google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

NDOTO YA MAISHA YAKO

UFUFUO NA UZIMA CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 31.05.2026
ASKOFU DKT GERSHOM MWAKILA
SOMO: NDOTO YA MAISHA YAKO

Kwa vinywa vya mashahidi wa mwili, ndoto huthibitika. Ndoto ni halisia; ndoto ni bayana. Ndoto ya mtu ni hatima ya mtu, ndoto ya mtu ni utajiri wa mtu, ndoto ya mtu ni maisha ya mtu, ndoto ya mtu ni mafanikio ya mtu, ndoto ya mtu ni kushinda au kushindwa kwa mtu. Kwa njia ya ndoto unaweza ukapata, na kwa njia ya ndoto unaweza ukakosa.

Ndoto zipo kwa mtazamo wa aina mbili. Mtazamo wa kwanza ni ndoto anayoota mtu kwa sababu amelala; hutokea mtu akiwa usingizini akaota ndoto kuhusu tukio fulani. Mtazamo wa pili ni ndoto kwa namna ya matamanio ya mtu; mtu kutamani aishi maisha fulani, amiliki nyumba ya namna fulani, awe na mke wa namna fulani, n.k. haihitaji mtu kulala; Mfano wa ndoto ya namna hii ni mtu kusema, “Nimepata kazi ya ndoto yangu”. Matamanio ya mtu kuhusu jambo fulani, ni ndoto ya mtu.

Maarifa ya ndoto ni ya muhimu. Kuwa na matamanio kuhusu jambo fulani / ndoto / maono bila kuwa na maarifa ni jambo baya na ni tatizo. Ukikosa maarifa kuhusu ndoto au maono yako utaangamia, kama ilivyoandikwa katika Hosea 4:6 na

“Pasipo maono, watu huacha kujizuia; Bali ana heri mtu yule aishikaye sheria.” Mithali 29:18.

Kama huna maono au ndoto, huwezi kujizuia; kunaangamiza, kwa sababu unakuwa kwenye hatari ya kupata madhara kwenye kila ufanyalo. Mwenye maono hujizuia kwenye mambo fulani ili aweze kulinda maono na ndoto zake.

Ndoto inatafsiri nyingi. Maana halisia ya ndoto inaweza ikaelezwa hivi; -

1.   Ndoto ni kiashiria cha rohoni cha kuwa mtu atakuwa nani hapo badae.

2.   Ndoto ni mfumo wa maisha unaomuongoza mtu na kuonesha mtu huyo ataishia wapi.

3.   Ndoto ni lugha ambayo Mungu huitumia kuwasiliana na watu wake.

4.   Ndoto ni hati miliki ya mtu kuhusu hatima yake. Hekima ni kupata hati miliki ambayo ni maisha ya mtu.

5.   Ndoto ni mawasiliano ya mtu ambaye ni roho, na ulimwengu wa roho; ni ama mtu anawasiliana na Mungu au Ibilisi.

Mungu ndiye asili ya ndoto. Mungu alikuwa na matamanio yake; hiyo ni ndoto ya Mungu. Mungu alitamani kuwa na mtu wa mfano wake, hivyo, akamfanya mtu kwa mfano wake na kwa sura yake, na mwenye kutenda kazi kama Mungu mwenyewe. Tumefanyika kuwa watu wa ndoto ya Bwana.

Mungu ndiye mwanzilishi wa mipango na Mawazo. Mawazo yetu na mipango yetu haifanani kutokana na makusudi ya Mungu. Kila mtu amebeba kusudi la Mungu juu yake, na hiyo ndiyo sababu ya kutofautiana kwetu, ambayo ndiyo huitwa ndoto ya mtu.

Katika mpangilio wa vitabu vyote vya Mungu vilivyo kwenye Agano la Kale na Agano Jipya, kitabu cha kwanza cha kila Agano (Mwanzo na Mathayo) kimeanza na ndoto. Huu ni mpango wa Mungu.

