UFUFUO NA UZIMA
CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 14.06.2026
ASKOFU DKT GERSHOM
MWAKILA
SOMO: VITA YA MTU
ANAYEKARIBIA KUPATA
![]() |
Mara nyingi mtu akipakwa mafuta kuwa masihi wa Bwana,
hutazamia kapata hitaji lake au kuliishi lile kusudi la maisha yake. Kupakwa mafuta
ni kutengwa kwa ajili ya kusudi maalumu; ni kitendo cha uhakika wa kupata
kusudi.
Mafuta yanamlinda mtu asidhurike, asizuiwe na asiguswe.
Unapopakwa mafuta unaelekea kupata. Unapoelekea kupata kuna vita inainuka
kukuzuia usipate. Akili ni kumshambulia adui pale unapohisi anataka kukuzuia. Vita
ipo kwenye kila kitu ambacho mtu anakitaka; lazima tupigane vita asubuhi,
mchana, jioni na usiku. Vita ilikuwepo tangu enzi na ilianzia mbinguni ambapo
mtesi wetu alitupwa ulimwenguni, hivyo yupo. Kwa Kadiri vita ya mtu inaonekana
ni kubwa, ndivyo kile kilicho ndani ya mtu ni kikubwa, kwa maana hata Mungu ni
Mungu wa vita.
Mtu aliyefunga siku arobaini ni lazima akutane na mitego
ya shetani. Biblia inatufundisha kuwa, wale wote waliofunga siku arobaini, walipomaliza
mfungo, shetani alijionesha kwao. Nabii Musa baada ya kufunga siku arobaini,
aliposhuka katika mlima Holebu, aliona uasi kwenye kambi ya mji aliokuwepo.
Yesu alipomaliza kufunga siku arobaini, akiwa
mlimani, alitokewa na shetani na akajaribiwa. Shetani anapokuja kwa watu
waliofunga siku arobaini, huja kupambana na lile kusudi la kufunga kwao;
shetani huja kile kipindi ambacho mtu anakaribia kupata, hivyo vita ya
aliyefunga siku arobaini ni maalum (special). Sisi pia, baada ya kumaliza mfugo
wetu wa siku arobaini, vita tunayopigana ni maalum kwa sababu tunaelekea kupata
“Na Yesu, hali amejaa Roho
Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini
nyikani, akijaribiwa na Ibilisi. Na siku hizo alikuwa hali kitu; hata
zilipotimia, aliona njaa. Ibilisi akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu,
liambie jiwe hili liwe mkate. Yesu akamjibu, Imeandikwa ya kwamba mtu
hataishi kwa mkate tu. Akampandisha juu, akamwonyesha milki zote za
ulimwengu kwa dakika moja. Ibilisi akamwambia, Nitakupa wewe enzi hii
yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi mwangu, nami humpa ye yote kama
nipendavyo. Basi, wewe ukisujudu mbele yangu yote yatakuwa yako. ”Luka
4:1-14
Uwapo kwenye mfungo wa siku arobaini au baada ya mfungo,
yakupasa uwe makini sana kwa maana shetani huja kwa sura ya ufumbuzi wa hitaji
lako, lakini huo ni mtego. Shetani hujua mahitaji yetu tuyaombayo kwa Bwana,
hivyo, hutujaribu kwa sura ya kujibiwa maombi yetu, na unapoingia kwenye mtego
huo, mwisho huwa ni mbaya. Kuna wakati mtu hufikiria kuwa Mungu anachelewa
kujibu maombi, lakini biblia inatufundisha kuwa Mungu hawahi wala hachelewi ila
hujibu wakati wa utimilifu wa wakati; unapokaribia utimilifu wa wakati, shetani
hujitanguliza kuharibu kusudi la Mungu kwa mtu.
