google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

MANENO YALIYOTAMKWA KINYUME NA HATIMA YAKO

UFUFUO NA UZIMA CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 16.08.2026
ASKOFU DKT GERSHOM MWAKILA
SOMO: MANENO YALIYOTAMKWA KINYUME NA HATIMA YAKO

Hakuna kitu kibaya kama maneno na hakuna kitu kizuri kama maneno. Kuna mambo mengi sana yameharibiwa na maneno, na hatima nyingi zimeharibiwa na maneno. Maneno huondoa kuaminika kwa mtu na mtu mwingine. Watu wengi maisha yao yameharibika kwa sababu ya maneno waliyotamkiwa kinyume cha hatima zao.

Mungu katika uumbaji wake aliumba kwa neno, na kila neno alilotamka lilikuwa vilevile na halisia. Imeandikwa katika Waebrania 11:3 kuwa, “Kwa imani twafahamu ya kuwa ulimwengu uliumbwa kwa neno la Mungu, hata vitu vinavyoonekana havikufanywa kwa vitu vilivyo dhahiri.”.

Kila kitu kinachoonekana ni zao la neno alilotamka Mungu, Nyota, milima vyote ni matokeo ya neno la Mungu. Katika kitabu cha Mwanzo 1:1-3 tunaona Mungu “akasema” ikawa. Mungu kabla hajafanya jambo lolote, anasema kwanza. Hata kanisani, makuhani wa Mungu hutanguliza kusema neno kwanza na baada ya hapo maombezi hufuata. Haiwezekani watu waje kanisani alafu moja kwa moja waanze kuomba bila kusikia neno kwanza, kwa sababu kanuni ya Mungu ni neno la Mungu kwanza ili watu wafunuliwe kwanza. Neno la Mungu ni msingi wa kila kitu.

Mambo hutokea sawasawa na neno lililotamkwa. Roho Mtakatifu huangalia kila neno la Mungu lililosemwa ili alithibitishe. Hitaji la mtu kwa ajili ya biashara hutanguliwa na neno la Mungu juu ya biashara; linaanza neno la Mungu badae ufumbuzi wa hitaji la mtu linapatikana. Mungu akisema, kitu cha ki Mungu kinatokea; wachawi wakitamka neno, matokeo ya kichawi yanatokea pia. Mwanzo wa kila kitu ni neno, na vyote vinafanyika kwa neno (Yohana 1:1).

Kanuni ya Mungu iko vilevile hata sasa; pasipo neno la Mungu hakuna uponyaji; linatangulia neno la kuponya kabla ya uponyaji. Ndani ya neno kuna uzima tele ambao ni nuru ing’aayo gizani. Giza haliishindi nuru ya neno la Bwana. Likitokea neno, giza linapotea. Usikimbize giza bali peleka neno la Bwana nalo Giza litakimbia lenyewe; mfano, giza kwenye ndoa, giza kwenye biashara, giza kwenye ajira, giza kwenye hatima. Roho Mtakatifu husimamia neno lililotoka, alitimize.

Baada ya mwanzo kuwako neno, badae neno liligeuka likawa mtu. Imeandikwa katika Yohana 1:14 kuwa, “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli.”.

Neno lolote likivaa mwili likawa mtu, watu wanaona matokeo / matunda. Hakuna neno linalotoka hewani bali kila neno linatoka kwa mtu. Mfano, ukitamka maneno ya kutishia kuua, hayakamatwi maneno ila anakamatwa mtu; maneno hayatenganishwi na mtu. Ukisema maneno yanayozuia hatima, maana yake ni mtu anazuia hatima yake mwenyewe au ya mtu mwingine, ndiyo maana ukisikia “neno la Bwana likamjia nabii Yeremia, kusema…” maana yake ni Mungu mwenyewe anashuka kutusaidia kwenye tabu zetu (Yeremia 37:6). Likitamkwa neno la uponyaji maana yake ni mtu Yesu anakuja kuponya hitaji la mtu.

