google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

KUFUTA KIAPO CHA KICHAWI

UFUFUO NA UZIMA CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 17.05.2026
ASKOFU DKT GERSHOM MWAKILA
SOMO: KUFUTA KIAPO CHA KICHAWI

Leo ni siku ya ishirini na moja ya Mfungo wa Upenyo. Ni siku muhimu sana. Biblia inatufundisha kuwa Danieli alifunga kwa siku ishirini na moja; ile siku ya ishirini na moja, Malaika Gabrieli aliyetumwa na Mungu alete taarifa kwa Danieli, alimjulisha Danieli kuwa maombi yake yalisikiwa tangu siku ya kwanza alipofunga, lakini mkuu wa Uajemi alimpinga ila Malaika Mikaeli alikuja kumsaidia kushindana naye.

Tunashawishika kuamini kuwa, miongoni mwa mambo yaliyofanyika kuzuia Danieli asipate taarifa kutoka kwa Mungu kuwa maombi yake yalisikiwa tangu siku ya kwanza, ni ‘Kiapo cha Kichawi.”

Kiapo ni maneno ambayo mtu husema, au jambo ambalo mtu analifanya ili kumaanisha kuwa kwenye hilo analosema ni kweli na anamaanisha. Kiapo kina nguvu sana kwa sababu asili yake ni ya rohoni. Makusudi ya kiapo yamebebwa kwenye ulimwengu wa roho; kiapo kinashikiriwa kwenye ulimwengu wa kiroho kwa uzuri au kwa ubaya. Mtu anapoapa, anaapa kwa mamlaka ya juu ya rohoni “Maana wanadamu huapa kwa yeye aliye mkuu kuliko wao; na kwao ukomo wa mashindano yote ya maneno ni kiapo, kwa kuyathibitisha.” Waebrania 6:16.

Mojawapo ya mambo yanayofanya watu wasije kwenye maisha ya mtu ni uwepo wa viapo vya kichawi. Kiapo ni hati miliki ya rohoni. Ukomo wa mambo yote ni kiapo. Mtu akishaapa hayo mambo hayawezi kubadilika na nilazima yatekelezwe vilevile kama yalivyoapwa. Ahadi za Mungu juu ya watu hutimia; ili Mungu ahakikishe yale aliyotuahidi kuwa atafanya vilevile alivyosema, amefunga ahadi zote kwa kamba ziitwazo kiapo. Kiapo cha Mungu akifunga huwa hakibadiliki.

Wale wanaobadilika badilika kwenda kinyume na kiapo ambacho wameweka au Mungu ameweka, Mungu hutekeleza yaleyale yaliyofanyika kwa kiapo

“Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeuka-geuka.” Yakobo 1:17.

Mfano ni kiapo cha Mungu na Musa kuwa Mungu atawatoa wana wa Israeli utumwani; wana wa Israeli walipomuasi Mungu kwa kujifanyia muungu awatoe utumwani, Mungu alitaka kuwaangamiza kwa uasi huo.

Musa alimkumbusha Mungu juu ya kiapo chake na wana wa Israeli kuwa atawatoa utumwani na kuwapeleka nchi ya ahadi, na siyo kuwaangamiza.

Mungu alikumbuka ahadi na kiapo chake, hakuwaangamiza wana wa Israeli; Mungu akatekeleza ahadi yake bila kujali kuwa wana wa Israeli walibadilika na kuasi

“Katika neno hilo Mungu, akitaka kuwaonyesha zaidi sana warithio ile ahadi, jinsi mashauri yake yasivyoweza kubadilika, alitia kiapo katikati;” Waebrania 6:17

Yale mambo ambayo Mungu ameahidi au ameweka ahadi juu ya mtu, hakuna litakalodondoka bure au kubadilika; zitabadilika nyakati, watabadilika watawala, yatabadilika masaa, lakini Mungu hatabadilika. Yale ambayo Mungu amesema, lazima yatatokea, na ameyafunga kwa kiapo. Mifumo ya ulimwengu itabadilika lakini ahadi za Bwana hazitabadiliki hata milele.

