UFUFUO NA UZIMA
CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 12.07.2026
ASKOFU DKT
JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO: WAMEOGOPA
HATIMA YAKO WAKAKUFICHA NYUMA YA JANGWA
Hatima ni utakavyomalizia maisha yako, au mustakabali
wa maisha ya mtu. Kiswahili hakitoi maana timilifu ya neno hatima. Unaondoka
duniani unapomaliza hatima yako. Somo hili kimsingi siyo mahubiri lakini ni maelekezo
kutoka kwa Mungu ili kutusaidia kumaliza mbio zetu hapa duniani kwa nguvu na
ushindi. “Wameogopa hatima yako wakakuficha nyuma ya jangwa” inamaanisha adui
ameiona hatima na kusudi kubwa la mtu hapa duniani hivyo anamzuia mtu asiishi
hatima hiyo kwa kumtenga na njia impelekayo mtu huyo kwenye hatima; jangwa,
kama linavyotajwa kwenye somo, linawezakuwa pingamizi lolote la kuzuia hatima,
mfano umasikini.
Nchi ya Israeli walilazimika kuchagua Rais kipindi
cha utawala wa mfalme / Rais Sauli, lakini nchi nzima walikuwa wahajui Rais
atakuwa nani. Kwa utaratibu wa kumpata kiongozi wa nchi kwa wakati huo, Mungu
alikuwa anamtumia nabii aliyemchagua kummiminia mafuta masihi ili awe Rais. Kipindi
cha utawala wa Sauli, nabii wa Mungu alikuwa Samweli aliyefunuliwa na Mungu
kumpaka mafuta mtu mwingine awe Rais. Katika maisha ya sasa, kitendo hiki cha kummiminia
mafuta mtu mwingine awe Rais wakati Rais yupo, kingetosha mtu kushitakiwa kwa kutenda
kosa la uhaini.
Mungu alimtuma nabii Samweli abebe pembe ya mafuta
na kwenda kwa familia ya Yese kumpaka mafuta masihi wake. Samweli akazungumza
na Mungu kuhusu mfalme Sauli ikiwa atasikia kuwa anampaka mafuta mtu mwingine,
lakini Mungu akamwambia Samweli aende kwa namna ya kutoa dhabihu, na Mungu
atamuongoza na kumpatia nguvu.
Samweli akaenda kwa familia ya mzee Yese, na wakati
huo, familia ya mzee Yese hawajui kama kuna mtu atakuwa Rais kutoka kwenye
nyumba yao. Wakati mtu haijui hatima yake, Mungu anaweza akamtumia mtumishi wake
mwenye uwezo wa kujua hatima ya mtu ili kumuelekeza mtu huyo kuiendea hatima
yake.
Kwenye nyumba ya Yese, Samweli anamkuta mzee Yese na
watoto wake saba wa ndoa wenye sifa za ukakamavu na ni wanajeshi; hata hivyo,
hakuna kati yao ambaye Samweli, kwa macho ya mbinguni, alimuona anatakiwa
kumiminiwa mafuta. Kwenye maisha, siyo mbio zako zinazoweza kukupa ushindi ila
wakati na Bahati huwapata wote (Mhubiri 9:11). Samweli alipomuuliza
mzee Yese kama kuna mtu mwingine kwenye nyumba yake, maana Samweli alijawa
shauku kuwa masihi wa Bwana anatoka kwenye nyumba hiyo, mzee Yese akamjibu kuwa
yupo mmoja mdogo mdogo ambaye hajamuita kwa sababu hata muonekano wake hauwezi
kumfanya awe mfalme.
Makuhani wa Mungu huona hatima ya mtu; ni vyema
kujionesha kwao, wakikuona wanakujua. Moyo wa mtu unafisha sana; namna mtu anavyojiona
ndiyo au siyo, kwa Mungu ni tofauti. Unaweza ukajiona hufai kwa kazi fulani,
lakini sivyo, kuna jambo lipo kubwa umebeba zaidi ya maisha uliyonayo; jambo la
msingi ni kulijua. Kutokujua kunatupa maswali mengi sana, mfano; Nini thamani
ya maisha? Je, tunaishi ili tuje kufa; Je, tunalala ili siku iishe? Hapana, hakuna
kipya hapa duniani.
Wote tumetumwa ili tufanye kile ambacho Mungu
angekuja kukifanya mwenyewe. Kuna kusudi ambalo Mungu ameliweka ndani ya mtu.
Je, ni nini kinachofanya mtu aishi hadi muda huu? Ni nini kilitokea hadi sikufa
nilipokuwa tumboni wakati wa mimba au kwenye ile ajali? Jibu ni kwamba, kuna
kusudi lipo ndani ya mtu ambalo kama hautalitekeleza Mungu atakuhukumu. Yampasa mtu aamke ili agundue kusudi lake na
kulifanya; lazima kila mtu ajione ana kitu amebeba. Lazima mtu achambuke mwili
na roho ili atende lile lililo la roho ambalo ametumwa kulitenda; CHAMBUKA!