Kama neno lilimjia Yeremia, Amosi na wengine, linaweza kutujia hata sisi, na linapotujia, ni Yesu anatutembelea kwenye biashara zetu, kwenye uponyaji; anatutembelea na kutupa yale tunayoyahitaji.

Neno ni mtu “naye neno akavaa mwili, akakaa kwetu, na sisi tukauona utukufu wake”. Neno akikaa mahali, utukufu wake unaonekana, na watu wote wanauona. Kwa jina la Yesu, neno akae kwenye biashara zetu, kanisani, kwenye maisha yetu, na watu wote wauone utukufu wake maana neno la Bwana linasema hivyo (Ufunuo 19:13).

Siku zote unaposikia neno maana yake unayemsikia ni mtu. Ukisoma kwenye kitabu cha Yohana 6:63, imeandikwa kuwa “Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima.” Tunapata tafsiri kuwa neno ni roho, na tunafahamu kuwa mtu ni roho. Kama mtu ni roho, na neno ni roho, hivyo, tafsiri ya wanamahesabu iko wazi kuwa neno ni mtu; mtu siyo mwili.

Kwakuwa mtu ni roho, imeandikwa katika Ezekieli 2:2 kuwa, “Naye aliposema nami, roho ikaniingia, ikanisimamisha; nikamsikia yeye aliyesema nami.”. Kila mtu anaposema na wewe kuna roho inakuingia. Ukitakia kuchagua roho ipi ikuingie, chagua wa kuongea naye; siyo kila mtu ni wa kumpa sikio lako. Kuna watu ukiongea nao, maneno yao yanakusimamisha, na kuna watu ukiongea nao, maneno yao yakakufanya uanguke.

Ukitaka kushinda baadhi ya vita, chagua watu wa kuwasikiliza. Ukichagua wa kumsikiliza, umechagua roho ya kukuingia. Kuna roho inakuingia na kukutia hofu, kukukatisha tamaa, inazuia hatima, inakurudisha nyuma na kwa ujumla inakuangusha. Sikiliza watu ambao roho ikikuingia unaiendea biashara, ndoa, unapata ujasiri na siyo hofu. Chagua wa kukupa ushauri, maana kuna mtu kwa kadiri anavyokushauri ndivyo anakutia hofu. Usikubali kushauriwa na mtu aliyeshindwa; kama alishindwa yeye, haimaanishi wewe pia utashindwa. Kama alishindwa, basi ana roho ya kushindwa; ukimsikiliza, roho ya kushindwa itakuingia.

Sisi tunaamini kushinda kwenye kila kitu, kwa maana imeandikwa katika Warumi 8:37 kuwa, “Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda.”.

Tunafanya yale ambayo baba yetu amekuwa akitusihi na kutufundisha ili kufikia hatima zetu. Tatizo watu ni wagumu kuamini katika neno na kuiendea hatima. Kuna watu labda tutumie kanuni za fizikia (Isack Newton’s law of motion) kwenye maisha yao kupata nguvu ya kuwasukuma ili waendee hatima zao. Ukisukumwa, sukumika; kwa jina la Yesu, neno la Bwana likusukume uende kwenye njia ambayo Bwana ameshakuandalia. Kwa njia ya neno ulizuiwa, basi leo kwa njia ya neno uachiliwe uende.

Imeandikwa katika Marko 16:17-18 kuwa, “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.”

 

Neno la Mungu hutangulia halafu matokeo / matunda hutokea. Katika kitabu cha Marko, Yesu ametanguliza neno lake. Kila neno lililosemwa linabeba ishara zinazofuatana nalo; neno la biashara linafuatana na ishara za biashara, neno la ajira linafuatana na ishara za ajira, neno la uponyaji linafuatana na ishara za uponyaji.

