UFUFUO NA UZIMA
CATHEDRAL
IBADA YA PASAKA 12.04.2026
ASKOFU DKT
JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO: MATUKIO YA
KICHAWI
![]() |
Ulimwengu una matukio mbalimbali; mfano, yapo matukio ya kijeshi ambapo nchi na nchi zinapigana. Kuna matukio ya kichawi. Yapo matukio ambayo unaweza kuyaona ni ya kawaida kumbe ni mambo ya kichawi.
Uchawi upo; Biblia takatifu na Quran vimethibitisha.
Mfano, Biblia imeandika kuwa, usimwache mwanamke mchawi kuishi. Kuna matukio
yanampata mtu ambaye anayatafsiri kuwa ni matukio ya kibinadamu lakini ni
uchawi.
Mungu aliumba Malaika; baadhi ya Malaika waliasi na
kutupwa duniani. Kwasababu hiyo, kuna Malaika wa aina mbili, yaani, Malaika
watakatifu na Malaika waovu. Malaika watakatifu hutumwa na Mungu kutuhudumia watoto
wake. Malaika waovu nao hutumwa na shetani kusababisha matatizo kwa watu.
Malaika waovu wana majina mengi ambayo hutofautiana
sababu ya majukumu yao; wapo huitwa, mapepo, mashetani, majini, mizimu,
vibwengo n.k., wote ni walewale. Mashetani ni watafiti. Mashetani wanaoufahamu
wao uleule waliokuwa nao kabla ya kuasi na kutupwa. Mashetani wakitolewa ndani ya
mtu huenda wakitafuta. Wana sifa zote za Malaika, lakini wao; -
- Ni Malaika wa kuzimu: Ufufuo,
9:11
- Ni Malaika wasioilinda enzi yao
wenyewe, Yuda 1:6
- Ni joka na Malaika zake, Ufunuo
12:7
- Ni Ibilisi na Malaika zake,
Mathayo 25:41
“Kwa maana ikiwa Mungu hakuwaachilia malaika
waliokosa, bali aliwatupa shimoni, akawatia katika vifungo vya giza, walindwe
hata ije hukumu;” 2 Petro 2:4
Kwa ufahamu huu juu ya Malaika waovu, ni dhahiri kama
isemavyo filosofia, huwezi kutatua tatizo bila kujua chanzo chake, na kama mtu
akijaribu kutatua tatizo bila kujua chanzo cha tatizo atatengeneza tatizo
tofauti na alilonalo. Mungu hutuma Malaika zake katika kila kazi yake, vivyo hivyo,
shetani naye hutuma malaika zake ili kutenda uovu, mfano, Malaika Gabrieli alitumwa
na Mungu kwa Daniel kuleta taarifa kuhusu kusikiwa maombi yake alivyosali na
kufunga siku ishirini na moja, na kwa Mariamu kuhusu kuchukua mimba kwa uwezo
wa Roho Mtakatifu. Malaika waovu hutumiwa na wachawi kuleta matatizo kwa watu.
Kanisa la Ufufuo na Uzima tunaamini kuwa kumtumikia
Mungu ni kuwatumikia watu, hivyo kuwatumikia watu ni kupambana na Malaika waovu
wawatoke watu, na siku ya leo tutaondoa Malaika waovu wote, kwa Jina la Yesu. Tatizo
kubwa la mtu ni kuwa na tatizo lakini hajui chanzo zha tatizo lake.
Malaika waovu ni roho. Hawafanyi kazi mpaka watumwe
na wachawi.
Sifa Za Malaika:
Wanaweza kujigeuza kuwa chochote; Malaika waovu wanaweza
kugeuka kuwa mtu, mti, upepo, mnyama, wadudu, n.k. pia Malaika waovu wanaweza
kuwa hali tofauti tofauti kama ugonjwa, ulemavu, matatizo, kifafa, ububu, ukichaa.
“Mtu mmoja katika mkutano
akamjibu, Mwalimu, nimemleta mwanangu kwako, ana pepo bubu; na kila
ampagaapo, humbwaga chini, naye hutoka povu na kusaga meno na kukonda; nikasema
na wanafunzi wako wamtoe pepo, wasiweze. Akawajibu, akasema, Enyi kizazi
kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi hata lini? Mleteni
kwangu.” Marko 9:17-26
Mtu anaweza kuwa na hali isiyo ya kawaida kumbe Malaika
waovu wametumwa na wachawi wamuingie na kuleta hali hiyo. Mtu anaweza kuwa
bubu, anaweza kuwa na hali ya kubwagwa chini, kukonda, kutoka povu, kuharibu
biashara, kifafa, nuksi, balaa, kukosa kibali, n.k.
Mtu akishaingiwa na pepo aliyetumwa na wachawi,
huonekana na ugonjwa fulani ambao hupewa jina la kisayansi, na kama mtu huyo
asipojua chanzo cha ugonjwa huo, huishia kukubaliana na sababu za kisayansi na
mwisho kurasimisha ugonjwa huo kwake.
