UFUFUO NA UZIMA
CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 24.05.2026
ASKOFU DKT GERSHOM
MWAKILA
SOMO: KUFUTA
KALENDA ZA KICHAWI
![]() |
Dunia ina wataalamu mbalimbali ambao katika usomaji
wao shuleni, kila walichosoma kiliumbwa na Mungu. Mungu ndiye mtaalamu wa kila
kitu. Kwa mfano, kulingana na Jiografia (elementary), dunia ni miongoni mwa
sayari nyingi zilizopo ulimwenguni lakini sayari tisa pekee ndiyo huzungumzwa
sana.
Wakati wanajiografia wanafanya utafiti kuhusu dunia,
waliona dunia ina mizunguko miwili.
1.
Dunia
kujizungusha kwenye mhimili wake (rotation); matokeo ya dunia kujizungusha
kwenye mhimili wake tunapata majira ya usiku na mchana. Mzunguko huo hukamilika
kwa masaa ishirini na nne (24).
2.
Dunia
kulizunguka jua (revolution). Dunia huzunguka jua kwa muda wa siku 3651/4
au 366. Matokeo ya dunia kulizunguka jua tunapata majira ya mwaka. Majira haya ni
ya aina nne, yaani, i) Kiangazi ii) Masika iii) Vuli, na iv) Kipupwe.
Majira yanasaidia mipango ya shughuli za kijamii. Majira
huendana na shughuli fulani za kijamii; mfano, wakati wa Masika shughuli za
kijamii ni kilimo, na Disemba wakulima huanza kuandaa mashamba. Imani ya
mkulima ipo kwenye majira. Kiangazi ni wakati wa joto.
Mjinga asiyejua majira akiamua kulima wakati wa
kiangazi, ataingia gharama kubwa sana kupata matokeo chanya. Mkulima hapandi
mbegu ili kushawishi majira, ila majira ndiyo huongoza shughuli za watu.
Mfano: Hatuvai sweta ili iwe baridi, ila baridi
husababisha tuvae sweta; hatuvui sweta ili iwe joto, ila joto husababisha tuvue
sweta.
Majira katika uumbaji wa Bwana yameandikwa katika kitabu
cha Mwanzo 1:14, yaani
“Mungu akasema, Na iwe mianga katika anga la
mbingu ili itenge kati ya mchana na usiku; nayo iwe ndiyo dalili na majira na
siku na miaka;”
Mungu ndiye aliyeumba majira na akaweka shughuli
ndani ya majira (Mhubiri 3:1).
Mambo yote chini ya mbingu yamewekwa kuakisi majira yake. Mfano: Lia
kwenye majira ya kulia, na furahi kwenye majira ya furaha; utaonekana mtu wa
ajabu sana kulia kwenye majira ya furaha na kufurahi kwenye majira ya kulia (kucheka
kwa furaha msibani, na kulia kwa huzuni harusini). Katika mambo yote, majira hayatakoma
“Muda nchi idumupo, majira ya
kupanda, na mavuno, wakati wa baridi na wakati wa hari, wakati wa kaskazi na
wakati wa kusi, mchana na usiku, havitakoma.” Mwanzo 8:22.
Hekima na akili kuliko zote ni kuwa na ufahamu wa
nyakati na majira, na kujua cha kufanya na kwa wakati gani ukifanye. Hata majira
haya ya mfungo wa siku 40, baba yetu ameweka mfungo huu kipindi hiki kwani
majira ya watu kupenya kwenye biashara, ajira, kazi, ndoa, kwenye yale
wayatafutayo kwa muda mrefu ni sasa, kwa jina la Yesu.
Majira yote yamepanga matukio. Wanadamu hupanga
ratiba zao kulingana na majira (1 Mambo ya Nyakati 12:32). Kuna wepesi
wa kufanya jambo ikiwa unalifanya katika nyakati na majira yake. Sisi tunaye
baba anayejua nyakati na majira, na watu watende nini ili wapate
wanavyovitafuta.
Yesu alilia akiangalia Yerusalemu na kusema, laiti ungelijua
majira haya, usingetenda hayo utendayo; lakini yamefichwa machoni pako (Luka
19:41-44). Kalenda huwa inafichwa; usipojua kalenda za kichawi vizuri,
adui atakuzunguka, atakujengea boma na atakuangusha wewe na watoto wako. Fanya likupasalo
kufanya ili kuzijua kalenda za adui.