Shetani ni baba wa uongo; akiahidi kukupa chochote,
hulenga kukukwamisha usiyapate yale Mungu ameahidi kukupa. Shetani anajua ya
kuwa, kupitia uongo wake, aliiba milki yote ya ulimwengu, hivyo hutumia ujanja wake
ili aendelee kubaki nayo; ni ahadi ya Mungu yenye utimilifu kwa yeyote kuwa mtu
akifanikiwa kurudisha vile vilivyoibiwa na shetani, Mungu atalikuza jina la mtu
huyo na atamzidisha katika dunia kwa sababu amefanikiwa kuirudisha asili ya
Mungu na kusudi la uumbaji wake.
Njia ya Mungu kutimiza kusudi lililo ndani ya mtu,
ni njia ngumu yenye sura ya kukatisha tamaa, lakini mwisho wake ni mwema na
wenye kumiliki vyote. Yesu, ili aukomboe ulimwengu uwe koloni lake, lilikuwa ni
kusudi la Mungu apitie mateso mengi na kejeli kwa ajili ya watu wote.
Njia ya shetani ni nyepesi na yenye kubembeleza. Yesu
alijaribiwa na shetani kuwa “ukisujudu mbele yangu yote yatakuwa yako”;
kwa sababu ahadi za Bwana ni za kweli, Yesu alichagua njia ngumu yenye mateso,
nalo jina lake ni kuu, kubwa na lenye kuponya wote wenye uhitaji.
Kabla Mungu hajalikuza jina “Yesu” kuwa jina
lipitalo majina yote, Yesu alipitia dhiki, kutengwa, kejeli, lakini alivumilia mateso
hata akafa akazikwa na kufufuka kwa ajili ya wote watakaompokea wawe na uwezo
wa kufanyika wana wa Mungu. Yeye akataliwaye na watu, ama ndugu zake au jamii
yake, asikate tamaa kwa maana kuna mahali jina lake lina thamani na anasubiriwa;
maumivu ni sababu ya kukataliwa.
“Alikuwako ulimwenguni, hata kwa
yeye ulimwengu ulipata kuwako, wala ulimwengu haukumtambua. Alikuja kwake,
wala walio wake hawakumpokea. Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa
kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake;” Yohana 1:10-12
Kuna watu wanakuza majina yao kwa njia za mitandao
na wengine wanatumia machawa lakini majina yao yanakuwa ya kawaida, ila ukiirudisha
dunia katika njia ya Bwana Mungu anakupa jina lipitalo majina yote. Unapoamua kuichagua
njia ya Bwana, kuna kukataliwa na familia, kutengwa na watu, kukejeliwa,
kusengenywa ila mwisho wake ni mzuri. Jipe moyo, usikate tamaa kwa maana hata Yesu
alienda kwa walio wake lakini hawakumpokea.
Biblia imejaa watu waliokataliwa. Wapo watu ambao
wako na nia ya kupindisha kesho ya mtu au kupindisha njia ya mtu, lakini Mungu
anayo njia ya kumrudisha mtu katika njia impasayo mtu kuiendea. Mtu awapo mgumu
kwa Mungu, Mungu humvuta mtu huyo kwa njia ngumu. Hivyo ni afadhali ujilegeze
kwa Mungu ili Mungu akupeleke kwenye kusudi lake kwa njio isiyo ngumu; Mungu kwa
wapole anakua mpole, mnyenyekevu kwa wanyenyekevu, na mgumu kwa wagumu.
Mfano1;
Paulo ambaye ndiye alikuwa Sauli, Mungu alitumia njia ngumu kumrudisha katika kusudi
lake kwa sababu Sauli alikuwa mgumu. Mungu alimpiga Sauli na upofu ili kulegeza
moyo wake arudi kwenye kusudi. Baada ya kuwa Paulo, watu waliomfahamu kama
Sauli walimkataa, naye akaenda kwa mataifa.