Mtu huapa kwa uovu au kwa wema; kwenye ulimwengu wa roho kiapo hicho husajiliwa. Kwa kujua ama kwa kutokujua watu huteswa na viapo walivyoviweka (Mambo ya walawi 5:4).

Kitabu cha Yeremia 4:2 kinatufundisha namna ya kuapa. Imeandikwa, “nawe utaapa hivi, Kama BWANA aishivyo, katika kweli, na katika hukumu, na katika haki ndipo mataifa watajibariki katika yeye, nao watajitukuza katika yeye.” Mtu unapoapa unajifunga kwa kifungo kuwa ulichosema hakitabadilika mpaka kitimie.

AINA YA VIAPO

Kuna aina tofauti za viapo; -

1.   Kiapo cha Kitaaluma: Wanataaluma fulani baada ya kutunukiwa hatua muhimu ya taaluma yao, huapa ili wakafanyie kazi taaluma waliyoipata. Mfano ni Wanasheria (kiapo cha kutenda haki), Madaktari (kiapo cha usiri bila upendeleo), Maaskari (kiapo cha utii kwa mamlaka ya nchi), n.k.

2.   Kiapo cha Viongozi: Viongozi wapatapo madaraka, huapa kutumia nafasi zao kwa malengo sahihi ya nafasi hizo.

3.   Kiapo cha Ndoa: Wanandoa wafungapo ndoa huapa kupendana kwenye hali yoyote, na kutoachana ila kwa kifo tu.

4.   Viapo vya Wachawi: Wachawi wafanyapo uchawi wao huapa kutimiza adhma zao.

5.   Kiapo cha Mungu: Kiapo cha Mungu kinalinda Uungu wake (Mwanzo 22:16-18). “ akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee” Aina zote za viapo huapa kwa jina la mamlaka zao za juu za rohoni zinazowaongoza, isipokuwa kiapo cha Mungu tu. Mungu huapa kwa nafsi Yake; Haapi kwa mamlaka nyingine yoyote kwakuwa hakuna mamlaka iliyo juu zaidi Yake.

Kiapo cha Mungu kina nguvu ya kufanya yale yasiyowezekana yakawezekana. Mfano; Baiolojia na sayansi kwa ujumla inasema, kwa desturi ya wanawake, mwanamke mwenye umri sawa na umri wa Sara mkewe Ibrahimu hawezi kupata mimba na kuzaa mtoto kwa maana tayari alishapita ukomo wa kuzaa.

Kiapa cha Mungu ni zaidi ya sayansi kwa maana Mungu kwa kiapo na ahadi yake kwa Ibrahimu na Sara ni kuwapatia mtoto; kwa kiapo cha Mungu, Sara akiwa na umri wa miaka tisini alimzaa Isaka.

Mungu ni Mungu wa ahadi na baraka zake juu ya mtu anazifunga na kiapo. Mungu hana mbadala wa ahadi zake. Ahadi ya Mungu imehakikishwa (2 Samweli 22:31, Zaburi 18:30).

Ahadi za Bwana hazikawii wala hazichelewi; huja kwa wakati ambao Bwana ameukusudia. Mungu alimtaka Ibrahimu amtolee sadaka, na akaahidi kumbariki Ibrahimu akimtii. Ibrahimu, akiyaheshimu maneno ya Mungu, akamtoa mwanaye Isaka kuwa sadaka kwa Mungu. Mungu akaapa kuwa, kwakuwa Ibrahimu amemtii

“akasema, Nimeapa kwa nafsi yangu asema BWANA, kwa kuwa umetenda neno hili, wala hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee, 17katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; 18na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu. ” Mwanzo 22:16-18

1.   Atambariki,

2.   Atauzidisha uzao wake kama nyota za mbinguni na kama mchanga ulioko pwani,

3.   Uzao wa Ibrahimu utamiliki milango ya adui zao, na

4.   Uzao wa Ibrahimu utajibarikia wenyewe.

Ahadi ya Mungu kwa wana wa Israeli: Baraka za Mungu kwa Ibrahimu zinaonekana kwa wana wa Israeli wakiwa utumwani. Kwa kiapo, Mungu aliwapa wana wa Israeli nchi ya maziwa na asali (Yeremia 11:5). Hata sasa, sisi pia tunamiliki nchi na vyote viijazavyo kwa kiapo. Mungu humtendea mtu sawasawa na kiapo. Kiapo ni kufungo (Ezekieli 16:59).

