google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

MAADUI WA HATIMA

UFUFUO NA UZIMA CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 23.08.2026
ASKOFU DKT GERSHOM MWAKILA
SOMO: MAADUI WA HATIMA

Hatima ya mtu ndiyo maisha ya mtu. Maadui wa hatima ndiyo maadui wa maisha ya mtu. Hakuna mtu asiye na adui; maadui ni wengi sana. Silaha kubwa ya adui ni kufanya uadui wake kwa kutoonekana. Mfano, nchi hununua rada ili kuwaona maadui wanapowashambulia. Ukifanikiwa kumfahamu adui una uwezekano mkubwa wa kushinda vita hiyo, kwa maana imeandikwa katika 2 Wakorintho 2:11 kuwa, “Shetani asije akapata kutushinda; kwa maana hatukosi kuzijua fikira zake”. Adui hataki kujulikana.

Maisha ya mtu yanajulikana kabla hujazaliwa, hivyo adui anaweza akawahi kushambulia hatima ya mtu kupitia maeneo tofauti tofauti.

     I.        Kupitia jina la mtu: Jina la mtu limeungana na hatima ya mtu. Adui akitaka kukuwahi, anawahi kwenye jina lako. Kwa mtizamo wa Mungu, jina la mtu linabeba hatima ya mtu, ndiyo maana adui anaweza kukushambulia kwasababu ya jina lako ulilopewa. Baraka za mtu zinaenda na jina la mtu, na kwa Kadiri watu wanavyoliita jina la mtu ndivyo wanaita hatima yake “BWANA akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka;” Mwanzo 12:1-2.

Mungu alipotaka kumuita mtu amtumikie, alimbadilisha jina kwanza kwa maana, jina linabeba kusudi la mtu huyo. Katika kitabu cha Mwanzo 17:1-6, Mungu anafanya agano na Abramu kuwa baba wa mataifa mengi. Wakati Mungu akifanya agano hilo, Abramu na mkewe Sarai walikuwa wazee wa umri wa zaidi ya miaka tisini, na hawakuwa na mtoto, isipokuwa Abramu alikuwa na mtoto aitwaye Ishmaeli.

Mungu akambadilisha jina Abramu na kumuita Ibrahimu ili aendane na hatima; jina Ibrahimu lina uwezo wa kuwa baba wa mataifa mengi lakini Abramu halikuwa na uwezo huo. Jina linabadilishwa ili kubeba hatima ya ki Mungu. Jina likibadilika, hatima ya mtu inabadilika, afya ya mtu inabadilika na hali ya mtu inabadilika.

Mungu aliposema na Abramu na kumbadilisha jina kuwa Ibrahimu, akamgeukia mke wa Abramu, Sarai na kumbadilisha jina kuwa Sara ili awe mke wa Ibrahimu baba wa mataifa mengi, naye sara awe mama wa mataifa mengi.

Ndoa ya mtu ina uhusiano sana na hatima yake; mume anaweza akaathiri hatima ya mke, vivyo hivyo mke anaweza akaathiri hatima ya mume. Mmoja akiwa imara anaweza akafanikisha hatima ya mwenzake, na mmoja akiwa dhaifu anaweza akaiangusha hatima ya mwenzake.

Mungu akikupa jina, baraka za jina zinakuja na desturi zake ili ziendane na hatima. Sarai katika umri wa miaka tisini hakuwa na mtoto na alikoma desturi za mwanamke, lakini Sara anapewa baraka za kuwa mama wa mataifa mengi naye anapata mtoto (Isaka) ambaye Mungu anaahidi kuimarisha agano lake kupitia Isaka kuwa la milele.

Baraka za Mungu kwa Ibrahimu na Sara ni kuwa baba na mama wa mataifa mengi, lakini wao walipata mtoto mmoja aitwaye Isaka. Mbele za Mungu mtu ni nchi, ni taifa; hata Rebeka alivyopata mimba ya mapacha ambao walikuwa wakishindana tumboni, Mungu alimwambia kuwa ni mataifa mawili tumboni mwake yanafarakana “Watoto wakashindana tumboni mwake. Naye akasema, Ikiwa ni hivi, kuishi kwanifaa nini? Akaenda kumwuliza BWANA. BWANA akamwambia, Mataifa mawili yako tumboni mwako, Na kabila mbili za watu watafarakana tangu tumboni mwako. Kabila moja litakuwa hodari kuliko la pili, Na mkubwa atamtumikia mdogo.” Mwanzo 25:22-23. Katika kutimiza hatima, yapo matumbo huzaa Wafalme mbele za Mungu.

