google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

KESHO KUBWA ILIYONASA NDANI YA MTU

UFUFUO NA UZIMA CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 13.09.2026
ASKOFU DKT JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO: KESHO KUBWA ILIYONASA NDANI YA MTU

Hatima ya mtu haikuanza siku aliyozaliwa. Hatima ya mwanadamu haianzi siku anayotoka tumboni mwa mama yake. Mtu alikuwepo mbinguni kama roho kabla ya kuja duniani. Neno la Mungu linasema katika Yeremia 1:5, "Kabla sijakufanya katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa." Hii ina maana kwamba mtu alikuwepo mbinguni kama roho kabla hajaletwa hapa duniani.

Mfano: Pasipoti za wananchi wa Korea Kusini huandikwa umri wa mtu kwa kurudisha nyuma miezi tisa; Serikali yao inatambua kuwa mtu alikuwepo tangu mimba ilipotungwa. Tumbo la mama ni kama uwanja wa ndege tu ambapo roho inatua ikitokea mbinguni, na mwili ni ubia tu kati ya wazazi wa kimwili na Mungu aliyeitoa roho.

Mungu Yesu hakuanza siku alipozaliwa; alikuwepo mbinguni tangu mwanzo. Mungu aliumba mbingu na nchi kwa Neno lake, na badae Neno akavaa mwili, akaja duniani kwa njia ileile ya kuwa duniani, yaani akazaliwa (Yohana 1:1-14).

Hatuko duniani kwa bahati mbaya: Hakuna mtu aliyeko Dar es Salaam au Tanzania kwa ajali; Mungu alituleta kwa kusudi lake maalum. Mfano, Yohana 1:6 inasema wazi kuwa Yohana alitumwa kutoka kwa Mungu. Hii inatufundisha kuwa ukitumwa na Mungu, unazaliwa duniani; ukikamilisha kazi uliyotumwa, unarudi kwa aliyekutuma (Mhubiri 12:7).

Tunatoka mbinguni kuja duniani katika utimilifu wa wakati tu (Wagalatia 4:4) na hatufi mpaka tutimize jukumu lililotutoa mbinguni kama ilivyokuwa kwa mzee Simeoni ambaye hakufa mpaka alipombeba mtoto Yesu (Luka 2:26-35). Mwenye jukumu hupewa neema ya kutimiza jukumu hilo; hata hivyo kuna wakati kesho ya mtu inakuwa imenaswa ndani ya uhalisia wa kibinadamu ikisubiri neno la ki Mungu na mafuta ya kinabii ili iachiliwe.

Maana ya "kunasa" kwa kesho ya mtu: Mifano katika Mbegu ya Embe na Yai: Kokwa la embe kwa macho ya kawaida ni mbegu, lakini ndani yake "kumenasa" shina, matawi, majani, na magunia ya maembe yatakayovunwa kwa miaka mingi ijayo. Ule uwezo mkubwa umefungiwa ndani ya mbegu ndogo tu. Yai limebeba kuku lakini ni mpaka uwadie utimilifu wa wakati ili kuku huyo adhihirike.

Kwa mifano hiyo, tunang’amua kuwa uwezo wa mtu uko ndani yake; kile Mungu amepanga mtu awe, hakiko mbinguni bali Mungu ameshakiweka ndani ya mtu. Kila kitu kwa ajili ya upenyo wa mtu kiko ndani yake, ila kimenaswa ili mtu asiwe na kesho iliyoamuriwa na Mungu. Ni lazima tuinasue kesho iliyonaswa, kwa jina la Yesu!

Mifano ya “kesho iliyonasa” na ikanasuka kwa jina la Yesu:

Katika 1 Samueli 1:1-2, Biblia inamtambulisha mtu mmoja aitwaye Elkana mwana wa Yohamu, aliyekuwa na wake wawili, Hana (mke mkubwa) na Penina (mke mdogo). Imeandikwa, "… naye huyo Penina alikuwa na watoto, lakini Hana hakuwa na watoto."

Penina alikuwa anazaa watoto kwa wepesi sana, na alipata watoto saba. Lakini Hana, aliyependwa sana na mumewe, hakupata mtoto. Penina alimsimanga na kumdhalilisha Hana kila siku, kwa maneno makali kwa sababu Hana hakuwa anajua uchungu wa uzazi.