Mfano2;
Daudi mwana wa Yese alikataliwa na baba yake kwenye tukio la kutafuta mfalme wa
nchi na masihi wa Bwana. Daudi alitengwa na familia ya baba yeke nyuma ya
jangwa ili nabii Samweli mwenye pembe ya mafuta asiweze kukutana naye. Biblia inatufundisha
kuwa, yeye aonekanaye kwa macho ya watu kuwa ndiye, sio lazima mbele za Mungu
awe ndiye, na yule asiyeonekana anafaa machoni pa watu yawezekana kabisa ndiye
anayefaa mbele za Mungu. Mungu haangalii kama wanadamu waangaliavyo; Yeye
huangalia roho. Pamoja na kuwa nabii Samweli aliona watoto wa Yese (isipokuwa
Daudi) wanasifa za mfalme, Mungu aliwakataa wote, na mbele za Mungu, ni Daudi
peke yake mwenye kustahili kupakwa mafuta.
Daudi alifichwa nyuma ya jangwa lakini mafuta
yalimtafuta. Nabii Samweli na familia ya Yese hawakula wala kunywa mpaka Daudi
aliye nyuma ya jangwa afike sawasawa na kusudi la Bwana. Hata sisi zile siku
tulizofunga ni sawa na tulikuwa nyuma ya jangwa; tumemaliza mfungo na sasa tumetoka
jangwani tukiwa na mafuta, na tunaenda huko tunakosubiriwa kwa maana, huko kuna
watu ambao hawali na hawanywi wala hawakai, wanatusubiria; wale wanaokataliwa
sana, ndio hao wenye kesho kubwa sana, na ndio hao wenye jina kubwa sana, na ndio
hao wanaosubiriwa sana, na ndio hao ambao mwisho wao ni mkubwa sana, kwa maana
kwa Mungu hakuna kuchelewa na hakuna kuwahi ila kuna utimilifu wa wakati
“Hata ulipowadia utimilifu wa
wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya
sheria,” Wagalatia 4:4
Ni vyema kuijua njia iliyo sahihi; imeandikwa katika
Mithali 14:12, 16:25 kuwa, “Iko njia
ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti.”
Njia isiyo sahihi ni moja tu lakini matokeo yake ni njia nyingi za mauti,
mfano, ukiiendea njia ya shetani (njia moja yenye kuanza na mvuto) itazalisha njia
nyingi za mauti kama mauti ya kazi, mauti ya ndoa, mauti ya biashara n.k., lakini
ipo njia inayoanza kwa kutengwa, kukataliwa, kuwa na huzuni lakini mwisho wa njia
hiyo ni mwema (njia ya Yesu).
Mtu achaguaye njia ya Yesu dhidi ya njia ya shetani atafanikiwa.
Yesu aliwapa ahadi wanafunzi wake / Thenashara na watu wote kuwa yeyote
aliyeacha mambo yake kwa ajili ya jina lake (Yesu), atapokea mara mia na
ataurithi uzima wa milele (Mathayo 19:29). Ahadi hii ya Yesu ilionekana
kuleta mashaka kwa baadhi ya wanafunzi wake, kwa mfano, Yesu anawaambia wanafunzi
wake kuwa atateswa, atakufa, atazikwa na atafufuka siku ya tatu; inawezekana
vipi kufa bila kutimiza ahadi ya kuwapa “mara mia” ya vyote walivyoviacha kwa ajili
ya jina lake?
Kwa sababu mtu akikaribia kupokea sawasawa na kusudi
lake, shetani hufanya hila ili kuharibu kusudi la Mungu, shetani akamwingia
Yuda na kumwongoza kumsaliti Yesu kwa kumuuza kwa vipande thelathini vya fedha.
Hili linatufundisha kuwa kuomba kunahitaji uvumilivu kwa maana Mungu hujibu wakati
unapotimilika; unaweza ukamuomba Mungu akupatie kazi, ila wakati utimilifu wa
ki Mungu wa kupata kazi uitakayo haujawadia, shetani anaweza akakuletea fursa
ya kazi ambayo siyo ya uwezo wa Mungu, na ukiingia ndiyo inakuwa chanzo cha
kuanguka kwako kwenye mauti nyingi. Shetani anaweza kabisa kumuingia mtu
aliyekaribia kupata ili akate tamaa.
