UFUFUO NA UZIMA
CATHEDRAL
IBADA YA JUMAPILI 09.08.2026
ASKOFU DKT GERSHOM
MWAKILA
SOMO: WAPELELEZI
WA HATIMA
Hatima ya mtu ndiyo maisha ya mtu. Wapelelezi siyo
jambo geni kulisikia na ni jambo zuri; hata kwenye biblia Mungu hutambua
wapelelezi. Taarifa kutoka kwa wapelelezi juu ya upelelezi waliofanya ni jambo
la kuzingatia sana. Nchi zina wapelelezi, taasisi pia. Zamani za wazee wetu,
mtu akitaka kuoa walitumwa wapelelezi ili kujua siri fulani muhimu za ukoo na
familia husika; mfano, ikiwa ukoo una ukoma au kama ukoo ni wa hovyo. Upelelezi
unatumika kwenye mambo mengi ili kufanya maamuzi sahihi.
Kimsingi kwenye taasisi kuna wapelelezi wa aina
tano; -
1. Wapelelezi wakazi wa eneo (Local spies):
Hawa ni wenyeji wa eneo ambao hutoa taarifa muhimu bila kujua kama
wanapelelezwa. Hutangulia kwa kusifiwa (wanajazwa) halafu wanalewa sifa na
kuanza kutoa siri.
2. Wapelelezi wa ndani (Inward spies):
Hawa ni wapelelezi ndani ya taasisi husika inayopelelezwa; ni waajiriwa. Kwa kadiri
wanavyofanya kazi ndiyo wanavyopeleleza. Kwa mfano, hata hapa kanisani
yawezekana kabisa wapo na wamejiunga kwenye madarasa ya baba au Glory Choir, au
Wana wa Asafu na wanahudumu kabisa, lakini wanapeleleza mambo ya hapa kanisani
na kupeleka kwa waliowatuma.
3. Wapelelezi Wajinga (Doomed spies):
Hawa ni wapelelezi wasio na maarifa ambao mara nyingi hugundulika na kupewa
taarifa za uongo.
4. Wapelelezi walioongoka (Converted
Spies): Hawa ni wapelelezi waliotumwa kupeleleza eneo Fulani lakini wenyeji wa
eneo hilo ama wakawatendea wema au wakawashawishi mpaka wakaanza kutoa siri za
waliowatuma.
5. Wapelelezi waliofanikiwa /
walionusurika (Surviving Spies): Hawa ni wapelelezi waliofanikiwa kupata
taarifa na kuzipeleka zinakohitajika / kwa waliowatuma.
Upelelezi upo kila mahali hata kwenye biblia
umeelezwa. Katika biblia, kwa mfano, Mungu anamwambia Musa apeleke watu wakaipeleleze
nchi ya Kanaani (Hesabu 13:1-3). Hapa tunaona kuwa upelelezi halikuwa
wazo la Musa ila ni wazo la Mungu anayeijua hiyo nchi na kuwajua wenyeji wake.
Musa akakusanya vichwa kumi na mbili kutoka katika
kabila kumi na mbili za wana wa Israeli, ambao walienda kuipeleleza Kanaani na
kuleta taarifa kwa Musa. Kuna wakati taarifa ya upelelezi inaweza ikakukatisha
tamaa; taarifa ya upelelezi wa Kanaani ilitolewa kwa jamii yote ya wana wa
Israeli bila siri, na ile ya wale kumi isipokuwa Kalebu na Yoshua iliwahuzunisha
sana maana iliwavunja moyo. Taarifa ya upelelezi iliyowatia moyo ni ile ya Kalebu
na Yoshua ambayo iliwapa nguvu wana wa Israeli kuwa Mungu ameyeyusha mioyo ya
Wakanaani na kuwa wanaweza kushinda vita; walitoa taarifa ya ushawishi wa mioyo
yao, hata walipotaka kudhuriwa Bwana aliwaokoa.
