google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

NGUVU YA UFUFUO

UFUFUO NA UZIMA CATHEDRAL
IBADA YA PASAKA 05.04.2026
ASKOFU DKT GERSHOM MWAKILA
SOMO: NGUVU YA UFUFUO 


Leo ni siku ya Pasaka. Siku hii imezoeleka kusherehekewa na Wakristo wote duniani. Lakini, je, Pasaka ni siku kuu ya kikristo? Swali hili linaweza kujibiwa kwa namna mbili;
moja, kibinadamu, na mbili kiroho.

Kibinadamu, watu husherehekea Pasaka kwa namna tofauti tofauti; kupika chakula kizuri, wapo hunywa vileo na kutembelea sehemu mbalimbali kufurahisha mioyo yao. Hawa wote hujiita Wakristo.

Je, Pasaka ni siku au sherehe ya Wakristo? Biblia imetaja neno “Wakristo” mara moja tu, vilevile imetaja “Wana wa Mungu” mara sitini na moja na “Mwana wa Mungu” mara arobaini na sita.

“hata alipokwisha kumwona akamleta Antiokia. Ikawa kwa muda wa mwaka mzima wakakusanyika pamoja na kanisa na kuwafundisha watu wengi. Na wanafunzi waliitwa Wakristo kwanza hapo Antiokia.” Matendo ya Mitume 11:26

Hivyo basi, ili kuwa sahihi sana, Biblia kutaja “Wana wa Mungu” na “Mwana wa Mungu” zaidi ya mara mia moja kwa pamoja imelenga kuifanya Pasaka kuwa ni sherehe ya Wana wa Mungu kwasababu Wana wa Mungu wamekombolewa, hawafi na wanarithi uzima wa milele. Wakristo hufa.

“isha baadhi ya Masadukayo wakamwendea, wale wasemao ya kwamba hakuna ufufuo, wakamwuliza,” Luka 20:27

-      Wana wa ulimwengu huu huoa/huolewa lakini Wana wa Mungu hawaoi/hawaolewi kwasababu ni Wana wa Ufufuo.

Kilichozaliwa na mwanadamu kinaitwa mwanadamu na kinachozaliwa na Mungu kinaitwa Mungu; kama ilivyo, mwana wa mbwa huitwa mbwa na mwana wa ng’ombe huitwa ng’ombe. Kimsingi, Wana wa Mungu ni miungu katika dunia hii kwa maana wamezaliwa na Mungu katika namna ya kiroho. Wana wa Mungu ni watu ambao wamempokea Yesu, na wamefanyika kwa namna ambayo sauti zao zimejazwa nguvu ya kusikilizwa kwa chochote watakachokifanya.

“Amin, amin, nawaambia, Saa inakuja, na sasa ipo, wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale waisikiao watakuwa hai.” Yohana 5:25

Sauti ya Mwana/Wana wa Mungu inasikika hata kwa waliokufa na vilivyokufa. Chochote kilichokufa au ambacho kiko kwenye msafara kuelekea kufa kikiisikia sauti ya Mwana wa Mungu hupata uhai/hakifi. Imani yetu imejazwa katika kifo cha Yesu na kufufuka kwake; tunaamini hivyo. Tunamwamini muasisi wa Imani yetu kama alivyozaliwa kimaajabu, akakua kimaajabu, akatenda kazi yake kimaajabu, akashtakiwa kimaajabu, akafa kifo cha maajabu, akazikwa na kufufuka kimaajabu. Kufufuka kwa Yesu kupo katika nguvu ya Mungu iliyomtoa kaburini, ambayo inakaa ndani yetu. Nguvu hiyo hutuhuisha sisi kwa Roho Mtakatifu.

“Hata sabato ilipokwisha, ikipambazuka siku ya kwanza ya juma, Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi. Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi; kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akalivingirisha lile jiwe akalikalia.” Mathayo 28:1-2

Nguvu ya Ufufuo:

Kufufuka kwa Yesu kumefanyika kwa Nguvu ya Ufufuo ambayo kwayo mambo makuu ya rohoni ni dhahiri na hutokea kama ifuatavyo; -

1.   Ufufuo una nguvu ya kusababisha tetemeko.

Kila mtu husikia bila kujua kuwa kuna mtu wa rohoni ameshuka. Akili za kibinadamu na kisayansi haziwezi kuelewa wala kusikia ila Wana wa Mungu pekee yaani, Wana wa Ufufuo.

Siku ya Ufufuo ni siku ya tetemeko ulimwenguni kutetemesha kila kilicho kinyume na kazi ya Mungu. Tukikumbuka Ufufuo tunaagiza tetemeko liende kwenye kila kaburi lililozika mambo yetu; mfano, kaburi lililozika afya, kazi, hatma, Nyota, huduma n.k.

Kupitia Nguvu ya Ufufuo kila kilichozikwa kwenye kaburi kinainuka na kuwa hai tena. Kuna viumbe wa rohoni ambao ni Malaika wa Bwana, hushuka na kuleta tetemeko kwenye kaburi na kufufua kila kilichozikwa.