Mungu hufuata ukamilifu wa wakati; hakuna neno litokalo
bure kutoka kwa Bwana (Isaya 55:11). Ahadi ya Bwana ya kupata “mara
mia” ilikuwa ni kanuni ya ki Mungu iliyohaririwa kwa matukio ya ki Mungu. Yatupasa
kuelewa litupasalo kufanya kwa wakati huo. Kanuni ya Mungu kwa Thenashara
ilikuwa kuwapa mara mia baada ya Yesu kusulubiwa, kufa, kuzikwa na kufufuka
siku ya tatu, ndiyo maana, wanafunzi wengine wa yesu walipata mara mia
isipokuwa Yuda aliyemsaliti Yesu.
Yesu aliasisi njia yake kwa mateso na akaikamilisha ili
ahadi ya kupokea mara mia iwapate watu wote. Alipomaliza kuitengeneza njia yake,
akatuachia Roho Mtakatifu atusaidie kuenenda katika njia yake. Wanafunzi wa
Yesu hawakuhitaji tena kupitia mateso ili wapate majibu ya mahitaji yao; jina
la Yesu linatosha kutatua yote.
Biblia inatufundisha kuwa, siku ya Pentekoste upepo
wa nguvu uliwaingia wanafunzi wa Yesu wawapo pamoja katika kusali, wote
wakajazwa Roho Mtakatifu wakaanza kunena kwa lugha; majibu ya mahitaji yao/ile
ahadi ya “mara mia” ikaanza kufanya kazi (Matendo ya Mitume 2:1-4).
Wanafunzi wa Yesu walikabidhiwa jina la Yesu; hiyo ni fimbo waliachiwa (Yohana
14:13). Walitangaza jina la Yesu kwa wote wenye uhitaji, waliponya wagonjwa,
waliwafungua wenye vifungo, walitumia fimbo yao kuwaongoza watu kwenye mahitaji
yao; hawakuhitaji elimu au Hekima za kidunia kwa maana fimbo waliyopewa ni
zaidi ya hivyo. Ukiwa pamoja na Yesu unafanya yale aliyoyafanya; tumia fimbo
uliyopewa ili ufanye yale aliyofanya yye aliyekupa fimbo.
Wanafuzi wa Yesu walipokutana na kiwete hawakumpa
fedha wala dhahabu ila kwa jina la Yesu wakamponya kiwete yule. Yule uliyenae
ndivyo utakuwa wewe; wanafunzi wa Yesu walifanya yale aliyoyafanya Yesu, kwa sababu,
alivyo baba ndivyo alivyo mwana. Ukitembelea mafuta ya anayekuongoza utafanya
kama yeye.
Sisi tuna baba ambaye ametupa fimbo/mafuta tutumie
kupata majibu ya mahitaji yetu. Hatuoni aibu
kutembea/kufanya yale afanyayo baba yetu kwa maana sisi na baba tu umoja (Warumi
1:16, Yohana 10:30). Kwa mafuta na moto wa baba, wengi
tumefanikiwa. Kuna jambo moja ambalo yatupasa kujifunza ili kukamilisha kanuni
ya mimi na baba tu umoja, nalo ni kutoa.
Mwenye kutoa hakaukiwi kupata, ila asiyetoa
anaelekea uhitaji. Kutoa ni mlango wa kupokea. Kutoa ni kanuni ya Mungu; Mungu
alimtoa mwanaye wa pekee ili aupate ulimwengu wote. Baada ya kumtoa mwanaye wa
pekee, sisi sote tumekombolewa kwa damu ya mwana wa kwanza wa Mungu, Yesu. Kwa kipimo
kile kile cha Yesu kuwa mwana wa Mungu, ndivyo sisi tumefanyika kuwa wana wa Mungu
“Tazameni, ni pendo la namna gani
alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii
ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye.” 1 Yohana 3:1
Ibrahimu na Sara walikubali kumtolea Mungu Isaka, mtoto
wao, naye Bwana akalikuza jina la Ibrahimu na kumzidisha katika dunia. Upenyo unakuwa
kwenye kutoa cha pekee; kidogo ulichonacho, kimetoka kwa Bwana
“Mtumaini BWANA kwa moyo wako
wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri
yeye, Naye atayanyosha mapito yako.” Mithali 3:5-6
Sadaka huwa haitolewi kwa watu au kwa walemavu; huo ni
msaada siyo sadaka. Sadaka inatolewa kwa Mungu au miungu. Ukihitaji Mungu
akutendee jambo lako ni lazima utoe sadaka. Ukipanda maombi utavuna maombi; usipande
kunena kwa lugha ukategemea kuvuna hela, kama unahitaji fedha, lazima umtolee Mungu
sadaka ya fedha; baraka ya fedha inakuja kwa kutoa fedha (Wagalatia 6:7).
