu ya
roho ya damu, hawajawahi kumiliki mali au kushika nafasi yoyote ya uongozi,
hata ile ndogo kabisa katika jamii. Damu husafiri kutoka uzao mmoja hadi uzao
mwingine ndani ya familia, vivyo hivyo matukio yanayoambatana na damu, mfano
magonjwa.
Kuna matukio ndani ya familia ambayo
yanawafuatilia wanafamilia. Matukio hayo yamezungumziwa katika Biblia Takatifu
na katika vyanzo vya kisayansi.
Sayansi inasema kuna mambo hutoka
kwa wazazi na kurithiwa na watoto, kwa mfano, rangi ya ngozi, kimo cha mtu, unene/wembamba
wa mtu, tabia, n.k. Mambo haya yote husafiri kwa njia ya damu.
Damu ina seli na ute ute. Damu ina
vitu visivyoonekana ambavyo kitaalamu vinaitwa vinasaba (DNA). Vinasaba ni
visafirishaji vya matukio kutoka uzao mmoja kwenda uzao mwingine. Mambo yote
yaliyotajwa juu yanarithishwa kwa njia ya vinasaba. Hivyo sayansi inakubaliana sawa
na Biblia kuwa mtoto anaweza kurithi tabia kutoka kwa mzazi.
“Baba zetu walitenda dhambi hata hawako; Na
sisi tumeyachukua maovu yao.” Maombolezo 5:7
-
Neno hili linatufundisha kuwa watoto wanabeba
maovu ya dhambi za wazazi wao.
“Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu
viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa
mlioupokea kwa baba zenu;” 1Petro 1:18
-
Watoto hupokea mwenendo kutoka kwa
wazazi wao. Mwenendo ni tabia.
Matukio ya ukoo huwafuata
wanaukoo kimya kimya kupitia damu. Mfano, mwenendo, muonekano na aina ya maisha
wanayopitia wanaukoo kutoka kizazi hadi kizazi.
Matukio Ambayo Biblia Imeyasema
Yamesafiri Kupitia Damu:
Biblia imetaja matukio mengi
katika koo tofauti tofauti ambayo yamesafiri kutoka uzao mmoja hadi uzao
mwingine.
1.
Tukio la uongo ndani ya familia.
i)
Familia ya Ibrahimu (Baba wa Imani)
Matukio katika familia ya
Ibrahimu ambayo yanatajwa ni; alioa mwanamke mzuri, hofu na uongo.
“Basi kulikuwa njaa katika nchi
ile; Abramu akashuka Misri, akae huko kwa muda maana njaa ilikuwa nzito katika
nchi. Ikawa alipokuwa karibu kuingia Misri, akamwambia Sarai mkewe,
Tazama, najua ya kuwa u mwanamke mzuri wa uso; basi itakuwa, Wamisri
watakapokuona watasema, Huyu ni mkewe; kisha wataniua mimi na wewe watakuacha
hai. Tafadhali useme, wewe u ndugu yangu, iwe heri kwangu kwa ajili yako,
na nafsi yangu iishi kwa ajili yako.” Mwanzo 12: 10-13
Matukio ya Ibrahimu; -
-
Alipungukiwa chakula na kwenda kutafuta,
-
Ibrahimu alitambua kuwa mkewe Sara ni
mzuri,
-
Ibrahimu aliingiwa hofu ya kuuawa,
-
Ibrahimu akaingia kwenye kudanganya
(kusema uongo)
-
Uongo aliosema Ibrahimu ukasajiliwa
kwenye damu ya Ibrahimu.
ii)
Isaka mtoto wa Ibrahimu
Kama ilivyokuwa kwa baba yake,
Isaka naye alipitia matukio yale yaliyosajiliwa kwenye damu ya Ibrahimu.