Mfano wa ‘kuchambuka’ upo kwenye mfumo wa Kemia; Sodiamu
(Sodium – Na) na Kloreni (Chlorine – Cl) zinapoungana kwa pamoja zinatengeneza chumvi
tunayotumia kwenye chakula, lakini zinaweza kutenganishwa zikatengana na kila
moja ikafanya kazi nyingine; vivyo hivyo, kuna roho na mwili ambavyo vikiungana
anapatikana mwanadamu na vikitengana kuna mwili kurudi kwenye mavumbi na roho
kurudi kwa Mungu. Kwahiyo, ni vizuri kuonekana kwa watumishi wa Mungu ili
wakuone yale usiyoweza kuyaona (mambo ya rohoni).
Kwakuwa Daudi alifichwa nyuma ya jangwa, na Samweli
kuwa na shauku, Samweli akasema hakuna kula wala kunywa mpaka Daudi aletwe. Hapa
tunafundishwa kuwa, hata kama wamekuogopa sana wakakupeleka nyuma ya jangwa ili
usionekane / usifikie hatima yako, watakufuata wao wenyewe. Alipofika Daudi na
kuonwa na nabii Samweli, na kupangwa upya ili kujua nani anastahili kupakwa
mafuta, hakuna kilichobadilika kwa wale saba; uwepo wa Daudi tu ukamfanya nabii
Samweli kusema masihi wa Bwana yupo katikati yao, na akammiminia pembe ya
mafuta.
Kwanini walimficha Daudi? Daudi alikuwa mtoto wa nje
ya ndoa; wale watoto saba walizaliwa na mama mmoja isipokuwa Daudi, lakini wote
walikuwa watoto wa mzee Yese (Zaburi 51:5, Zaburi 22:10).
Hatima ya Daudi ilitoka kwa Mungu mwenyewe na hakuwepo wa kuizuia; umasikini
hauwezi kuzuia hatima.
Hatukuanza siku ya kuzaliwa (Mwanzo 2:7);
tulikuwepo kabla hatujazaliwa. Tulikuwepo ndani ya Mungu; wakati anaumba
tulikuwa naye. Bibilia inatufundisha kuwa;
1.
“Mtu
kwa mavumbi ya ardhi” ni mwili.
2.
“Mtu
nafsi hai” ni roho.
Mimi siyo mtu kwa mavumbi ya ardhi; mimi ni mtu nafsi
hai (Warumi 7:12, Waefeso 3:16). Mimi ni mtu wa
ndani. Aliyenibeba ndiye “mtu kwa mavumbi ya ardhi” ambaye atarudi mavumbini,
lakini mimi hakuna wa kunirudisha mavumbini kwa sababu sijatokea huko
“kwa jasho la
uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo
ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” Mwanzo 3:19.
Mimi nilitolewa kwa Mungu nikaingia ndani ya mwili
kwa pumzi ya Mungu; nitarudi kwa Mungu (Mhubiri 12:7). Ninaweza nikawa
kwenye hatari yoyote lakini siogopi kwakuwa hakuna wa kuniua kwa sababu mimi
siyo mwili (Mathayo 10:28); yeyote unayenitafuta, HUNIUI (Zaburi
91:10). Aliyetolewa kwa Mungu atarudi kwa Mungu; Yesu alitolewa na
Mungu, alipomaliza kazi yake akarudi kwa Mungu
“Kwa maana jinsi hii Mungu
aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye
asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Yohana 3:16.
Mtu wa kwanza (Adamu) hakuzaliwa wala hakunywa
maziwa; alibuniwa na kuumbwa na Mungu. Alianza kwa kuwepo na kupuliziwa pumzi
ya uhai. Wazo/fikra huzalisha itikadi; wazo/fikra duni huzaa itikadi dhaifu. Wakati
Mungu akimuumba Adamu alikuwa na wazo/fikra bora zilizozaa itikadi imara. Mungu
alipokuwa anaumba mwili wa kwanza, alizingatia kuwa hataumba miili mingine
isipokuwa huo mwili anaouumba anaupa uwezo wa kutengeneza miili mingine. Mungu
akaweka mbegu ndani ya mwili wa mwanaume ili miili itengenezeke, kisha Mungu
akammega mwanaume na kumtengeneza mwanamke, na ndani ya mwanamke akaweka mayai yenye
uwezo wa kurutubisha mbegu za mwanaume ili kupata miili.
Siku mbegu na yai zikikutana, mwili mpya unaanza
kutengenezwa siku hiyo, na Mungu anamtuma mwanaye ambaye ni roho. Siku hiyo
mbinguni ni kama send-off, ila unakuta siku yako ilipofika mwili ulio tayari
upo kwa wazinzi kwenye baa; ndiyo unajikuta umezaliwa sehemu hiyo. Kuna waliotumwa
kwa kusudi fulani, wakanyofolewa na adui wakiwa tumboni na kufichwa kwenye mashimo;
wanasaidiwa na waliotumwa na Mungu kuwarudisha wote walionaswa kwenye mashimo ili
wakakamilishe kusudi lao (Isaya 42:22).