Ukijua asili ya wachawi huogopi tena, na ukijua
nguvu iliyo ndani ya damu ya Yesu huogopi mchawi kabisa. Yesu anasema mwenye
hali/matatizo yoyote ALETWE KWAKE
“Akawajibu, akasema, Enyi kizazi
kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi hata lini? Mleteni
kwangu.” Marko 9:19
Fungua moyo wako kwa Yesu naye atakutibu; Matendo
ya Mitume 16:14, Mathayo 11:28. Roho Mtakatifu hushuka na
kuyeyusha kamba zote za kichawi.
Mapepo, majini, vibwengo, mashetani n.k. wakimuingia
mtu huweza kumfanya mtu ajipeleke mwenyewe kwenye hatari; mfano, unamuona mtu
amening’inia kwenye chombo cha moto kwa namna ya kuhatarisha maisha yake lakini
anaona ni kawaida kwake. Huitwa ajali ya kujitakia
“Enyi Wagalatia msio na akili, ni nani
aliyewaloga, ninyi ambao Yesu Kristo aliwekwa wazi mbele ya macho yenu ya kuwa
amesulibiwa?” Wagalatia 3:1
Yesu hukemea kwa amri. Sisi pia tunayoamri ya kukemea
pepo atoke na kumrudia yeye aliyemtuma; ni msaada utokao juu. Mara nyingi mtu akipata
msaada shetani huzidisha tatizo la mtu ili akate tamaa; mfano, ustawi wa biashara
ya mtu kuporomoka zaidi.
Mfano, Yesu alipomkemea pepo wa kifafa amtoke mtu,
pepo akamtia kifafa sana mtu huyo na kumfanya aonekane amekufa, hata watu wengi
wakasema amekufa (Marko 9:26). Machoni pa watu hali ya mtu
huonekana kama amekosa msaada lakini yampasa mtu kutoacha kumfuata Yesu kwani bidii
husababisha shetani kumuachia mtu.
Mashetani wanaweza wakamfanya mtu aonekane amekufa. Bahati
mbaya zaidi hospitalini hawana kipimo cha kupima kifo; wao hupima viashiria tu
kuwa mtu yawezekana amekufa, mfano, mapigo ya moyo, kucheza kwa macho n.k. Mashetani
wanaweza kufanya vipimo kuonesha mapigo ya moyo yamesimama na macho hayachezi
na hivyo mtu huyo kuthibitishwa kitabibu kuwa amekufa, kumbe ni kulogwa.
Wachawi ni watu ambao ni mawakala wa shetani. Wachawi
hutumia roho ambazo ni Malaika wa giza ili kumloga mtu. Mchawi anaweza kuwa
baba, mama, kaka, dada, shangazi, mjomba. Wachawi sio mapepo ni binadamu, wanaweza
kuwa viongozi, mfano askofu, mchungaji, shehe, diwani, mbunge, au kiongozi wa
ngazi yoyote; na wachawi wote ni kuwafyeka na akitokea tena fyeka zaidi “Usimwache
mwanamke mchawi kuishi.” Kutoka 22:18
Sisi kwa mamlaka ya Jina la Yesu tunatumia upanga wa
roho ambao kazi yake ni kufyeka (Waefeso 6:17); tunafyeka mchawi
yeyoye. Mchawi akiwa; -
- Baba mdogo, fyekaaaaa!
- Shangazi, fyekaaaaa!
- Baba, fyekaaaaa!
- Kaka, fyekaaaaa!
- Dada, fyekaaaaa!
- Askofu, fyekaaaaa!
- Shehe, fyekaaaaa!
- Mtu yeyote, fyekaaaaa!
Kila kinachoonekana kimekufa Yesu anayo mamlaka na
uwezo wa kukishika mkono na kukiinua nacho kikasimama; mfano, kazi, maisha,
biashara, afya, huduma, n.k. Marko 9:27
Neno: Marko 1:21-23
Mashetani yanaelewa, yana utambuzi, yanaongea,
yanaangamiza, na yanapotumwa na wachawi kwa mtu, yanamtambua vizuri mtu huyo ni
nani. Mashetani ni wanajeshi kamili wa ufalme wa giza (Waefeso 6:12).
Ili kuyazuia mashetani ni lazima yashindane na Majeshi ya Bwana.
Majeshi ya giza yakiwa mahali yanamiliki; akiingia
Yesu utawala wao unakoma. Kwenye maisha yetu tunayo amri ya kumkemea pepo
afumbe kinywa na atoke kwenye biashara, afya, kazi, huduma, n.k., kwa Jina la
Yesu na anatii. Sisi hatuhitaji nywele, mafuta, kucha au kitu chochote ili
kutoa pepo; sisi ni FUMBA KINYWA, TOKA kwa Jina la Yesu.
Tatizo la mtu lipo hapa; kutambua chanzo cha tatizo
na utatuzi wake. Mchawi, msoma Nyota, mpiga ramli, mganga wa kienyeji ni
walewale kama ilivyo wizara mbalimbali ndani ya serikali moja. Huwezi kutatua
tatizo la kulogwa kwa kwenda kupata msaada kwa mganga wa kienyeji.