“Isaka akakaa katika
Gerari. 7Watu wa mahali hapo wakamwuliza habari za mkewe. Akasema, Ni
ndugu yangu huyu maana aliogopa kusema, Ni mke wangu, watu wa nchi wasije
wakamwua kwa ajili ya Rebeka; kwa maana alikuwa mzuri wa uso.” Mwanzo 26: 6-7
Matukio ya Isaka; -
-
Alimuoa Rebeka aliyekuwa mzuri,
-
Hakuwa na chakula akaenda kutafuta
Gerari,
-
Aliingiwa na hofu ya kuuawa,
-
Alisema uongo kama baba yake kuwa Rebeka
ni ndugu yake
Mfano katika maisha yetu; -
Kuna wakati mwanandoa anakuwa na
mgogoro wa ndoa na mwenza wake kuhusu tabia fulani inayomlazimu kushitaki kwa
wakwe zake bila kufahamu kuwa tabia husika imesafiri kwa njia ya damu kutoka
kwa baba/mama mkwe wake kwenda kwa mwenza wake. Mara nyingi migogoro hiyo hukosa
ufumbuzi.
iii)
Esau na Yakobo, Watoto wa Isaka.
Kwa Kadiri tabia inavyozidi
kurithishwa ndivyo inaimarika na kuwa hatari zaidi. Kwa Yesu tabia hizo
hukomeshwa bila kujali ukubwa wake.
Isaka akiwa mzee alitaka
kumbariki mwanae mzaliwa wa kwanza, Esau. Yakobo, hali akiipata taarifa hiyo,
alijiandaa kudanganya. Yakobo akijua Ngozi ya kaka yake (Esau) kuwa
inavinyweleo, aliamua kutengeneza vazi la ngozi ili kufanana na Esau na kulivaa
kufanikisha kudanganya. Yakobo alifanikiwa kudanganya kwa sababu baba yake
(Isaka) alikuwa kipofu.
2.
Tabia kwa njia ya damu.
i)
Nyumba ya Ibrahimu – kila mzaliwa wa
kwanza hapati/hafanikiwi.
Mzaliwa wa kwanza wa Ibrahimu
aliitwa Ishmaeli aliyemzaa kwa kijakazi. Mzaliwa wa pili alikuwa Isaka. Mungu alifanya
agano na mzaliwa wa pili wa Ibrahimu.
“Ibrahimu akamwambia Mungu, Lau kwamba
Ishmaeli angeishi mbele yako. Mungu akasema, Sivyo, lakini Sara mkeo atakuzalia
mwana wa kiume, nawe utamwita jina lake Isaka. Nami nitafanya agano langu imara
kwake kuwa agano la milele kwa ajili ya uzao wake baada yake.” Mwanzo 17:
18-19
ii)
Mzaliwa wa kwanza wa Isaka aliitwa Esau
na hakupata, ila Yakobo mzaliwa wa pili alipata.
“Akasema, Je! Hakuitwa Yakobo kwa
haki, maana amejitia mahali pangu mara mbili hizi? Alichukua haki yangu ya
mzaliwa wa kwanza, na sasa amechukua mbaraka wangu. Akasema, Je! Hukuniwekea na
mimi mbaraka?” Mwanzo 27:36
iii)
Mzaliwa wa kwanza wa Yakobo aliitwa
Reubeni na hakupata.
“Yakobo akawaita wanawe, akasema, Kusanyikeni,
ili niwaambie yatakayowapata siku za mwisho. Kusanyikeni, msikie, enyi
wana wa Yakobo,Msikilizeni Israeli, baba yenu.
Reubeni, u mzaliwa wangu wa
kwanza,Nguvu zangu, na malimbuko ya uwezo wangu.Umewapita wengine kwa ukuu na
kwa nguvu.Umeruka mpaka kama maji, basi usiwe na ukuu,Kwa sababu ulikipanda
kitanda cha baba yako,Ukakitia unajisi; alikipandia kitanda changu.” Mwanzo 49:
1-4
Reubeni alikuwa na nguvu na ukuu
akiwazidi nduguze, yaani alikuwa mahiri, hata hivyo alikosa kwa sababu
alikinajisi kitanda cha baba yake kwa kulala na mwanamke; baba yake alimnyang’anya
ukuu.
Kwenye damu kuna vitu vinapokea
kila neno. Baada ya Yakobo kumnyang’anya ukuu Reubeni, Yakobo akafariki, na
hivyo Reubeni hakusomeka kuwa mtoto wa Yakobo. Ndugu zake kuanzia mzaliwa wa
pili wakalinda nafasi zao ili Reubeni asiweze kuzichukua.