Kiapo cha Mungu kimefungana na neno la Mungu; Mungu ameapa na akatamka neno lake ili watu wote walitii, ya kwamba, kila goti litapigwa mbele zake na kila ulimi utaapa (Isaya 45:23). Kiapo cha Mungu kimeweka “inclusive criteria” kwa kila mtu na kwa yeyote kwenye kila nafasi; wakuu wa nchi, wakuu wa dola, wakuu wa taasisi, viongozi, au mtu yeyote, mwema na muovu, kupiga goti mbele za Bwana.

Kiapo ni tendo la rohoni. Mashetani nayo hujua nguvu ya kiapo. Marko 5:6-7; mtu mmoja mwenye pepo alipomuona Yesu, pepo akamuongoza kumkimbilia Yesu na kumsujudia, na mara moja pepo akamuapisha Yesu kwa Mungu ili asimtese.

Maneno ya pepo yule, “… Nakuapisha kwa Mungu usinitese.” Yanamaana kuwa; -

1.   Pepo anaapa ili kukwepa mateso,

2.   Ukiapishwa ukaapishika hutaweza kumwajibisha au kumtesa pepo/adui.

Ni muhimu sana kuvunja kiapo kilichowekwa na adui yako kwa sababu, ikiwa adui yako amekuwahi kwenye kiapo, mashambulizi yako kwake hayampati.

Kiapo kinaambatana na majaribu, na ukikiuka kiapo hicho adhabu ni kifo. Mfalme Sauli alijifunga kwenye kiapo yeye na watu wake/majeshi kwenda vitani bila kula (kwa kufunga) ili kulipa kisasi. Majeshi yakaogopa kukiuka kiapo hicho. Kule vitani walipokuwa mwituni kukawa na asali ikidondoka na kuleta tamaa ya kula lakini hakuna aliyejaribu kula kwa sababu ya kiapo

“Nao watu wa Israeli walisumbuka sana siku ile; lakini Sauli alikuwa amewaapisha watu, akisema, Na alaaniwe mtu awaye yote alaye chakula cho chote hata jioni, nipate kujilipiza kisasi juu ya adui zangu. Basi hakuna mtu miongoni mwa watu aliyeonja chakula.” 1 Samweli 14:24-28

Mwana wa Sauli aitwaye Yonathani ambaye hakuwepo wakati Sauli akiwaapisha watu wake, akala asali ile, akatiwa nuru machoni na kuwapiga Wafilisti sana. Hata hivyo kwa kukiuka kiapo, Yonathani alistahili kufa. Kama unauhusiano na kiapo kilichowekwa, ukikiuka unauwawa “Ndipo Sauli akamwambia Yonathani, Niambie ulilolifanya. Basi Yonathani akamwambia, akasema, Ni kweli, mimi nalionja asali kidogo kwa ncha ya fimbo ile iliyokuwa mkononi mwangu; na tazama, imenipasa kufa.” 1 Samweli 14:43-44.

Kuna viapo vya namna mbalimbali; -

1.   Kiapo cha Maneno:

Mtu huongea maneno bila kujua wala kujali nguvu iliyopo nyuma ya maneno hayo. Maneno kama, “naapa kabisa” au “I swear” yanatengeneza kiapo. Maneno yana nguvu kwenye maisha ya mtu. Kuna maneno yanatamkwa na mtu, na ndiyo inakuwa chanzo cha matatizo anayoyapitia yeye au mtu aliyetamkiwa maneno hayo. Maneno hayo pengine ni ya uongo au ya laana ila kwa sababu ni kiapo, yanatekelezwa na mamlaka ya ulimwengu wa roho sawasawa na yalivyotamkwa.