Shetani anaijua kanuni ya kupata, ndiyo maana anabana sana kwenye matoleo
kanisani. Sadaka huvuta Roho wa Mungu; Sadaka ya Kornelio iliwavuta malaika
waende kwake, na sadaka ya Habili ilimuinua.
Ni kanuni ya Mungu kumtolea zaka na dhabibu. Zaka na
dhabihu lazima ziwe za ukamilifu, vinginevyo ni kuleta laana. Laana ni kinyume cha
baraka, na ni mlango kwa mtu afikwe na mabaya yote. Tunatoa kwa Mungu kwa maana
ndiye atoaye nguvu za kupata utajiri (Mithali 23:4). Mtu anaweza
akawa amefunguliwa kwenye mambo yote, lakini hafanikiwi kwa sababu ya kukiuka
kanuni ya Mungu ya utoaji. Usipotoa au ukatoa sadaka/zaka/dhabibu isiyokuwa ya
ukamilifu, shetani hutushtaki kwa Mungu, Naye Mungu husimamia kanuni yake.
Binadamu humwibia Mungu na hivyo kupata laana kwenye
yote wafanyayo. Laana inayotokana na kumwibia Mungu zaka na dhabihu, haitoki
kwa kubadilisha unachofanya; badilisha nia, Mungu huponya laana. Upenyo wa mtu
kwenye mambo ya fedha umelala kwenye kuijua kweli. Laana za wachawi au wazazi
tukimwomba Mungu tunaziondoa, ila laana ya Mungu hakuna maombi yanayoweza
kuiondoa.
Tunamtolea Mungu zaka na dhabihu ili nyumbani mwa
Bwana kuwe na chakula. Chakula katika nyumba ya Bwana maana yake ni uponyaji. Hivyo,
tunamtolea Bwana ili nyumba ya Bwana iwe na uponyaji. Mungu ameturuhusu
tumjaribu kwa kumtolea; tumtolee Mungu kwa ukamilifu ili tusiwe na hatia mbele
zake
“Je! Mwanadamu atamwibia Mungu?
Lakini ninyi mnaniibia mimi. Lakini ninyi mwasema, Tumekuibia kwa namna gani?
Mmeniibia zaka na dhabihu. Ninyi mmelaaniwa kwa laana; maana mnaniibia
mimi, naam, taifa hili lote. Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo
chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, asema BWANA wa majeshi;
mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata
isiwepo nafasi ya kutosha, au la. Nami kwa ajili yenu nitamkemea yeye
alaye, wala hataharibu mazao ya ardhi yenu; wala mzabibu wenu hautapukutisha
matunda yake kabla ya wakati wake katika mashamba, asema BWANA wa majeshi.” Malaki
3:8-11.
Kanuni ya fedha ina njia zake, na mojawapo ya njia
hizo ni uaminifu kwenye kutoa fungu la kumi. Kama mtu siyo mwaminifu kwa Mungu
kwenye kutoa, mtu huyo ni mwizi anayemuibia Mungu. Kumuibia Mungu ni mbaya sana
kuliko kuwaibia watu; tubu uanze upya uaminifu na Bwana kwenye kumtolea zaka na
dhabihu.


0 Comments