Neno: 1 Nyakati 5:1
Kwakuwa Reubeni alipoteza nafasi
yake, haki yake ya mzaliwa wa kwanza walipewa watoto wa Yusufu.
Magonjwa mengi yanayowapata watu
huwa yanarithishwa kupitia damu (DNA). Kwa jina la Yesu magonjwa ya kurithishwa
kutoka kwa baba kwenda kwa mwana yanaondolewa.
Baba yetu siku zote hupenda
kusaidia watu tangu zamani amekuwa akifanya hivyo. Muujiza wa mtu upo kwenye
kufuata anachoambiwa.
3.
Nyumba ya Yoabu
Kuna namna ya rohoni ambapo
unaweza kuitengeneza mtu usiweze kurithi tabia kutoka kwenye familia au kwenye
ukoo. Ni kwa kushindana kwenye ulimwengu wa roho kwenye familia na kwenye ukoo
ili uweze kuziondoa zisikupate wewe na uzao wako.
Kuna familia inayoathirika kwasababu
ya maneno waliyotamkiwa ambayo yanaingia kwenye damu na kwa kadiri wanavyozaliana
ndivyo matatizo yanazidi kuongezeka kwenye uzao wao. Namna ya kuweza kushinda
tatizo hilo ni kwa kutumia Neno.
Neno: 2 Samweli 3:27
Kwa Kadiri familia za nyumba ya Yoabu
walivyoendelea kuoa ndivyo matukio ya ukoma, ombaomba, ulemavu yalivyosambaa.
Hata hivyo Bwana huyabatilisha
maneno yote tunayotamkiwa - Waebrania 4:12
Kuna tabia au matukio ambayo yapo
kwenye familia ambayo ni tatizo kwenye maisha ya watu wa familia yako; namna ya
kushinda tatizo au matukio hayo ni kutoroka na kwenda kwenye ukoo wa Yesu. Ukiwa
ndani ya familia ya Yesu unakuwa mrithi wa tabia za Yesu na namna ya kuingia
kwenye ukoo wa Yesu ni kupitia damu ya Yesu.
Sisi sote tumekombolewa kwa damu
ya Yesu – 1 Petro 1:18-23
Damu inaweza kusajili tabia
kutoka kwa mzazi Kwenda kwa mtoto. Tabia hiyo inaweza kuwa magonjwa, umasikini,
ulevi au wizi, au tabia nyingine yoyote. Usifanye au kusema jambo lolote kwa
ajili ya kujifurahisha wewe mwenyewe kwa sababu, jambo au neno hilo linaweza kuwa
madhara kwenye uzao wako.
Neno: Waebrania 7: 9-10
Matukio katika ukoo yanaenda
mpaka kwenye sadaka. Lawi alihesabika katoa sehemu ya kumi kwa sababu, wakati
Ibrahimu akitoa sehemu ya kumi, Lawi alikuwa kwenye kiuno cha Ibrahimu (Lawi na
baba yake hawakuwa wamezaliwa).
Kama jema au baya ulifanyalo,
hilo linakuwa limesajiliwa kwenye damu yako na watoto wako au wajukuu wako au
vitukuu vyako au mtu yeyote anayetokana na uzao wako atahesabika ametenda jambo
hilo kwa sababu, wakati ukitenda jambo hilo, wao walikuwa kwenye kiuno chako. Damu
iliyosajiliwa kwenye damu yako itasafiri mpaka kwa uzao wako. Tumtumikie Mungu
kwa ajili ya uzao wetu.
Kuna mambo mema pia huenda kwa
uzao wa mtu kupitia damu. Mtu anaweza kurithi imani kutoka kwa wazazi wake na mara
nyingi imani ya kurithi inakuwa ni kali kuliko.
Neno: 2 Timotheo 1: 3-5
Namna ambayo matukio ya familia husafiri;
-
1.