Kulogwa, kuharibu mimba, utasa, magonjwa, laana,
mikosi, ajali, na mambo ya adui kama hayo, yamewekwa kwenye kalenda za kichawi.
Wachawi hupanga kwenye kalenda zao ili muda ukifika uaibike, upate ajali,
uumwe, upate hasara, n.k., na adui ana tabia ya kukamata ufahamu wa mtu ili asijue
majira yake; hapo ndiyo adui anapata nafasi ya kutimiza mambo yaliyo kwenye
kalenda yake ya kichawi. Wachawi huficha kalenda zao ili zisijulikane wazi kwa
watu; huloga akili watu wasijue nyakati na majira (2 Wakorintho 4:4).
Kile ambacho hakijasajiliwa kwenye akili, jicho haliwezi kukiona: Unapaswa kuzirarua,
kuzichana na kuzifuta kalenda za kichawi, kwa jina la Yesu.
Kufanya kazi ndani ya majira kuna neema yake. Kuna mambo
ya kufanya leo yana mahusiano na mambo yako ya kesho. Furaha ya leo ni kwa
sababu ya yale tulitengeneza jana. Tunachotengeneza leo kina mahusiano na watoto,
mafanikio, mega church, au chochote cha mafanikio ya mtu cha kesho. Futa kalenda
leo ili yale ya kesho yatokee kama vile Mungu alivyoyakusudia kwako. Ukiziondoa
kalenda za kichawi, unamuondolea nguvu adui yako.
Tunaomba ili tupate njia kwa Mungu, sisi na wote
wanaotuhusu. Njia zinapatikana kwa kufuta kalenda za kichawi. Ukiondoa kalenda
umeondoa matukio ya kichawi kwa sababu wachawi huloga ndani ya kalenda zao. Ukiondoa
kalenda shetani na wachawi wanabaki wanamangamanga hawana ujanja.
Kuna kalenda za aina mbili; kalenda za Mungu na
kalenda za kichawi.
1.
Kalenda
za Mungu.
Mungu akitaka kufanya jambo
lolote anafuata kalenda yake; haruki hata nukta ya kalenda yake. Mungu ana
majira na nyakati ambazo ameweka kwa ajili ya kufanya kila jambo katika uso wa
nchi.
Nguvu ya kalenda ya Mungu ipo
pale ambapo mtu anakuwa anajua nini cha kufanya katika majira fulani. Usipojua
nini cha kufanya, kalenda ya Mungu inakuwa haina nguvu juu ya maisha yako. Hivyo,
siri ya nguvu ya kalenda ya Mungu katika maisha ya mtu ni akili na hekima ya
kujua yakupasayo kufanya.
Nguvu ya mtu ipo kwenye maarifa
ya mtu; nguvu kidogo, maarifa kidogo; nguvu nyingi, maarifa mengi (Hosea
4:6). Kalenda ya Mungu ina nguvu pale mtu aliyekusudiwa anapokuwa na
maarifa juu yake.
Mifano ya Kalenda za Mungu:
a)
Kalenda
ya kuwatoa wana wa Israeli utumwani.
“BWANA akamwambia Abramu, Ujue
hakika ya kwamba uzao wako utakuwa mgeni katika nchi isiyo yake, watawatumikia
watu wale, nao watateswa muda wa miaka mia nne. 14Hata na taifa lile,
watakaowatumikia, nitawahukumu; baadaye watatoka na mali mengi.” Mwanzo
15:13-14
Wana wa Israeli kuwa utumwani
kwenye nchi ya ugeni, majira yake yalipangwa na Mungu. Kwenye kalenda ya Mungu,
aliwaona wana wa Israeli wengi wakati Ibrahimu hata hajamzaa Isaka.
Mungu alikuwa ameandaa mpango wa
kuwatoa wana wa Israeli utumwani hata kabla ya wakati wa kutoka Misri kufika.
Bwana huona mwisho wa jambo lolote mwanzoni, na huweka kwenye kalenda yake ili
muda unapofika akutendee. Mafanikio yako, ushindi wako, kumiliki kwako, na kuwa
na kila kitu unachohitaji, yapo kwenye kalenda ya Bwana.