Kusudi lazima litimie, haijalishi umeshukia wapi;
muda ukifika wa kutimiza kusudi lako Mungu atakuongoza katika njia zake za kukutoa
mautini (Zaburi 68:20). Yapo mahesabu ya kimbingu ambayo yanajua
mahali fulani kuna hitaji fulani, na hivyo mbingu zimeweka kabisa muda na utimilifu
wake. Jambo lililopangwa ili jasusi litumwe, lazima litimie na halitimizwi na
aliyetumwa peke yake; Mungu hutuma majasusi wengine kushirikiana naye ili akamilishe.
Popote litakaposhushiwa jasusi siyo tatizo kwa maana Bwana atamuongoza katika
njia zake mpaka akutane na wenzake wenye nia moja.
Inatupasa tuchambuke; ukichambuka ukajijua na ukalijua
kusudi lako utalitenda. Paulo ni mfano wa kuchambuka; kuna wakati aliongea
yeye, na kuna wakati aliongea Bwana kupitia yeye (1 Wakorintho 7:12).
Kwenye kutekeleza jukumu haihitaji nguvu nyingi kwa
sababu kitu hicho kipo ndani yako. Anayeshuka kutoka mbinguni ni roho, ni mtu kabisa
(1 Wakorintho 15:47). Kama tulivyoona awali habari ya “mtu kwa
mavumbi ya ardhi” na “mtu nafsi hai”, biblia inatupa maana zaidi kuwa;
1.
“Mtu
wa kwanza” ndiyo huyo huyo “mtu kwa mavumbi ya ardhi” ambaye ni mwili, na
2.
“Mtu
wa pili” ndiye huyo huyo “mtu nafsi hai” ambaye ni roho.
Mtu wa kwanza ndiye alianza kuumbwa na alipokamilika
Mungu akamtoa mtu wa pili / akapuliza pumzi ya uhai kwa mtu wa kwanza. Mtu wa
kwanza na mtu wa pili wana miili kabisa na wote hula. Chakula cha mtu wa kwanza
kinafahamika, na chakula cha mtu wa pili pia. Mtu wa pili hula chakula cha roho
(1Wakorintho 10:4). Wekeza kwa mtu wa pili; mlishe sana kila
wakati ili amtawale na kumuongoza mtu wa kwanza, kinyume chake, ukimlisha sana
mtu wa kwanza utamdhoofisha mtu wa pili kwa kuwa nia ya mwili ni mauti (Warumi
8:6).
Mfano wa mtu wa kwanza na mtu wa pili ni gari na
dereva wa gari; mtu wa kwanza ni gari, na mtu wa pili ni dereva wa gari.
Biblia inafafanua tena kuwa kuna mwili wa asili na
mwili wa roho (1 Wakorintho 15:44). Mwili wa asili ni mtu wa
kwanza, na mwili wa roho ni mtu wa pili. Mfano wa uwepo wa mwili wa roho ni
Yesu alipokufa msalabani na roho yake kwenda mpaka kuzimu kuhubiri na kuchukua
funguo za kuzimu.
Mfano mwingine wa uwepo wa mwili wa roho ni wakati
wa ujenzi wa mnara wa Babeli; Mungu ni roho (Yohana 4:24) lakini
Mungu akiwa kwenye kikao cha mbinguni anasema washuke wakawachafulie usemi (Mwanzo
11:7). Popote walipo wa mwili wa asili, wa roho wanaweza wakafika tena
bila kuonekana; watakachokipanga kututenda, tunaouwezo wa kuwafuata kwenye
vikao vyao kwa namna ya miili ya roho na hawatuoni ila tupo.
Ibrahimu amekufa miaka mia tisa, badae Yesu akawepo
ulimwenguni na kusema alimwona Ibrahimu, jambo lililowashangaza Wayahudi (Yohana
8:57); Yesu alikuwako mbinguni kabla ya Ibrahimu, kwa maana Yesu
mwenyewe ndiye Mungu.
Ni desturi ya kushuka mtu, kuanza mwili wa asili
kwanza halafu unafuata mwili wa roho. Mariamu anapashwa habari kuwa atachukua
mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu na atamzaa mtoto jina lake Yesu; ilianza
mimba, akashuka Mungu mwenyewe. Wakati anashuka, Mamajusi wakamuona. Unaposhushwa
unaonekana na wenye macho ya rohoni, kwa hiyo adui anaweza akakuficha ili lile
kusudi lisitimie.
Wewe peke yako huwezi kuijua hatima yako; hata
waliokuzunguka hawajui. Mungu huweka watu wanaoijua hatima yako. Hata kama
wakufiche kwenye ganda la chuma ili usionekane, ganda litapasuka. Unatakiwa ukutane
tu na Samweli wako. Usiogope kuanguka kwa maana mwenye haki huanguka na kuinuka
tena; asiye haki / mwovu akianguka hainuki (Mithali 24:16, Mika
7:8, Warumi 7:19).


0 Comments