Mazindiko ya familia
Mazindiko
yanatokea ikiwa mtu ambaye ni kiongozi wa familia anaikabidhi familia kwa
shetani ili ilindwe. Ni mkataba wa shetani na wazee wa ukoo. Malipo kwa Shetani
ni damu kutoka kwa mwana wa ukoo huo. shetani hutengeneza matukio mbalimbali
kama vile magonjwa au ajali ili kupata damu.
Ikiwa,
kutokana na mkataba wa kishetani ambao wazee wa ukoo wameingia na shetani, damu
inapaswa kuchukuliwa kwa magonjwa, basi shetani hutengeneza aina fulani ya
ugonjwa, mfano, shinikizo la damu, mshtuko wa moyo, au ugonjwa wowote, na huo
ndiyo utakuwa utaratibu wa vifo vya wana wa ukoo huo.
Sambamba
na mikatabo ya kishetani ya ukoo, kunakuwa na mashetani yaitwayo mizimu yanayolinda
familia/ukoo/mikataba hiyo. Mashetani hayo yanakuwa vilevile kama kabila la
ukoo huo lilivyo; mfano, kama ni kabila la kisukuma, mashetani yatafanania
usukuma.
“Mwivi
haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha
wawe nao tele.” Yohana 10:10
2.
Dhambi
Dhambi
pia inaweza ikaleta tatizo kwenye familia yako kwa sababu ya dhambi ulizonazo. Dhambi
inaleta kifo, unaweza kufanya jambo na usilimalize kwasababu ya dhambi. Dhambi husababisha
matukio katika damu.
Kwa
sababu ya dhambi, Mungu humuua mtenda dhambi.
“Yuda
akamwoza mke Eri, mzaliwa wake wa kwanza, na jina lake huyo mke ni
Tamari. Naye Eri, mzaliwa wa kwanza wa Yuda, alikuwa mbaya machoni pa
BWANA; na BWANA akamwua.” Mwanzo 38:6-7
–
Mzaliwa wa kwanza wa Yuda alitenda dhambi, Mungu akamuua.
Warumi
6:23
– Mshahara wa dhambi ni mauti.
3.
Kushiriki mambo ya mila na desturi
Mila
na desturi huendeshwa na wakuu wa familia au ukoo, na ni sharti kuhudhuria. Huwekwa
masharti kwa hao wasiohudhuria, mfano kutengwa na familia au ukoo.
Yesu
anatuita twende kwake, tumtegemee Yeye kwakuwa ndani ya ukoo wa Yesu kuna kila
kitu na tunapata ulinzi wa damu ya Yesu dhidi ya mambo ya ukoo wa kidunia.
“Njoni kwangu, ninyi nyote
msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.”
Mathayo 11:28
Kwenye
ukoo wa Yesu tunapata ndugu wengi na hakuna hata laana ya mzaliwa wa kwanza,
kwa maana, kwa kupigwa kwake Yesu familia zetu zimekombolewa.
Isaya
53:5
Mafarisayo
waliogopa kulitaja jina la Yesu kwa sababu ya mambo ambayo yangewatokea.
“akisema, Je!
Hatukuwaamuru ninyi kwa nguvu, msifundishe kwa jina hili? Nanyi, tazameni,
mmeijaza Yerusalemu mafundisho yenu, na mnataka kuileta damu ya mtu yule juu
yetu.” Matendo ya Mitume 5:28
Ukilitaja
jina la Yesu maana yake unaileta damu ya Yesu Kristo juu yako.
Yesu
anatuita watu wote kutoka kwenye familia na koo zetu tulizonazo tuziache na
tuingie kwenye ukoo wa Yesu. Kitendo cha kuhama kutoka kwenye koo zetu za
kidunia tulizonazo na kuingia kwenye ukoo wa Yesu kinaitwa Kumpokea Yesu.
Ukoo
wa Yesu hauchagui aina ya watu; hubeba watu wote, tajiri au masikini wa dini zote.
Inakupasa leo kukubali kuwa ndani ya ukoo wa Yesu, nawe utakuwa umetoroka katika
matukio kwenye familia. Unaposema damu ya Yesu Kristo unairuhusu damu iingie
kwenye familia yako.`


0 Comments