Mfano1: Katika kitabu cha Mwanzo 20:3, Mungu kamjia mfalme Abimeleki katika ndoto ya usiku akimkemea kwa kumchukua mke wa Ibrahimu (Sara), na Mungu katika ndoto hiyo akamwambia mfalme Abimeleki kuwa kwa jambo hilo atakufa.

Ndoto siyo za kupuuza kabisa kwa maana madhara ya kupuuzia ndoto yanaathari kubwa sana kwenye maisha ya mtu. Watu wengi hudhurika kwa sababu huota ndoto lakini wakiamka kutoka kulala kwao hawachukui hatua kushughulika na ndoto walizoota.

Katika kitabu cha Mwanzo 20:8-9, mfalme Abimeleki alipoamka tu kutoka usingizini alikoota ndoto kuwa atakufa, akaanza kushughulika na ndoto ili kukwepa kifo alichoambiwa na Bwana ndotoni. Tunatakiwa kufanyia kazi ndoto tunazoota kwa sababu, kwa kadili tunavyopuuzia ndoto, madhara yake yanakuwa makubwa. Usiposhughulika na ndoto utaangamia (Mithali 29:1).

Mfano2: “Yakobo akatoka Beer-sheba, kwenda Harani. Akafika mahali fulani akakaa huko usiku kucha, maana jua lilikuwa limekuchwa; akatwaa jiwe moja la mahali pale akaliweka chini ya kichwa chake, akalala usingizi pale pale. Akaota ndoto; na tazama, ngazi imesimamishwa juu ya nchi, na ncha yake yafika mbinguni. Tena, tazama, malaika wa Mungu wanapanda, na kushuka juu yake.” Mwanzo 28:10-22

Yakobo anakimbia baada ya Esau, ndugu yake, kumwibia baraka zake. Akiwa kwenye kukimbia ardhi ya nyumbani kwao, mwenye kuchoka, akaamua kupumzika kwenye kichaka na akapata usingizi.

Akiwa amelala kichakani, mahali pasipofaa, tena hapana chochote cha thamani, Mungu akamjia Yakobo katika ndoto na kumwambia kuwa amempa nchi ya mahali alipolala, yeye na uzao wake. Baraka ya maneno pekee aliyotamkiwa na baba yake, Isaka, Mungu ameigeuza kuwa ndoto ya umiliki wa nchi.

Jambo la muhimu pia, Mungu anajitambulisha kwa Yakobo ndotoni; imeandikwa katika Mwanzo 28:13 kuwa, “Na tazama, Bwana amesimama juu yake, akasema, Mimi ni Bwana, Mungu wa Ibrahimu baba yako, na Mungu wa Isaka; nchi hii uilalayo nitakupa wewe na uzao wako.”

Kiuhalisia, Ibrahimu ni babu yake Yakobo; Isaka ndiye baba yake Yakobo. Hii inatufundisha kuwa kwa Mungu hakuna babu, kuna baba tu. Ulimwengu wa roho hauna babu bali una baba, kwa sababu, baba huwa anammilikisha mwana. Mungu wa baba yake Yakobo amemmilikisha Yakobo ndotoni.

Na sisi tunaye Mungu wa baba yetu, ambaye tunamuomba atumilikishe yale yote tuyaotayo ndotoni kwa habari ya kusudi la maisha yetu, kwa jina la Yesu.

Ndoto imempa Yakobo umiliki ndotoni, kuongezeka ndotoni, na uhakika wa ulinzi ndotoni, mpaka yote ambayo Mungu wa baba yake ameyatamka, yadhihirike mwilini. Mungu hawezi kuruhusu mabaya yatupate kwa sababu anawajibika na kusudi lake kwetu (Mwanzo 28:15, Zaburi 121).