Ibrahimu alipokea baraka zake kwa umakini sana lakini wakati anaambiwa baraka za mkewe, akacheka. Hili linatufundisha kuwa, pokea baraka zako wewe mwenyewe na usisubiri kupokelewa na mwenza wako. Mungu hakuangalia yanayotoka mdomoni mwa Ibrahimu, ila yale yatokayo moyoni mwake Ibrahimu. Chochote uwazacho na kusema moyoni, kiwe sawa na vile Bwana anavyosema, na midomo iseme hayo. Alichowaza Ibrahimu na kusema kilikuwa tofauti na Mawazo ya Mungu (Mwanzo 17:17-19).

Imeandikwa katika Mithali 10:22 kuwa, “Baraka ya BWANA hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo.”. Mungu akisema anatimiza; yeye aliyeishi tasa ataitwa mama wa watoto na hakuna wasiwasi, nchi ya ukame itazaa matunda, kwa jina la Yesu! Kwa yote Mungu atakayosema, wewe mwamini tu ili uthibitike, na kwakuwa Mungu hutenda kazi zake kupitia watu wake, waamini manabii wa Mungu ili ufanikiwe “Wakaamka asubuhi na mapema, wakaenda nje katika jangwa la Tekoa; nao walipokuwa wakitoka, Yehoshafati akasimama, akasema, Nisikieni, enyi Yuda nanyi wenyeji wa Yerusalemu; mwaminini BWANA, Mungu wenu, ndivyo mtakavyothibitika; waaminini manabii wake, ndivyo mtakavyofanikiwa.” 2 Mambo ya Nyakati 20:20. Mambo ya Mungu ogopa kuyapima nae limu yakow ala sayansi. Neno la Bwana linakuja kwa wakati sahihi, na likija linakuja na majibu yote unayoyahitaji; neno likitoka halirudi bure.

Mungu siyo wa yeyote; hafanyi kazi na waliopo. Mungu hufanya kazi na aliowachagua kutimiza kusudi lake. Mfano, nabii Samweli kwenye familia ya Yese hakupaka mafuta Watoto waliokuwepo tena waliokuwa na sifa kimuonekano kwa sababu aliyechaguliwa na Mungu, Daudi, hakuwepo lakini alikuwa na neema ya kusubiriwa. Mungu humsubiri aliyemkusudia hata kama amefichwa mbali asionekane. Neema ya Mungu ya kusubiriwa na iwe kwetu kwa jina la Yesu, ili kule kwenye hatima zetu tusubiriwe.

Hatima ikiwepo, ipo tu. Daudi alivyoletwa kutoka nyuma ya jangwa, na nabii Samweli alivyomuona tu, akammiminia mafuta. Mungu siyo wa mbadala. Ibrahimu alimwambia Mungu kuhusu uwepo wa Ishmaeli lakini Mungu hakutaka aliyepo (Mwanzo 17:21). Hii inatufundisha kuwa tuombe kwa ajili ya kusudi la Mungu, vinginevyo tunaomba vibaya “Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu.” Yakobo 4:3.

Mungu aliweka kusudi kwa isaka ambaye hakuwepo wakati huo. Wakati Mungu anaweka agano na Ibrahimu, ni kama ilikuwa haiwezekani hivi lakini mwaka uliofuata majira yaleyale Sara na uzee wake, akamzaa Isaka. Mungu akufanyie muujiza wako ili mwakani majira kama haya uwe na ushuhuda mbele zake, kwa jina la Yesu!

Kuzaliwa kwa Yesu: Jina la Yesu lilitangulia kabla ya kuzaliwa kwake (Mathayo 1:18-21). Jina lake limeambatana na kusudi lake, yaani, mwokozi wa watu wake na dhambi zao. Alipoanza kuishi hatima yake, wapo waliojaribu kupotosha kusudi lake na kumuita mwenye pepo. Kwa kusudi lake Yesu, kila neno alilosema lilihusiana na kuokoa watu na dhambi zao, lakini walimuona mwenye pepo (Yohana 8:45-59). Yesu hakubadili kusudi lake; alishikilia msimamo wake ambao, maneno yote aliyosema yalihusu wokovu, yaani, kila amwaminiye hatakufa milele “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Yohana 3:16. Kwa kusudi la Yesu, inawapasa watu wake wamwamini tui li wawe na uzima wa milele (Yohana 17:3).