Biblia inasema katika 1 Samueli 1:5 kuwa Bwana alikuwa amefunga tumbo la Hana. Hapa tunajifunza kuwa sio kila kuzuiliwa ni laana. Tumbo la Hana lilishikiliwa na falme za giza zilizojua kuwa Hana akizaa, hatoi mtoto wa kawaida tofauti na Penina aliyekuwa anazaa watoto wa kawaida tu (quantity); Hana alibeba hatima nzito (quality). Ndani ya tumbo la Hana kulikuwa kumekwamia Nabii Samueli, na ndani ya Samueli kulikuwa na wafalme wa Israeli.

Hana alipozidiwa na huzuni ya kutopata mtoto, hakukimbilia kwa waganga; Hana alimimina roho yake mbele za Bwana, na Bwana, kupitia mtumishi wake, Eli, alimwambia Hana katika 1 Samueli 1:17 kuwa, "Enenda kwa Amani; na Mungu wa Israeli akujalie haja yako uliyomwomba." Biblia inasema katika 1 Samueli 1:20 kuwa wakati ulipowadia, Hana akachukua mimba, akamzaa mtoto mwanamume, akamwita jina lake Samueli.

Baada ya kumzaa Samueli, Hana alipata watoto wengine watano, lakini Biblia haiwazungumzii wala haitaji majina yao (1 Samueli 2:18-21). Mungu alimchagua Samueli pekee kutoka kwenye tumbo la Hana kwa ajili ya taifa la Israeli. Samueli akapa kibali kwa Bwana na kwa watu (1 Samueli 2:26). Hana akamtoa Samueli kwa Bwana.

Mungu alimuita Samueli akiwa bado mtoto mdogo. Ili Mungu anene na mtu, ni lazima mtu huyo aisikie sauti ya Bwana ikimuita na aitike. Baba wa kiroho wa Samueli alikuwa Eli, lakini Eli hakuwa akisikia sauti ya Bwana ila alijua namna ya kuitika na alimfundisha Samueli. Yatupasa kujua namna ya kuitika tutwapo na Mungu. Mungu alipomuita Samueli, Samueli aliitika kwa kusema, "Nena, Bwana, kwa kuwa mtumishi wako anasikia." (1 Samueli 3:10).

Baada ya kuitwa na Mungu akaitika, kuanzia hapo Samweli aliisikia sauti ya Mungu katika maisha yake yote. Mungu alimtumia kwa mambo mengi kwenye taifa la Israeli. Ukiitwa, ukaitika, Mungu anakutumia. Bwana aliwaokoa Wana wa Israeli kupitia maombi na sadaka ya Samueli, wakawashinda Wafilisti kwa radi na ngurumo zilizowasambaratisha (1 Samueli 7:10). Samueli alifanyika kiwanda cha kutengeneza wafalme wa Israeli; ndani yake kulikuwa na pembe ya mafuta iliyobeba kesho ya Sauli na Daudi.

Kuna wakati Mungu anaruhusu mtu apoteze vitu vyake ili amkutanishe na mtu wa hatima yake. Sauli, kijana wa kabila la Benjamini, alitumwa na baba yake kwenda kutafuta punda waliopotea. Akiwa amezunguka miji mingi bila kuwapata punda na akakata tamaa na kutaka kurudi nyumbani, mtumishi wake anamuongoza kukutana na muonaji mwenye kuheshimiwa ili amuonee punda waliopotea (1 Samueli 9:6).

Imeandikwa katika 1 Samueli 9:16 kuwa, "Kesho, wakati kama huu, nitakuletea mtu kutoka nchi ya Benyamini, nawe mtie mafuta ili awe mkuu juu ya watu wangu Israeli." Hapa tunajifunza kuwa Mungu ndiye aliwapoteza wale punda wasipatikane kwa siku tatu ili kumpeleka Sauli mbele ya Samueli. Mungu hutengeneza matukio ili mtu aifikie hatima yake. Siyo kila kupoteza unakemea shetani; kuna kupoteza ili uipate hatima. Mungu akikuita, anaruhusu Roho wake awe juu yako; Roho akikushukia unageuzwa na kuwa mtu mwingine kabisa. Sauli aligeuzwa akawa mpaka mnenaji. Asingepatikana Samueli, Sauli naye asingepatikana; hatima ya Sauli ilinasa tumboni mwa Hana.