Kama kuna ndoto yoyote ambayo Bwana amekuonesha atahakikisha inatokea vilevile sawasawa na makusudi ya Mungu na mapenzi yake. Ndoto haichagui mahali; hutokea mahali popote bila kujali mazingira ya mtu alipo. Kitu cha msingi ni mtu alale tu.

Hatutakufa mpaka yale aliyosema Bwana katika ndoto juu ya maisha yetu, yatokee. Unachokifanya baada ya Mungu kukuonesha ndoto ni cha muhimu sana. Mahali popote ambapo Mungu anazungumza katika ndoto, yupo mahali hapo; hapo huitwa Nyumba ya Mungu. Yakobo alipopewa nchi na Mungu ndotoni, palikuwa pakiitwa Luzu, akapabadili jina na kupaita Betheli.

Mahali popote upewapo na Mungu, yakupasa upabadili jina ili uweze kupaongoza kulingana na ndoto uliyopewa. Jina unalotoa, Mungu hulisajili sawasawa na ndoto aliyosema. Mwenye kutoa jina ndiye mmiliki. Jina litabadilisha tabia na mambo mengine ili yaendane na jina.

Majina ya mtu yanatokana na tabia ya mtu; mtu anapokuwa na jina la ovyo na tabia ya mtu inakuwa ya hovyo. Ndoto ya mtu inathibitisha mahali pa mtu. Usijidharau kwa maana ni Mungu huwaletea watu ndoto.

Kwa sababu ndoto ya Yakobo ilihusika na kumpa ulinzi, chakula na mavazi mpaka itimie, Yakobo akaweka nadhiri kwa Bwana ya kumtolea fungu la kumi ikiwa ni kweli atammilikisha yale aliyomwambia katika ndoto.

Tusipuuze ndoto, na tukiota ndoto tushughulike na ndoto bila kujali ukubwa wa ndoto na uhalisia wa maisha yetu. Ndoto ya Bwana haina uhusiano na halisia ya maisha ya mtu. Mungu husababisha jambo ili yale tuotayo yatokee. Usijidharau kwa maana ni Mungu ndiye huleta ndoto. Mwenye ndoto hatapeliwi; hata ikitokea anatapeliwa, Mungu hutokea na kumtetea.

Mwanzo 31:10 - 29

Maisha ni mchezo wa ndoto; Yakobo anatembea katika ndoto tu. Mungu anawaona wote wanaocheza na ndoto aliyompa mtu. Labani alijaribu kuchepusha ndoto ya Yakobo kwa kutengeneza utaratibu/kanuni za kumbana Yakobo, lakini Mungu, kwa kumkumbusha Yakobo juu ya Betheli na nadhiri ya Yakobo, akamlinda Yakobo na vyote alivyompa. Mungu ni Mungu ashikaye maagano.

Kanuni na sheria zinaweza kutumika kuzuia ndoto ya mtu, lakini Mungu huzitumia kanuni na sheria hizo hizo kumpatia mtu sawasawa na ndoto yake. Kwa Kadili wanavyokuzuia ndivyo unanyoongezeka, kwa Jina la Yesu.                                                                                              

Adui wa ndoto anayekuzuia kwenda mahali pa ndoto yako, dawa yake ni kumtandika. Kuna wakati unaelekea kupata ila kuna adui anakuzuia usiende kule ulipo kusudiwa; kwakuwa tunaye Mungu aliye hai, dawa ni kumtandika. Mungu aliyemuahidi Yakobo kumlinda, alimkemea Labani katika ndoto na kumuagiza asimsemeshe Yakobo la heri au la shari.

Ukiwa na baba, Mungu wa baba yako anazungumza na adui zako na kuwakemea; Bwana huwapiga adui kupitia mikono ya watumishi wake kwa maana yeye hutenda kazi ndani yetu (Wafilipi 2:14, 1 Samweli 2:10).

Baada ya mfungo huu, Bwana amesema iandike njozi yako ifahamike (Habakuki 2:2).

