UFUFUO NA UZIMA
CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI
06.09.2026
ASKOFU DKT GERSHOM
MWAKILA
SOMO: ADUI WA NJIA
YA HATIMA
Yesu ndiye Njia Kuu. Kulingana na Yohana 14:4-6 na Matendo 4:12, Yesu ndiye njia pekee ya kufika kwa Baba; njia
nyingine zote za wanadamu kuelekea kwa Mungu zimefungwa. Siyo kila njia ni sahihi kwa kila
mtu. Njia iliyo sahihi kwa mtu mmoja inaweza kuwa anguko la mwingine. Mfano:
Bahari ya Shamu ilikuwa njia ya wokovu kwa Wana wa Israeli, lakini ikawa njia
ya mauti na maangamizi kwa majeshi ya Farao.
Kwakuwa njia ni mtu na adui wa njia ni mtu, kuna
maadui na mitego ya njiani:
Kuna njia ya majuto kwa mtu
kuielekea hatima yake. Njia hii hutokea kwa namna ambayo watu wanakuja kama wajumbe wa
ibilisi wenye sura njema, lakini mwisho wao huacha majuto kwenye kazi, ndoa,
biashara au jambo jema la mtu. Muombe Mungu akufunulie kujua kama njia ni
salama kwa maana imeandikwa katika Zaburi 139:24
kuwa, “Ukaone kama iko njia ya ubaya ndani yangu, Ukaniongoze katika njia ya
milele”.
"Kwa
jina la Yesu, mtu yeyote aliyebeba majuto aende mbali na asikaribie biashara
zangu, kazi zangu, ndoa yangu, na miradi yangu. Ninamkatilia mbali kwa jina la
Yesu!"
Mungu na Shetani Kupitia Watu: Mungu hufungua mambo kupitia
mkono wa mtu mwenye nia ya Mungu, na Shetani huharibu, kuloga, au kuleta
magonjwa kupitia mtu mwenye nia ya uharibifu. Imeandikwa katika Warumi
8:28 kuwa, “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na
wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake.”.
Kwahiyo, ukikutana na mtu aliyebeba nia ya Mungu, kimsingi umekutana na Mungu
katika sura ya mtu, kwa maana Mungu hapendi kuwahuzunisha watu wake (Maombolezo
3:33). Hata hivyo, mara nyingi adui hutoka miongoni mwa watu wa
nyumbani (Mika
7:6).
Kwa mantiki hii, mambo ya mtu hufunguliwa na
kubarikiwa kwa mkono wa mtu, na mambo ya mtu uharibiwa na kufungwa kwa mkono wa
mtu. Ukitaka kusafisha njia yako, anza na wale wanaokuzunguka. Njia za kuingia
mautini ni mtu, na njia za kutoka mautini ni mtu pia. Ni imani yetu kuwa njia
za kutoka mautini zina Yehova; Bwana amezinyoosha na hajamkabidhi mtu kwa maana
anazo mwenyewe.
Sisi tulio na Kristo tunaimani thabiti kuwa mauti
siyo mwisho. Tunayo imani ya kuziendea njia za kutoka mautini. Kupitia Roho
Mtakatifu aliyemfufua Yesu, ndoa iliyokufa, biashara iliyokufa, miradi
iliyokufa, vyote vinahuishwa na kufufuka. Ile roho iliyomtoa Yesu Kristo katika
wafu kwa kuhuisha roho yake, ipo kuhuisha roho zetu. Roho hiyo inakaa ndani
yetu kama ilivyoandikwa katika Warumi 8:11 kuwa, “Lakini
ikiwa Roho wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye
aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali
ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu.” Roho ya kuhuisha
ikimuingia mtu, inamtoa kwenye mauti ya kila kilichokufa kwenye maisha yake.
"Ikiwa
Roho aliyemfufua Kristo kutoka kwa wafu anakaa ndani yangu, ninamuru mwili
wangu ulio katika hali ya kufa uhuishwe! Ninatangaza uzima kwenye figo zangu,
seli zangu, na ubongo wangu. Ninaamuru biashara yangu iliyokuwa inakufa iamke
tena, ndoa yangu iishi tena, na miradi yangu isimame tena, kwa jina la Yesu
Kristo!"
Roho ya Amaleki (Unyonge
na Uchovu): Amaleki
anawakilisha adui anayevizia pale mwanadamu anapochoka au kuonyesha unyonge (Kumbukumbu la Torati 25:17-18). Ukielekea
kwenye njia uliyopewa na Bwana, adui huibuka kwenye njia yako ili akuzuie. Adui
akiona umechoka, anaibuka ili akumalize. Adui huyu hachapi kiongozi wa mbele,
anapiga walio nyuma (wanyonge). Epuka kumuonesha adui yako kuwa umechoka;
ulimwengu wa roho hautaki unyonge; kataa maneno kama "nimechoka" au "sisi
wanyonge"
kwani unyonge huvutia mapigo ya adui badala ya huruma kwa maana imeandikwa
katika Ufunuo 21:27 kuwa “Na ndani yake hakitaingia kamwe chochote
kilicho kinyonge, wala yeye afanyaye machafuko na uongo, bali wale walioandikwa
katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo.”