Wana wa Israeli, kwa agano la amani na Wagibeoni, wakaapa kutowaua Wagibeoni. Yoshua alipojua kuwa Wagibeoni hawakueleza ukweli, na kwamba agano lililofanyika limetokana na uongo, aliwaongoza wana wa Israeli kutowapiga Wagibeoni kwa sababu wakuu wa mkutano walikuwa wamekwisha kuwaapia kwa Bwana. Wagibeoni wakaachwa kuishi nchi ya ahadi kama watumwa kwa ajili ya nyumba ya Mungu “Naye Yoshua akafanya amani pamoja nao, na kufanya agano nao, ili kwamba waachwe hai; na wakuu wa mkutano wakawaapia.” Yoshua 9:15-23.

Ndoa ya Isaka ilihusisha kiapo cha maneno cha Ibrahimu baba yake ili Isaka asipate mke miongoni wa wanawake wa Kanaani (Mwanzo 24:1-4).

Nyuma ya maneno kuna roho: Yohana 6:63, Ezekieli 3:24, Yeremia 1:12, Yohana 1:14. Kiapo cha maneno kinauwezo wa kubeba laana kwa sababu ya roho iliyopo nyuma yake. Unaweza ukaanza jambo vizuri lakini mwisho halifanikiwi.

Maneno huapizwa sehemu yoyote; njia panda, kwenye miti, majini n.k., hivyo kiapo ni lazima kivunjwe na kubomolewa kwa jina la Yesu.

2.   Kiapo cha Kufunga:

Hiki ni kiapo cha kutokula. Wana wa Mungu wanapofunga kwa mambo fulani kwenye maisha yao, wana wa ibilisi nao hufunga kwa mambo yao. Adui na wachawi wanaweza wakaapa kwamba hawatokula hadi watakapokamilisha kuharibu maisha ya mtu. Hiki ni kiapo kikali sana. Waingiapo kwenye kiapo hiki, hufanya kwa haraka sana na kwa bidii sana; kwa kadili wanavyokuwa na njaa ndivyo wanakuwa na hasira sana. Hata hivyo, Mungu alichokiahidi juu ya maisha yako ni lazima yatimie kwa sababu Mungu alishaweka kiapo juu ya maisha yako.

Wayahudi zaidi ya 40 wamepatana kufunga kwa kutokula wala kunywa chochote mpaka wamuue Paulo (Matendo ya mitume 23:12-14).

Yeye atulindaye halali wala hasinzii wala haruhusu miguu yetu isogenzwe kwa jina la Yesu (Zaburi 121); Hapana uchawi kwa Yakobo (Hesabu 23:23).

3.   Kiapo cha Damu:

Watu wanaapa wakiwa wanamwaga damu. Kuna kiapo cha urafiki ambacho watu wanachanja damu zao wanazichanganya au wanakunywa damu ndivyo hivyo kwa wachawi wanaweka kiapo chao kwa kumwaga damu yao au wanatoa kafara zao kwa ajili ya kupokelewa kiapo chao. Kupitia kiapo cha damu, damu inakuwa inaongea kwa ajili ya kiapo walichokiweka kwenye maisha ya mtu huyo, “Musa akaitwaa ile damu, akawanyunyizia watu, akasema, Hii ndiyo damu ya agano alilolifanya BWANA pamoja nanyi katika maneno haya yote.” Kutoka 24:8.

Mambo ambayo Mungu ameyaweka juu yako ni lazima yatimie hata kama maadui wametoa kafara zao. Kiapo cha Mungu ni lazima kitimizwe.

Wachawi huapa kwa siri kwenye sehemu za viapo vyao, lakini Mungu aliyeviumba vitu vyote yupo kila mahali watakapoenda kuapia; Mungu huwaona na hivyo hakuna siri (Zaburi 91:10, Yohana 10:10).

BONYEZA HAPA KUANGALIA IBADA YA JUMAPILI

Post a Comment

0 Comments