Utatuzi kwa tatizo la kulogwa na wachawi ni kumfuata
Mtu wa Mungu, Mtu aliyetumwa na Mungu kufanya kazi ya Kimungu. Mungu hutuma
watu kwenye maisha yetu. Chochote tunachokitaka kutoka kwa Mungu kipo kwa watu;
Mungu alishashusha yote kwa watu. Ukimkosa Mtu aliyetumwa na Mungu, umemkosa
Mungu.
Kidunia, kila familia huwa imezindikwa. Tunahakikisha
leo wachawi wote wanapoteza wateja. Mizimu ni mashetani waliokaa kwenye ukoo
kwa miaka mingi. Kila ukoo/kabila kuna mizimu inayomiliki ukoo/kabila hilo;
mfano, kwa kabila la Wasukuma, kila ukoo una bibi wa ukoo ambaye kila salamu
inamtaja.
Wanaukoo hutengenezwa na mizimu kuwa na tabia fulani.
Wanaukoo huzuiwa mambo fulani; mfano, kuoa/kuolewa, kula aina fulani ya
chakula, umasikini/umiliki unaopimwa. Ikitokea mwanaukoo kafanikiwa jambo fulani
kinyume na tabia ya ukoo, mizimu huyaondoa mafanikio hayo.
Mizimu ya ukoo pia husafirisha tabia fulani au hali
kutoka kizazi hadi kizazi. Mizimu ikivunjika tabia hizo zinaondoka katika ukoo
huo. Ukitoka kwenye vifungo vya mizimu ya ukoo unakuwa huru na matatizo na
taabu zote. Mashetani wako wa viwango tofauti, mfano, kuna wakuu wa giza,
wafalme wa giza, na mamlaka za giza.
Mungu huwashika mkono watu. Unatakiwa kukubali
kushikwa mkono na Mungu. Kuna watu wana Bahati ya kushikwa mkono na Mungu
lakini hawashikiki; mfano, mke wa Ruthu alishikwa mkono na Mungu kumuepusha na
moto mkali wa Sodoma na Gomora lakini hakuvumilia akageuka nyuma na kuwa jiwe
la chumvi. Hatupaswi kumuogopa shetani auaye mwili. Yatupasa kumuogopa Mungu
auaye mwili na roho.
Sala zote tunazosali sio mbaya; mfano sala ya Bwana,
sala ya Bikira Maria, ama dua ya Quran. Ubaya wa sala hizi hazishughuliki na
shetani. Sisi Ufufuo na Uzima katika sala tunashughulika na shetani;
tunamuamrisha shetani atoke kwenye maisha yetu na hali zetu za maisha, kwa Jina
la Yesu.
Kuna viumbe ndani ya mtu wanamwendesha mtu kufanya
yale asiyopenda kufanya. Kuna familia hawaelewani kabisa wao kwa wao. Mambo haya
yote yanatokana na tabia ambazo zinaongozwa na mizimu.
Pepo hutumwa na mtu. Bahati mbaya sana mtu huyo
lazima awe anakufahamu. Pepo anapotumwa huwa na kazi ya kutimiza alichotumwa kufanya;
mfano kuiba Nyota ya uso wa kibali au Nyota ya macho ya kuona fursa. Wachawi wakikuibia
hutumia Nyota hiyo kuendesha mambo yao. Unapokuwa umeibiwa Nyota mfano, Nyota ya
uso, kila anayekuona anakuwa havutiwi nawe.
“Amemeza mali, naye atayatapika tena; Mungu atayatoa
tumboni mwake.”Ayubu 20:1
Ukimkemea shetani na Malaika zake wanahama katika maisha
yako na hawatakuwako tena kwa sababu Jina la Yesu ni jina lipitalo majina yote.
Kuna viumbe vinakuendesha bila wewe kujua na ukiviondoa viumbe hivyo kuna
baadhi ya tabia zitaondoka kwako. Mungu amemuumba mtu na uso wenye kibali,
mashetani wakichukua hicho kibali kila mtu anayekuona hataki kukuona tena kwa
sababu umeibiwa Nyota ya uso wako.
Unazaliwa na akili ya kufikiri na uwezo mkubwa wakukumbuka
lakini zikichukuliwa na wachawi wanazitumia kwa ajili ya kazi za kichawi. Majini
na pepo wanapotumwa huja ili kuharibu lile kusudi maalum ambalo Mungu ameliweka
ndani ya mtu; pia huweza kuharibu mifumo ya mwili wa mtu na kuleta magonjwa na
mtu huyo akifa huonekana kama alikufa kutokana na ugonjwa fulani au shida fulani,
kumbe ni moja ya matukio ya kishetani ambayo wanafanya ndani ya mtu huyo.
Ili mtu awe na nguvu za kushindana na mashetani
hayo, ni lazima mtu huyo awe amempokea Yesu katika maisha yake (Waefeso
6:12). Mpokee Yesu akujaze nguvu za kuyashinda mashetani.


0 Comments