Mungu anasema, yeye aliye dhaifu na aseme “mimi ni
hodari (Yoeli 3:10). Ni kanuni ya rohoni kuwa, hata kama umechoka sema
“nina nguvu” (Mithali 8:14, 18:21). Sema kinyume na udhaifu wako; Mungu
atakutendea sawasawa na neno la kinywa chako (Zaburi 118:17). Adui wa
njiani anavizia udhaifu wa mtu ili amuangamize (Ezra 8:31); batilisha
maneno yote uliyojinenea udhaifu, kwa damu ya Yesu inenayo mema. Kuna watu
wakiwa dhaifu hutia huruma, lakini wana wa Mungu hawapeani pole ila hutiana
moyo kwa maneno ya Mungu yanayohuisha nguvu.
"Kwa jina la Yesu, ninafuta kila ukiri wa kinyume
niliowahi kuutamka kwa kinywa changu. Ninakataa lugha ya unyonge na uchovu.
Hata kama nilikuwa dhaifu, ninasema mimi ni hodari na nina nguvu! Nguvu ya
Amaleki ya kunivizia kwenye uchovu wangu ninaitengulia sasa hivi, kwa jina la
Yesu!"
Walinzi Wakali na Fomula za Kifamilia: Mamlaka za
giza huweka walinzi wakali ili kuzuia na kuchepusha njia ya ustawi (Mathayo 8:28). Mtu aviziaye / anyemeleaye, haji waziwazi; Mungu
humzuia yeye aviziaye. Elisha alimuokoa mfalme wa Israeli mara nyingi
alipoviziwa na adui njiani. Adui hutengeneza fomula ya kumfunga mtu na
kumuangusha kupitia vizazi hata vizazi. Mfano, kuwa na magonjwa ya kufanana,
vifo vya kufanana na ukomo wa umri unaofanana. Adui awekapo fomula hiyo, njia
za kuelekea mafanikio hulindwa sana na mamlaka za rohoni ili mtu asiendee wala
asione. Zipo dalili zinazoashiria mtu analindwa sana, mfano ni kuwa na wasiwasi
wa kuanza jambo kama biashara.
Kuelekea nchi ya Wagerasi, Yesu alipita kwa sababu
njia zina yeye. Sisi tunamtanguliza Yesu; akipita na sisi tunapita. Vaa nia ya
kupita kwenye njia; achia Upanga wa roho kuwafyeka walinzi wote wa njiani
waondoke kwenye njia.
"Ninatoa upanga wa Roho kinyume na walinzi wote
wakali waliokaa kwenye njia ya ustawi wangu, ndoa yangu, na promotion yangu.
Ninawafyeka wote kwa jina la Yesu! Ninabatilisha kila mtego wa hasara,
umaskini, kifo, au ajali uliotegwa njiani mwangu. Mitego hiyo ninairudisha kwa
adui, wazame wao kwenye mashimo waliyochimba kwa jina la Yesu!"
Kufichwa, Kuzuiliwa, na Kupindishwa kwa Njia:
Njia ya mtu inaweza kufichwa (Isaya 40:27). Njia ni
mtu; mtu akifichwa usionane naye, huwezi ukafika kule unatakiwa uende.
Njia inaweza ikazuiliwa (Warumi 1:13). Njia ni mtu;
mtu anaweza akazuiliwa na mtu / watu wenye nia ya shetani. Mtume Paulo
alijaribu mara nyingi kwenda Rumi kueneza injili lakini shetani akawa akizuia
asiende. Kuzuiliwa kwa Paulo ni kuzuia hatima ya Warumi wengi ambao Paulo, kwa
neno la Mungu, angewasaidia kufikia hatima zao.
Njia
ya mtu inaweza ikapindishwa; Mungu anapoandaa hatima, anaandaa na namna ya mtu
kuifikia hatima hiyo. Mafanikio ya mtu yapo kwenye hatima yake. Walimwengu
huingilia njia ya mtu kuelekea mafanikio. Mtu hujikuta anapambana sana lakini
hafiki kwa sababu ya hao walimwengu.
Njia
za Mungu zimenyooka sana lakini wachawi, wenye kujaa hila, wana wa uovu wote,
adui wa haki yote, wana wa Ibilisi na manabii wa uongo huzipindisha, na matokeo
yake mtu hupambana sana kujishughulisha na hafikii mafanikio (Matendo ya
mitume 13:6-10). Kama wapindishaji wasingekuwepo, mafanikio
yangepatikana bila kupambana kwa maana njia za Bwana zimenyooka.


0 Comments