Kabla taifa la Israeli kuwepo,
Mungu alimwambia Ibrahimu atawatoa wana wa Israeli utumwani na kuwapeleka
katika nchi ya ahadi. Mungu aliyaona mateso ya wana wa Israeli kabla
hawajazaliwa, na alimuona Farao kabla ya utumwa. Hivyo, kalenda ya Mungu ya
kuwatoa wana wa Israeli utumwani ilikuwepo tangu mwanzo kabla ya taifa la
Israeli kuwepo.
b)
Kalenda
ya Yusufu kuwa Waziri Mkuu wa Misri
Mungu alikuwa ameandaa mpango wa
Yusufu mwana wa Yakobo kufika kwenye nafasi ya Waziri mkuu wa Misri. Mungu aliruhusu
Yusufu auzwe Misri na ndugu zake; Yusufu akafika Misri bila kutumia ghaama
yoyote. Kalenda ya Mungu iliruhusu Yusufu auzwe Misri.
Akiwa mtumwa Misri, Yusufu
alisingiziwa kosa akapelekwa gerezani. Ulikuwa mpango wa Mungu kupitia kalenda
yake kuwa, ili Yusufu afikie hatma yake ni lazima awe mfungwa gerezani. Mungu ana
desturi ya kuruhusu baadhi ya mambo yakukute ili akufikishe kwenye hatma yako.
Mungu akampa ndoto Farao kwa makusudi akijua gerezani yupo Yusufu mwenye uwezo
wa kutafsiri ndoto ambaye alikuwa na mpango nae. Mungu akamuinua mtumishi wa
Farao kumtaja Yusufu kwa Farao kuwa anaweza kutafsiri ndoto ya Farao. Kwa hiyo
tunaona kila hatua aliyoipitia Yusufu ilikuwa na mahusiano ya kumfikisha kwenye
hatma yake; kuuzwa na ndugu zake Misri, kufungwa gerezani na kutafsiri ndoto ya
Farao zote zilikuwa ni njia kwenye kalenda ya Mungu kufanikisha hatma ya Yusufu
kuwa Waziri mkuu wa Misri, na wana wa Israeli kufika Misri.
c)
Kalenda
ya kuzaliwa, kufa na kufufuka kwa Yesu.
Miaka mia saba kabla ya Yesu
kuzaliwa, nabii Isaya alioneshwa (Isaya 1:1) kuwa Yesu atazaliwa
ili kuukomboa ulimwengu. Kuzaliwa kwake Yesu ilikuwa ni mpango wa Mungu; kabla hajazaliwa,
hajafa, hajafufuka, hajatukuzwa Yesu, Mungu alijua yote imekwisha.
Katika maono yake, Isaya alimuona
bikra akichukua mimba na kuzaa mtoto (Isaya 7:14). Ni kanuni ya
Mungu kuwa, akiyaona huyasema hata kabla ya kutokea; yanatokea kwa sababu
yamewekwa kwenye kalenda ya Mungu.
Isaya anaona serikali na kusema
kabla haijakuwapo; miaka mia saba badae, serikali inatokea
“Maana kwa ajili yetu mtoto
amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake;
Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele,
Mfalme wa amani.” Isaya 9:6
Isaya
anasema kuhusu, kuchukua masikitiko yetu na kuteswa kwa ajili yetu, na kwamba
kwa hayo yote sisi tumeponywa, kabla hakujakuwako “Hakika ameyachukua
masikitiko yetu,Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa,Amepigwa
na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu,Alichubuliwa kwa
maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi
tumepona.” Isaya 53:4-5
Miaka mia saba baada ya maono ya Isaya,
ukafika utimilifu wa wakati ambapo Yesu akazaliwa kama ilivyotabiriwa/kama
kalenda ya Bwana ilivyo (Wagalatia 4:4).
Maisha yamejaa maelekezo/kalenda
za Mungu zimejaa maelekezo. Mungu alipanga Yesu azaliwe bethlehemu na
akamuelekeza Yusufu ampeleke Mariamu huko; akamzaa katika zizi la ng’ombe. Baada
ya muda mfalme Herode alitaka kumuua mtoto Yesu, na Mungu akamuelekeza Yusufu amtoroshe
mtoto kwenda Misri. Baada ya mfalme Herode kufa, Mungu akamuelekeza Yusufu kwenda
Nazareti, na badae ulipofika wakati wa kubatizwa, Yesu akabatizwa, na wakati wa
kufa alikufa, na wakati wa kupaa kurudi mbinguni alipaa, na hakuna kilichomzuia
kwa sababu kalenda ya Mungu ilikuwa imewekwa hivyo. Hapo tunaona mchoro mzima
ulipangwa na Mungu hata kabla Yesu kuzaliwa.