Kukataliwa na Bwana haikuanza leo. Badae Sauli aliasi na Mungu akamkataa. Mungu akamtuma tena Samueli kwenye nyumba ya mzee Yese kumpaka mafuta Daudi. Imeandikwa katika 1 Samueli 16:1 kuwa, "Hata lini utamlilia Sauli, ikiwa mimi nimemkataa asiwamiliki Israeli? Ijaza pembe yako mafuta, uende, nami nitakupeleka kwa Yese, Mbethlehemi; maana nimejipatia mfalme katika wanawe."

Baada ya kukataliwa na Bwana, Sauli alijaribu namna nyingi kujinasua lakini hakuweza; aliendelea kumchukiza Bwana. Mungu akikukataa, ukijaribu kujiokoa unaharibu zaidi.

Katika familia ya mzee Yese, Daudi alikuwa anachunga kondoo, na familia yake haikuona ufalme ndani yake. Kesho ya Daudi kuwa mfalme ilikuwa imenasa ndani ya pembe ya mafuta aliyokuwa nayo Samueli. Kuna matukio mengi ya kidunia yanayoweza kumchelewesha mtu kuifikia hatima yake; hata ndugu ndani ya familia kuna mambo huchelewesha kwa kuangalia sura. Mungu huangalia moyo ili kumchagua amtakaye. Mungu alimchagua Daudi kwa kuangalia moyo. Mtu akichaguliwa na Bwana, husubiriwa atoke alikozuiliwa. Dharau na kufichwa hakuzuii hatima kutimia.

Nyuma ya mafanikio ya Daudi, yupo Goliati. Ili mtu afanikiwe, lazima apatikane Goliati wa maisha yake. Goliati ni daraja la mafanikio. Baada ya Daudi kupakwa mafuta kwa siri Bethlehemu, ilibidi atokee Goliati wa kitaifa ili mafuta ya Daudi yajulikane kitaifa / yadhihirike. Kuna matukio yanatengenezwa na Mungu siyo yakuue, ila yakufanikishe. Mungu akikubariki hakupi hela, anakupa Goliati; changamoto, vita, au dhiki anazopitia mtu leo hazijaja kumuua, zimekuja kujenga misuli yake ya kiroho na kumtambulisha kwenye hatima yake.

Daudi alimshinda Goliati na mafuta ya Samueli yakadhihirisha ushujaa wake. Pamoja na laana za Goliati kwa Daudi kwa miungu yake (Dagon), Daudi alimshinda Goliati kwa Jina la Bwana na kumkata kichwa kwa upanga wa Goliati mwenyewe. Fitina zilizopangwa na adui zako dhidi yako ndizo zitakuwa silaha zako dhidi ya adui zako; wageuzie uwashinde.

Vita kubwa unayopitia kwenye familia yako, biashara yako, au afya yako ni thibitisho kuwa kuna "Kesho Kubwa" imenasa ndani yako. Wewe ndiye uliyebeba ufunguo wa ukombozi wa ndugu zako.

Kama vile Eli alivyomwambia Hana, nami natamka: "Enenda kwa amani, na Mungu wa Israeli akupe haja ya moyo wako." Kila kilichonasa kikiwa cha kifedha, kibiashara, au kifamilia kianze kupenya sasa, kwa jina la Yesu!

Maombi na Baraka za baba Yetu kwetu:

Baba mtakatifu, Muumba wa mbingu na nchi, Mungu mkuu kuliko miungu yote ya Tanzania! Tazama mwanao ameinua mikono yake juu; Kesho yake kubwa imenaswa mahali; Kazi yake, biashara yake, afya yake imeshikiliwa; Kama vile maneno ya Eli Kuhani yalivyomkwamua Hana, nami natamka leo: Mwanangu, enenda kwa amani! Na Mungu wa Israeli akupe haja ya moyo wako!

Ninaamuru upenyo usiokuwa wa kawaida kwenye maisha yako kuanzia sasa! Ninamwagiza Sauli na majeshi ya giza yaliyojipanga kukuangamiza yasambaratike kwa jina la Yesu! Kila Goliati aliyesimama mbele ya hatima yako aanguke sasa hivi! Kila utendalo kuanzia leo lifanikiwa; kazi imefanikiwa, biashara imefanikiwa, ndoa imefanikiwa, na afya yako inarejea kwa jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu! Amina.

BONYEZA HAPA KUANGALIA IBADA YA JUMAPILI



Post a Comment

0 Comments