Miradi ya Bwana inafadhiliwa na Mungu mwenyewe; Yeye anasimamia mradi wa kuigeuza dunia kuwa koloni la Mwana-Kondoo. Mungu anatuambia kuwa mambo hayo hayana budi kutokea, kwa jina la Yesu.

Mfano3: 1 Wafalme 3:4-28

Kuna sadaka ukitoa inamvuta Mungu aje kuzungumza na wewe kupitia ndoto. Unapotoa sadaka inavuta moyo wa Mungu kwa uzuri au kwa ubaya. Unapotoa kwa uzuri Mungu anakuwa anazungumza na wewe na anakupa chochote unachokitaka. Ila kwa kadili unapokuwa hautoi sadaka kwa uaminifu, unaukwaza Moyo wa Mungu.

Mtu anaweza kuomba ndotoni na kupewa majibu ndotoni. Kwenye biblia, mfalme Sulemani alimtolea Mungu sadaka yenye kumfurahisha na kumpendeza Mungu, naye Mungu akamtokea katika ndoto na kumwambia aombe chochote anachotaka ili amtendee. Sulemani akaomba hekima akiwa ndotoni na akapatiwa hekima akiwa ndotoni. Unaweza kupewa maelekezo kwa njia ya ndoto. Ndoto ina mahusiano na mahitaji yako kama vile utajiri au umaskini, uponyaji wako au ugonjwa wako. Unapotoa sadaka unajimilikisha ndoto hiyo, kwa jina la Yesu.

Sulemani alipoamka na kukuta ni ndoto, akaanza kushughulika na ndoto. Akamtolea Bwana sadaka. Katika biblia, hakuna mtu aliyepuuzia ndoto.

Mfano4: Ndoto inaweza kusahaulika. Ndoto ikisahaulika haimaanishi kuwa haipo; ipo ila imefichwa na wachawi. Mfalme Nebukadreza aliota ndoto iliyomtia hofu ila alipoamka hakuikumbuka. Pamoja na kuwa Nebukadreza aliisahau ndoto aliyoota, alipoamka alishughulika na ndoto. Mungu hutenda kazi vizuri kwenye changamoto kubwa inayohitaji majibu ya ki Mungu. Danieli, mtu wa Mungu, peke yake aliweza kumkumbusha ndoto yake na akatoa tafsiri ya ndoto hiyo (Danieli 4).

Biblia katika kitabu cha Ayubu 20:8, inatufundisha pia kuwa ndoto inaweza kupaa.

Mambo ya hatari ambayo ndoto inawezakuleta kwenye maisha ya mtu; -

1.   Ndoto inaweza kukuletea maadui wa ndani;

Kwenye biblia Yusuph aliota ndoto na kuwasimulia ndugu zake, na wale ndugu zake wakamchukia na kumuuza Misri. Ndoto yako inaweza ikasababisha uchukiwe na ndugu zako, na jamaa zako, na watu wako wa karibu (Mwanzo 37:5-8).

Hata ukichukiwa wewe endelea kuota; usibadili ndoto na maono yako kwa sababu ya chuki za ndugu zako na chuki za marafiki zako. Ndoto haiachwi kizembe; kuwa thabiti kwenye ndoto zako leo na siku zote (Mwanzo 37:9).

Wazazi wanaweza wakakunyamazisha, lakini kama ndoto inatoka kwa Bwana, haiwezi kunyamazishwa. Kupigwa vita, na vizuizi kutoka kwa adui wa mtu haibadilishi ndoto ya mtu. Mungu humpa mtu ndoto kwa sababu amemuona ni wa maana. Usibadilishe msimamo wako. Mungu aliyekuchagua anakulinda (Warumi 8:29-30).

Hakuna silaha wala jambo lolote kinyume na ndoto yako litakalofanikiwa, asema Bwana (Isaya 54:17).