2.   Ufufuo una nguvu ya kuondoa lolote ambalo limewekwa na wanadamu kwa lengo la kuzuia mpango wa Mungu.

“Hata ilipokuwa jioni akafika mtu tajiri wa Arimathaya, jina lake Yusufu, naye mwenyewe alikuwa mwanafunzi wa Yesu; mtu huyu alimwendea Pilato akauomba mwili wa Yesu. Ndipo Pilato akaamuru apewe. Yusufu akautwaa mwili, akauzonga-zonga katika sanda ya kitani safi, akauweka katika kaburi lake jipya, alilokuwa amelichonga mwambani; akavingirisha jiwe kubwa mbele ya mlango wa kaburi, akaenda zake.” Mathayo 27:57-60

Yusufu, mmoja wa wanafunzi wa Yesu, aliuomba mwili wa Yesu na kuuvingirisha sanda, akauweka kaburini, kisha akaweka jiwe kubwa mlangoni mwa kaburi.

Kukawa na walinzi Mafarisayo ambao waliweka muhuri kwenye jiwe kuzuia mtu/watu kuligusa jiwe hilo ili mwili usitolewe na kudanganya kuwa Yesu amefufuka.

Mafarisayo walitenda kibinadamu bila kuzingatia kuwa ilitabiriwa kutendeka kiroho, na Mbingu zina mpango wa kutekeleza Ufufuo siku ya tatu (wakati ulionenwa utakapotimia).

Siku ya tatu ilipotimia, Mbingu hazikusubiri mkono wa mwanadamu; Mbingu zilituma Malaika kwenda kuliondoa jiwe na Yesu akafufuka.

Wakati binadamu wanaweka mpango wa kukuzuia usiende kwenye muujiza wako, Mbingu zina mpango kinyume nao wa kukufanya upenye katika ule wakati sahihi ambao Mbingu zimepanga ufanikiwe.

Mbingu hutuma mjumbe/wajumbe wake/Malaika kututoa kwenye majaribu ya muovu/mkono wa kibinadamu.

Mbingu husikiliza Kanisa liseme tu ili zitume mjumbe wake kuondoa vizuizi vyote vilivyowekwa na shetani kupitia watoto wake/binadamu.

“Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi; kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akalivingirisha lile jiwe akalikalia.” Mathayo 28:2

Katika kalenda ya Bwana, ni saa ya Ufufuo duniani, na ifahamike kwamba, kama Baba yetu mpendwa alivyotuambia, Pasaka hii ni ya mwisho tunakula tukiwa na hali tuliyonayo; katika Pasaka hii tunajazwa utele wa Bwana.

Mungu anafanya mambo yote kuwa mapya katika Pasaka hii. Katika hili, Mungu ameachilia Malaika wake kuondoa vizuizi katika maisha yetu; Yeye hutuwazia yaliyo mema siku zote.

Kila kizuizi angukaaaa, kwa Jina la Yesu!

Kwetu sisi, Ufufuo ni Malaika wa Bwana kuondoa vizuizi katika maisha yetu. Malaika wanatetea walio Wana wa Mungu kwa kuwaondolea vikwazo vyao.

3.   Ufufuo una nguvu ya kuwafanya walinzi wa maisha wafe.

Wana wa Mungu wanalindwa na Nguvu za Mungu. Hakuna nguvu nyingine ya kutegemea ila ni kupitia nguvu za Mungu na kuwa na ulinzi wa Mungu. Mungu huyatembelea maisha yetu. Nguvu ya Ufufuo; -

-      Inawafanya watu wanaotaka kukuangamiza wafe.

-      Inawalaza chini walinzi wote wanaokulinda ubaki kwenye shida.

-      Hukulinda dhidi ya nguvu za giza.

Wana wa Mungu hawalindwi na viumbe au vitu vyovyote kama chumvi, mafuta, sabuni, chupa, maji n.k., Wana wa Mungu wanalindwa na Neno la Mungu. Chumvi, mafuta, sabuni, chupa, maji n.k., haviwezi kukukimbilia ili kukuokoa kwenye hatari ila Neno la Mungu, ambalo kwa hilo; -

-      Mungu halali wala hasinzii.

-      Ni taa na lina macho.

-      Atulindae ana miguu hivyo anatembea; Bwana hutembea kuja kututendea sawasawa na haja zetu; kwa wachawi ni nyundo iangukayo kwenye vifua vyao, ni mkate au chakula cha uzima, Neno linafyeka maana ndilo Upanga wa Roho, lakini vilevile Neno li shahidi wa kazi njema za Mungu. Kwenye Biblia wachawi waliishia kupigwa.

Ufufuo una nguvu ya kufanya wote watulindao kwenye matatizo wafe, kwa maana kutaka kwetu ndiko kutaka kwa Bwana. Siku ambayo mtu anaenda kupokea miujiza ni siku ambayo kunakuwa na vizuizi vingi ambavyo vinamzuia mtu asiende nyumbani mwa Bwana; ni kwa sababu kuna watu wanakuzuia usiende.