Kuna roho nyuma ya maneno, kuna mtu nyuma ya maneno kwa sababu neno ni roho na mtu ni roho. Kuna mtu anaharibikiwa sababu ya maneno yake mwenyewe. Imeandikwa katika kitabu cha Yakobo 3:2 kuwa, “Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”. Vitu vyote vinavyomsumbua mtu ni sababu ya mdomo wake. Imeandikwa pia katika kitabu cha 1 Petro 1:10 kuwa, “Katika habari ya wokovu huo manabii walitafuta-tafuta na kuchunguza-chunguza, ambao walitabiri habari za neema itakayowafikia ninyi.”. Ukitaka kutoboa maisha, siku zako ziwe njema, ufurahie maisha yako ya ndoa, kazini, zuia ulimi wako usiseme mabaya kinyume na neno la Bwana; kamdomo katakuponza.

Imeandikwa katika kitabu cha Mithali 18:21 kuwa, “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake”. Ukitaka matunda ya uzima, sema kuhusu uzima; ukitaka matunda ya ajali, sema kuhusu ajali; ukitaka matunda ya mauti, sema kuhusu mauti.

Imeandikwa katika kitabu cha Zaburi 118:18 kuwa, “BWANA ameniadhibu sana, Lakini hakuniacha nife”. Sababu ya kutokufa ipo; biashara yangu haitakufa, ndoa yangu haitakufa, hatima yangu haitakufa … ILI NIYASIMULIE MATENDO YA BWANA, kwa maana Mtetezi wetu yu hai (Ayubu 19:25).

Neno linaweza likageuza maisha ya mtu. Watu wabaya wakijua unaelekea kupenya kwenye hatima yako, wanatuma neno lakutaka kwenda kinyume na hatima yako. Mfano; mfalme Dario alitaka kumpa nafasi ya juu katika ufalme wake mtumishi wa Mungu Danieli, taarifa zikasambaa kwenda kwa watu na hao watu wakaenda kutoa ushauri kwa mfalme lengo lao kubwa ni kutaka kuzua kupenya kwa Danieli. Walishawishi mpaka kuweka sheria kali, na wakati wa kupitisha sheria Danieli hakuwepo.

Neno moja hubadili kabisa moyo wa mtu kumwamini mtu; mfano, maneno kama “angalia sana mkeo / mumeo” yanaweza kuvuruga ndoa iliyo na amani. Kuna neno limesababisha mtu aachishwe kazi isivyo sawa.

Neno la laana kwa Reubeni lilibadilisha Reubeni kuwa mzaliwa wa kwanza wa Yakobo, na nguvu ya neno iliathiri mpaka vinasaba vya Reubeni kwa Yakobo (1 Mambo ya Nyakati 5:1).

Maneno aliyotamkiwa mtu ni lazima ipatikane nguvu / mamlaka ya rohoni ya kuyatangua. Maneno na laana kwa Reubeni yalikuja kutanguliwa na Musa; uzao wa Reubeni ukaonekana tena kwa wana wa Israeli (Kumbukumbu la Torati 33:1-6, Ufunuo 7:1-5). Kadhalika, neno la laana juu ya mtu atakayeijenga Yeriko lililotolewa na Yoshua, badae lilitanguliwa na Elisha.

Kuna uchawi wa kuzuia watu kwa maneno; imeandikwa katika kitabu cha Ufunuo 2:14 kuwa, “Lakini ninayo maneno machache juu yako, kwa kuwa unao huko watu washikao mafundisho ya Balaamu, yeye aliyemfundisha Balaki atie ukwazo mbele ya Waisraeli, kwamba wavile vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini.”.

Maneno, “mafundisho ya Balaamu” ni mafundisho ya kuzuia watu wasipenye / wasiende kwenye hatima. Ni mafundisho ya kutia ukwazo. Yapo mafundisho ya kuondoa ukwazo / kuondoa vizuizi. Sisi tumefundishwa na baba yetu mafundisho haya; jinsi ya kuhubiri, kuwafungua watu na kuondoa vizuizi. Tunayazuia mafundisho ya Balaamu yasifanye kazi kwenye maisha ya watu. Kama analaani bila aibu, tunakanusha / tunatangua bila aibu; wanalaani kwa mdomo, tunatangua kwa mdomo.

BONYEZA HAPA KUANGALIA IBADA YA JUMAPILI


Post a Comment

0 Comments