Kama ambavyo Yesu hakubadili hatima yake hata baada ya kukataliwa (Yohana 1:11-12), sisi pia hatubadili hatima; tukibezwa, watu wakiwa kinyume na sisi, hatubadili hatima, tunang’ang’ania hivyo hivyo kwa maana, “sisi siyo kama wale”. Tukikataliwa haibadilishi chochote; sisi ni wana wa Mungu tu. Popote tuendapo tunaeneza mila za mbinguni. Popote tulipo, sisi ni mfano wa Mungu hapa duniani; ukituona umemuona Mungu duniani, ukitusikia umemsikia Mungu duniani. Imeandikwa katika 1 Yohana 3:1 kuwa, “Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye.”.

Jina linabeba hatima. Jina la Yesu ni jina lililoambatana na ukombozi wa ulimwengu kutoka kwenye dhambi. Hatufi kwa sababu hamna magonjwa, ila ni kwasababu ya kuamini jina la Yesu. Hatima iliyobebwa na jina inaonekana katika kitabu cha Mwanzo 32:25-30 ambapo Yakobo anabadilishwa jina na kuitwa Israeli kumaanisha amemshinda Mungu na watu. Yakobo alishinda kwa sababu ya kanuni ya rohoni; ili roho ifanye kazi kwa ufanisi, lazima ivae mwili.

Kuzaliwa kwa Yohana: Lilitangulia jina la Yohana (Luka 1:8-13). Jina huambatana na hatima; hatima ya Yohana imeelezwa katika kitabu cha Luka 1:15-17. Jina likichengeshwa hatima inachengeshwa; watu walitaka kuchengesha hatima ya Yohana, hivyo wakataka kumpa jina tofauti, lakini Zakaria na Elizabethi walilijua kusudi la Mungu wakamuita mtoto wao Yohana (Luka 1:57-64). Ukichengesha jina la mtu umeharibu hatima ya mtu; usiwe mwepesi wa kukubali kupewa majina ambayo yanaweza kupindisha hatima yako.

Wapo watu hutoa majina kulingana na mazingira ya wakati wa kuzaa; mfano, shida, sikitu, chausiku, butiku, Mawazo, matatizo, ndivyo maana za majina hufuata maisha yao. Batilisha nguvu zote za adui nyuma ya jina ulilopewa, kwa jina la Yesu.

   II.        Watu kukusema kinyume na hatima yako: Unapoanza kuishi kusudi lako, jamii inajiinua kinyume na mwenendo wako ili ukate tamaa. Mfano umeitwa na Mungu kwa ajili ya kuhubiri neno lake, lakini kwa sababu ya watu kukuzungumzia vibaya kinyume na mwenendo na jitihada zako, maneno yale yanakudhoofisha na kukufanya uache kile ulichoitiwa na Mungu kumbe unaenda kinyume na hatima yako.

Kwenye biblia Mungu alimtuma Nehemia kuujenga ukuta wa Yerusalemu lakini wakaibuka watu wawili waliotaka kukwamisha, Sanbalati na Tobia (Neemia 4:1-3). Usiogope kughadhibiwa, watu kuingiwa uchungu, kudhihakiwa na kusemwa kinyume na unachokifanya ili uache kusudi lako la ki Mungu unalolifanya; piga moyo konde, maneno kama, “eti naye” yasikurudishe nyuma. Ukisikia hayo wewe amini tu kuwa unayaweza mambo yote katika yeye akutiaye nguvu (Wafilipi 4:13), na kwamba ufalme wa mbinguni unapatikana kwa nguvu, na ni wenye nguvu pekee wenye uwezo wa kuuteka, hivyo usisuse (Mathayo 11:12).

Kusemwa, hiyo no roho na ipo sehemu yoyote kwenye jambo lolote. Kwa kadiri unavyoendelea bila kukata tamaa, ndivyo unavyomtumikia Bwana; usiionee haya injili (Warumi 1:16). Usisubiri kupongezwa kwenye yale ufanyayo kwa maana utakumbana na roho ya Sanbalati na Tobia. Ukiacha kile Mungu anataka ufanye, utawajibika, na usipokuwa tayari kufanya upaswayo kuyafanya, utapigwa (Luka 12:47-48); asiwepo wa kumkatisha tamaa mwenzake.