Bwana hututukuza kwa kutupenda na
kwa kutuchagua tangu asili (Warumi 8:30, Yohana 17:22). Bwana ametupa
utukufu na heshima. Vyote alivyoviumba Bwana vinapaswa kutuheshimu. Tumewekwa kusimamia
vyote kwa niaba ya Bwana, na mafanikio yatokee sawasawa na kalenda ya Bwana.
Watumishi wa Mungu ni wasimamizi
wa kalenda ya bwana. Bwana amewachagua kusimamia yote ili watu wafanikiwe, watu
warudishwe, watu waponywe magonjwa, wakupigwa wapigwe, wakubomolewa wabomolewe,
wakutukuzwa watukuzwe.
Hata muda tulionao kuhubiri na
kusema neno la Bwana upo kwenye kalenda ya Mungu. Mahubiri yana nyakati;
hayatakuwepo wakati wote. Hii ni mbaya (Amosi 8:11-12).
Ukiona jambo linapatikana kwa
wingi sana ujue lina thamani kubwa. Vile vitu vya umuhimu sana, Mungu amefanya
vipatikane kwa urahisi sana. Vitu vya bure vina gharama sana; kama visingekuwa
vinapatikana bure, ingekuwa ni vigumu sana kuvimudu. Mfano; hospitalini, dawa
za kufubaza virusi vya ukimwi, ARVs, zinatolewa bure kwa sababu kama isingekuwa
hivyo, gharama yake ni kubwa kwa kidonge kimoja na hivyo isingekuwa rahisi
kumudu kwa walio wengi.
Kalenda ya Mungu huwa
haibadiliki. Mungu amesema ataleta njaa ya neno lake majira hayo yakifika. Watu
watalitafuta neno la Mungu lakini hawatalipata. Katika majira haya, neno
linatusisitiza tulitafute sana maadamu linapatikana (Isaya 55:6).
Mungu atupe akili ya kuyafahamu haya ili tusipate kiu ya neno majira yakifika
wakati halipatikani, na kule litakakoenda tuweko.
2.
Kalenda
za Kichawi
Wachawi huandaa mipango yao namna
watakavyoleta uharibifu kwenye maisha ya mtu. Hupanga walete lini, mahali gani
na kwa njia gani uharibifu wao. Huandaa mpango siku nyingi. Utekelezaji wa
uharibifu huo huitwa pia siku ya uovu au siku ya mabaya (Waefeso 6:13,
Zaburi 27:5).
Uharibifu ukiwekwa umpate mtu,
utampata kama haukubatilishwa. Mfano; Hamani alipanga ubaya dhidi ya Mordekai
na kutafuta majira sahihi ya kumuua Mordekai na Wayahudi wote. Hamani
akamshawishi mfalme Ahasuero akakubali na nyaraka zikaandikwa na kusambazwa
mikoa yote. Siku ya uovu ikapatikana kuwa tarehe kumi na tatu ya mwezi wa kumi
na mbili.
Mordekai na Esta wakaazimia
Wayahudi kufunga ili kubatilisha uovu unaopangwa na Hamani. Esta akamwendea
mfalme kinyume na sheria na Wayahudi wakafanikiwa kubatilisha majira
yaliyoandaliwa na Hamani kwa ajili ya uovu juu ya Mordekai na Wayahudi wote (Esta
3:3-15, 4:15-17). Bwana hutujibu kinyume cha sheria kupitia
maombi tumwombayo. Sara alipata mimba na kuzaa kinyume cha sheria.
Bwana huigeuza siku ya uovu kuwa siku ya nuru, furaha, shangwe na amani kwa wana wa Mungu/majeshi ya Bwana. Bwana huitangua kalenda ya wachawi/uovu, na ule mti ulioandaliwa na wana wa uovu ili kuwatundika wana wa Mungu, utatumika kuwatundika wana wa uovu wenyewe
"Naye Mordekai akatoka usoni pa mfalme, amevaa mavazi ya kifalme, ya rangi ya samawi na nyeupe, mwenye taji kubwa ya dhahabu, na joho ya kitani safi na rangi ya zambarau. Mji wa Shushani wakapaza sauti, wakashangilia. Ikawa nuru na furaha na shangwe na heshima kwa Wayahudi. Na katika kila jimbo, na kila mji, po pote palipowasili amri ya mfalme na mbiu yake, Wayahudi wakapata furaha na shangwe, karamu na sikukuu. Hata wengi wa watu wa nchi wakajifanya Wayahudi, kwa kuwa hofu ya Wayahudi imewaangukia."Esta 8:15-17


0 Comments