“Na kwa kumwogopa, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu.” Mathayo 28:4

Wakati Yesu anakufa, maandiko yanasema watu wengi walifufuka; -

“Nimesulibiwa pamoja na Kristo; lakini ni hai; wala si mimi tena, bali Kristo yu hai ndani yangu; na uhai nilio nao sasa katika mwili, ninao katika imani ya Mwana wa Mungu, ambaye alinipenda, akajitoa nafsi yake kwa ajili yangu.” Wagalatia 2:20.

Wakati wa kufufuka kwa Yesu walinzi, waganga, wachawi, wasoma nyota, wapiga ramli ni zamu yao kufa, kwa Jina la Yesu.

4.   Ufufuo una nguvu ya kukamilisha maneno yote yaliyosemwa juu ya mtu.

Bwana Yesu hakukubali kwenda kinyume na kila alichoandikiwa bali alifuata kile kilichoandikwa na Mungu na vyote alivyoandikiwa na Mungu alivitimiza.

-      Alizaliwa kama ilivyotabiriwa.

-      Alienda Misri kama ilivyotabiriwa.

-      Alienda Bethlehemu, Galilaya, Yerusalemu n.k. kama ilivyotabiriwa.

-      Alisema atasalitiwa na akasalitiwa kama ilivyotabiriwa.

Wakati Yesu akila chakula mara ya mwisho pamoja na wanafunzi wake, alitabiri kusalitiwa kwake ambapo wanafunzi wake walifadhaika sana mioyoni mwao kusikia utabiri wa Yesu kusalitiwa. Hata hivyo, Bwana Yesu aliwatia moyo wale kumi na moja mara tu Yuda msaliti alipokuwa hayupo.

Neno hili linatufundisha kuwa, Yuda wa maisha ya mtu akiondoka, Yesu huzungumza na mtu kwa habari ya maisha yake. Yuda yeyote aliyekuja/aliyepo kwenye maisha ya mtu leo tunamfyekaaa, kwa Jina la Yesu!

Kuna wakati watu wanajifanya wanakupenda sana ila mpango wao ni ishara ya kutaka kukuangamiza; hao tunawaitwa kuwa ni Yuda wa maisha yako. Kama vile Petro alivyochomoa panga lake na kumfyeka Yuda, kwa Jina la Yesu tunatwaa Upanga wa Roho ambao ni Neno la Mungu na tunakufyeka Yuda yeyote uliye kwenye maisha yetu.

-      Mchawi kwenye kazi, fyekaaaa!

-      Mchawi kwenye familia, fyekaaaa!

-      Mchawi kwenye ndoa, fyekaaaa!

-      Mchawi unayezuia safari, fyekaaaa!

-      Mchawi unayeiba Nyota, fyekaaaa!

5.   Nguvu ya Ufufuo inathibitisha kuwa yote ni kweli.

Kupitia nguvu ya Ufufuo, ahadi za Mungu zitatimia kwenye maisha yetu. Yesu alipopaa kwenda kwa Baba yake alituahidi anakwenda kutuandalia makao ya milele, na atarudi tena. Yesu alisema anatuachia Roho Mtakatifu kuwa msaidizi wetu, na ndivyo ilivyo.

Kama ambavyo yote yaliyotabiriwa yalifanyika, kwa Nguvu ya Ufufuo tunaamini vilevile ahadi ya Yesu kwetu itatimia. Kwakuwa tunaamini atarudi, kabla hajarudi lazima tuhakikishe tunakomesha wachawi na kuzuia nguvu za ibilisi kwenye maisha yetu, kwa Jina la Yesu.

Hatari kubwa ni kwa mtu anayeambiwa Yesu atarudi tena ila mtu huyo bado hajampokea Yesu.

Yote yaliyotabiriwa yalitokea, iweje mtu huyo asiamini kuwa Yesu atarudi? Ni heri leo mtu huyo ampokee Yesu, na kwa kuzingatia kuwa leo ni Pasaka, basi itakuwa kumbukumbu nzuri sana kwa mtu huyo kumpokea Yesu siku ya Pasaka.

Biblia inasema, mtu asiyempokea Yesu maishani mwake, hawezi kuurithi ufalme wa Mungu.

Faida za kumpokea Yesu: -

-      Mungu atakusamehe makosa yako yote,

-      Mungu atafuta jina lako kwenye kitabu cha kifo,

-      Mungu ataandika jina lako kwenye kitabu cha uzima wa milele,

-      Wewe unakuwa mtoto wa Mungu,

-      Wewe unakuwa rai awa Mbinguni, na

-      Mungu anakuwa Baba yako na atawajibika kwenye mahitaji yako yote.

Mkiri Yesu mbele za watu naye atakukiri mbele za Baba yake aliye Mbinguni;

“Basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni.” Mathayo 10:32

“Nami nawaambia, kila atakayenikiri mbele ya watu, Mwana wa Adamu naye atamkiri yeye mbele ya malaika wa Mungu;” Luka 12:8.

BONYEZA HAPA KUANGALIA IBADA YA JUMAPILI

Post a Comment

0 Comments