google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

ULICHOKIBEBA NDIO CHANZO CHA VITA YAKO

UFUFUO NA UZIMA CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 06.04.2025
ASKOFU DKT JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO: ULICHOKIBEBA NDIO CHANZO CHA VITA YAKO

Mtu haanzi siku anapozaliwa, kabla hujazaliwa ulikuwepo. Mtu ni roho ambayo inakaa ndani ya nyumba ya udongo inayoitwa mwili. Mfano maji yanapokuwa ndani ya chupa huwezi ukachukua maji bila chupa, hivyo mwili ni kama chupa na maji ni roho. Mtu anapokufa, sio roho inayo kufa bali kontena ambalo ni mwili ndio unaokufa na kuzikwa. Kufa ni utengano kati ya mwili na roho, ambapo mtu mwenyewe ni roho.

“Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, Nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa.” Mhubiri 12:7

Baba na mama wanapokutana wao hutengeneza dongo yaani mwili, lakini Mungu ndiye anayeweka roho ndani ya hilo dongo. Ndani ya hiyo roho Mungu anakuwa ameweka jukumu flani ambalo anataka huyo mtu akalifanye. Mungu mbinguni anakuwa ana jambo lake ambalo anataka kulifanya hapa duniani, hivyo anamtuma mtu duniani ndani ya dongo ambalo ni mwili ili aifanye hiyo kazi kwa niaba yake. Mtu huyo anakuwa mwakilishi wa Mungu duniani katika nyanja mbalimbali. Ndio maana kuna maraisi, wahandisi, madaktari na wengine ambao Mungu amewapa majukumu ya kumuwakilisha duniani.

“Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho.” Yohana 3:6

Mtu anapokuja duniani, huja akiwa amebeba kusudi ndani yake ambalo Mungu amemuwekea. Ndani yake Mungu anakuwa ameweka vitu vya kuweza kumfanya atimize lile kusudi alilomuwekea. Katika ulimwengu wa roho, wachawi wanauwezo wakuona vile vitu na lile jukumu ambalo Mungu amempa mtu na kuanza kumpinga asiweze kutimiza jukumu hilo. Kutokana na kusudi hilo la Mungu ndani ya mtu, mara nyingi husababisha vita kutoka kwa shetani ili ashindwe kutimiza jukumu hilo. 

“Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu.” 1Yohana 5:14

Mtu aliyebeba jukumu kutoka kwa Mungu anakuwa na neema inayo mwongoza na kumsaidia ili kutimiza jukumu lake. Ukitaka uweze kufanikiwa, lazima utembee katika njia ile uliyoitiwa. Mtu aliyeitiwa jukumu flani na Mungu analindwa na Mungu kwa sababu jambo analotakiwa kulifanya ni jambo la Mungu mwenyewe. Yeye anakuwa mwakilishi tu, ila mwenye jukumu hilo ni Mungu mwenyewe.

“Naam, hatasinzia wala hatalala usingizi, Yeye aliye mlinzi wa Israeli.” Zaburi 121:4

Kuna sehemu Mungu anataka upite ili uende kwenye kusudi lako. Ingawa njiani kuna watu ambao wanataka kukuzuia, ila Bwana akiwa upande wako, hakuna kitu cha kukuzuia. Kuna mambo ambayo mtu anapitia, Mungu huruhusu ili kumtengeneza na kumfanya kuwa imara ili aweze kutimiza kusudi alilomuitia.

“Hataogopa habari mbaya; Moyo wake u imara ukimtumaini BWANA.” Zaburi 112:7

Aliyetumwa hana nguvu sawasawa na aliyemtuma, ila aliyetuma humpatia nguvu aliyemtuma ili kazi yake itimie. Wachawi na waganga kwenye ulimwengu wa roho hushindana na mtu aliyetumwa na Mungu, lakini hawawezi kufanikiwa kwa sababu Mungu anamlinda aliyemtuma kwaajili ya kusudi lake. Hivyo, vita yake mtu huyo ni kubwa kwenye ulimwengu wa roho katika ufalme wa giza na silaha yao kubwa ni laana.

“Basi Yesu akapaza sauti yake hekaluni, akifundisha na kusema, Mimi mnanijua, na huko nitokako mnakujua; wala sikuja kwa nafsi yangu; ila yeye aliyenipeleka ni wa kweli, msiyemjua ninyi. Mimi namjua, kwa kuwa nimetoka kwake, naye ndiye aliyenituma.” Yohana 7:28-29

Kuna baadhi ya mambo mabaya yanaruhusiwa na Mungu yampate mtu ili kumpeleka kwenye ukuu wake. Mungu ili kutimiza kusudi lake duniani hutumia vitu vyote kama watumishi wake. Hata wachawi ni watumishi wa Mungu pale inapobidi ili kusudi la Mungu lisimame.

“Tazama, nimepewa amri kubariki,Yeye amebariki, nami siwezi kulitangua  Hakutazama uovu katika Yakobo,Wala hakuona ukaidi katika Israeli.BWANA, Mungu wake, yu pamoja naye,Na sauti kuu ya mfalme i katikati yao. Mungu amewaleta kutoka Misri,Naye ana nguvu kama nguvu za nyati.Hakika hapana uchawi juu ya Yakobo,Wala hapana uganga juu ya Israeli.Sasa habari za Yakobo na Israeli zitasemwa,Ni mambo gani aliyoyatenda Mungu! Tazama, watu hawa wanaondoka kama simba mke,Na kama simba anajiinua nafsi yake,Hatalala hata atakapokula mawindo,Na kunywa damu yao waliouawa.Balaki akamwambia Balaamu, Basi usiwalaani kabisa, wala usiwabariki kabisa. Lakini Balaamu akajibu akamwambia Balaki, Je! Sikukuambia ya kwamba, Kila neno BWANA atakalolisema sina budi kulitenda?” Hesabu 23:20-25

Hakuna mchawi anayeweza kuzuia hatima ya mtu. Hatima yako inafahamika kwenye ulimwengu wa roho katika ufalme za giza. Yapo mambo ambayo mtu ni lazima ayafanye ili kuweza kumruhusu Mungu kumuongoza katika kulitimiza kusudi lake. 

"BONYEZA HAPA KUANGALIA IBADA YA JUMAPILI"

Post a Comment

0 Comments