2.   Ndoto inaweza ikakufanya ufe kabla ya wakati;

Usipojua cha kufanya/kutenda, unaweza ukafa. Mungu anataka upenye na usife. Watu wengi wenye ndoto kubwa wasipojua cha kufanya wanaweza wakafa kabla ya wakati. Ndugu wa Yusuph walifanya mashauriano ili wamuuwe kwa sababu ya ndoto zake.

Ndoto ina tabia ya kuonekana kutokea mbali. Hata ukiwa bado mdogo wachawi wanaweza kujua, nao wakakutengenezea matukio ya kukuua. Lakini Bwana yeye anatulinda ili ndoto zetu zitimie (Zaburi 118:17).

Yesu alipozaliwa tu mamajusi wa Mashariki ya mbali wakaona kutokea mbali ndoto ya Yesu kuwa atakuwa mfalme. Naye nabii Isaya anaitangaza ndoto ya Yesu kabla Yesu hajazaliwa (Isaya 9:6). Wachawi wanaweza kumloga mtu mwenye ndoto kabla hajazaliwa ili kukwambisha ndoto yake. Vita kubwa aipatayo mtu ni sababu ya wachawi wameiona ndoto ya mtu kutokea mbali. Kama Mungu alivyomuokoa Yakobo, atatuokoa na adui wote wanaopambana na ndoto zetu (Zaburi 68:20).

Kila ndoto ina adui wa ndoto. Mungu wa Yakobo ndiye Mungu wangu; ameapa kunilinda mpaka yale yaliyo kwenye ndoto yangu yatimie. Mungu wa baba yangu ndiye Mungu wa Yakobo. Adui wote watainama mbele zangu. Mamlaka zote za rohoni zitainama.

Adui wa ndoto anaweza akatengeneza matukio kinyume na ndoto ili kukwamisha ndoto isitimie. Mfano; kama ndoto ya mtu ni kuwa askari, adui anaweza akasababisha matukio ya magonjwa kwa mtu ili kumuondolea ukakamavu na utimamu wa akili.

Mwili hulala lakini roho ambayo ndiye mtu mwenyewe, halali. Mwili ulalapo, roho huendelea na kuona (hiyo ndiyo ndoto). Kuamka kwa mwili hakusimamishi matukio ya roho.

Ndoto ina mahusiano na kibali cha mtu. Kuota unalishwa chakula ni mbaya sana kwa sababu maadui wa giza wanapomlisha mtu vyakula ndotoni, wanakuwa wanaimarisha matatizo waliyoyaweka kwa mtu huyo. Matatizo hayo huondoa kibali cha mtu. Kwa kulishwa vyakula ndotoni, mambo mengi katika maisha yanaharibika na vifungo alivyofungwa mtu vinaimarika.

Unapokula chakula cha kichawi kuna tabia zinabadilika na kuiona kazi ya Mungu ni ya kawaida, na kuifanya kazi ya Mungu kwa ulegevu; na ndivyo unavyokosa kibali.

Kuna watu huota ndoto wakinyolewa nywele. Maana ya kunyolewa nywele ndotoni ni kuwa kuna nguvu ya mtu inaondolewa kwenye maisha yake. Kuna wengine wanaota wakichanjwa chale mwilini. Haya yote yanafanyika ili kuimarisha matatizo ya mtu.

Kanuni ya usingizi ni ileile; ukilazwa ni ama unawekewa kitu au unaondolewa kitu. Mfalme Sulemani alipolala, Mungu alimuwekea hekima. Pambana sana kuondoa vizuizi kwenye maisha. Mungu huleta msaada kupitia maombi; omba sana mchana na usiku. Ni kwa sababu ya dhabihu na sadaka ya kueleweka, Mungu hummilikisha mtu mambo yote ya ndoto yake. Toa sadaka ambayo haitaleta ugomvi kati yako na Mungu. Toa kwa ukamilifu “Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema BWANA wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la.” Malaki 3:10

BONYEZA HAPA KUANGALIA IBADA YA JUMAPILI

Post a Comment

0 Comments