Kokote ulikowekwa kufanya kazi ya Mungu, Fanya kwa uaminifu sana kwa sababu yeye aonaye sirini anakuona. Hekima ni kufanya kwa bidii sana bila kujali watu wanakuangaliaje.

 III.        Maadui wa hatima wakishindwa kukukatisha tamaa, watajitokeza waziwazi kushindana na wewe: Inawezakutokea kwa namna ya kukuletea ushauri, na usipofanya kama wanavyokushauri watashindana nawe “Lakini ikawa, Sanbalati, na Tobia, na Waarabu, na Waamoni, na Waashdodi, waliposikia ya kuwa kazi ya kuzitengeneza kuta za Yerusalemu inaendelea, na ya kuwa mahali palipobomoka panaanza kuzibwa, basi wakaghadhibika mno; wakafanya shauri wote pamoja kuja kupigana na Yerusalemu, na kufanya machafuko humo.” Nehemia 4:7-8.

Ukibaki katika kusudi la Mungu, hata wakishindana hawatakushinda. Hatuachi kumtumikia Mungu na Kutenda kusudi lake jema kwa maana maisha ya wokovu ni maisha ya kupigana vita; TUNAJENGA HUKU TUNAPIGANA VITA. Sisi ni kanisa la kupigana vita

 IV.        Wakijitokeza ukawashinda, watatuma mashetani: Mara nyingi watu hujiuliza kwanini wanalogwa. Kulogwa ni hatua ya mwisho kabisa. Wakituma mashetani wanadhamiria wakuongoze vibaya kwenye maamuzi yako ili uanguke.

Shetani akitumwa anakujia kukushawishi ufanye vile anavyotaka (1 mambo ya nyakati 21:1). Shetani anaweza akasimama juu ya familia yako, biashara yako, miradi yako au kusudi lako lolote akakushawishi ufanye kinyume.

Ni kanuni ya Mungu kuwa siku zote hutenda kazi kwa utashi wa mtu (Wafilipi 2:13). Shetani huingilia utashi huo ili mtu asifanye yale yampasayo kufanya. Vile utakavyoamua ndivyo utakavyomaliza hatima yako; vuzuri au vibaya, itategemea na utakavyoamua. Ukifanikiwa, utakuwa umeamua sawasawa, na kushindwa, utakuwa umeshawishiwa na shetani ukashawishika.

Kutumia akili ya shetani ni chukizo mbele za Mungu. Mawazo ya shetani yanasababisha kubadili tabia ya mtu. Angalia sana unachowaza kwa maana kile unachowaza, siku moja utakisema; na unachokisema, siku moja utakifanya. Mungu hakumuadhibu shetani kwa alichotenda ila kwa alichowaza.

Wakati mwingine mashetani wanatumwa kwako ili kuharibu tabia; tabia ikiharibika, hatima inaharibika. Unachokifanya mara kwa mara hugeuka kuwa tabia yako. Pepo humwingia mtu na kuleta tabia yoyote, mfano, uongo ni pepo (2 Mambo ya Nyakati 18:21), udhaifu ni pepo (Luka 13:11).

Habari njema ni kwamba, Yesu anao uwezo wa kuwafungua watu waliofungwa kwa tabia za kipepo kama alivyomfungua mwanamke aliyepindana kwa miaka kumi; msadiki tu Yesu, naye atakufungua (Isaya 53:1-5).

Unamshinda adui kwa kumkabidhi Yesu maisha yako. Maisha yetu yamegawanyika katika kambi mbili tofauti; 1) Kambi ya Yesu, 2) Kambi ya Shetani. Huwezi ukapigana vita ukiwa ndani ya kambi ya shetani, hivyo ni lazima utoke kwenye kambi ya shetani kwa kumpa Yesu maisha yako halafu tunaungana kuishambulia kambi ya shetani. Ukimpa Yesu maisha yako unakuwa umeokoka, na unakuwa na uwezo wa kutandika maadui wanaosimama kinyume na hatima yako.

Ukiokoka, maadui zako wanakuwa maadui wa Bwana.

BONYEZA HAPA KUANGALIA IBADA YA JUMAPILI

Post a Comment

0 Comments