Tunajifunza kuwa, Bwana haangalii wingi wa watu ili
aokoe; yeye ni Mungu wa mmoja aliye kwenye njia ya kweli. Mungu hushuka na
kusimama pamoja na mtu aliye kwenye njia ya kweli dhidi ya maadui zake. Hasira ya
Bwana iliwaka dhidi ya taarifa ya wale wapelelezi wapotoshaji. Siku zote
angalia taarifa ya Bwana; usiangalie ni hali gani utakayoambana nayo, kama
ilivyoandikwa katika Matendo ya Mitume 27:25 kuwa, “Basi,
wanaume, changamkeni; kwa sababu namwamini Mungu, ya kwamba yatakuwa vile vile
kama nilivyoambiwa.”. Mungu akikwambia nenda, wewe nenda kwa maana yeye
ndiye muasisi wa upelelezi. Mungu akikusemesha juu ya jambo moja, nenda
kalipeleleze kwanza.
Upelelezi pia unaonekana katika kitabu cha Yoshua
2:1-3, ya kuwa, Yoshua alituma wapelelezi wawili, kwa siri, kuipeleleza
Yeriko. Wenyeji wa nchi wakatoa taarifa kwa mfalme juu ya wapelelezi walioingia.
Mfalme akatuma askari wake kuwakamata, lakini Rahabu aliyekuwa akawaficha wapelelezi
wa Bwana wakawa salama, na yeye akawa salama. Nchi ikipelelezwa ikapelelezeka,
imekwisha; mambo ya mtu yakipelelezwa yakapelelezeka, amekwisha. Adui hashambulii
bila kupeleleza kwanza.
Mambo ya upelelezi hayakuanza na sisi; yapo kwenye biblia.
Adui hutumia taarifa ya upelelezi kumshambulia mtu; adui haji mpaka awe na
taarifa. Mfano, pale Bustani ya Edeni, nyoka alipeleleza kwanza ili kuwaangusha
Adamu na Eva. Hatima ya Adamu na Eva ilikuwa ni Bustani ya Edeni. Kabla hatima
ya mtu haijaharibika, ilipelelezwa kwanza. Yakupasa uanze kushughulika na
mpelelezi anayepeleleza maisha yako kabla hajapata taarifa zako.
Nyoka alikuwa mwerevu kuliko Wanyama wote (Mwanzo
3:1-3). Maneno ya nyoka, “Ati!” ni njama ya kutafuta taarifa. Mpelelezi ana
akili ya upelelezi; haji akikwambia nimekuja kukupeleleza. Kuwa mwerevu;
usimfafanulie jambo mpelelezi. Eva alimfafanulia nyoka nahiyo ikawa ni kosa
kubwa lililomfanya nyoka ajue ulipo mtego. Mtego wa shetani ni kumtamanisha mtu
kufanya alichokatazwa kukifanya. Ni rahisi sana kufanya ulichokatazwa kwa
sababu utataka kujua kwanini umekatazwa. Kosa walilolifanya Adamu na Eva
likawaondoa kwenye hatima yao.
Adui hutumia taarifa unazotoa kukudhuru; ukifanikiwa
kuficha taarifa zako, umeshinda.mfano, ukiambiwa, “mbona siku hizi unang’aa
sana”, waambie tu “damu ya mwana kondoo inatung’arisha", au ukiambiwa
“mbona una furaha sana siku hizi” wewe sema tu “Furaha ya Bwana ndiyo nguvu
zangu”. Yafiche mambo yako dhidi ya wapelelezi.
Baada ya mpelelezi (nyoka) kuwapeleleza nao (Adamu
na Eva) wakapelelezeka, shida zikaanzia hapo; mavazi awali hayakuwa tatizo,
yakawa tatizo; Wanyama hawakuwa na tatizo na wanadamu, ghafla wakawa maadui
n.k.
Wapelelezi huja kwa sura ya kuvutia; Neno la
Bwana litawafichua wote kwa jina la Yesu Kristo! kwa moto wa roho
mtakatifu tunawapima na kuwaweka wazi wapelelezi wa mambo yetu wajulikane maana
kwa neno la bwana wanachambuka na hakuna wa kutoroka. Imeandikwa katika Waebrania
4:12 kuwa, “Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena
lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya
nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi
kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.”
Kwa jina la Yesu, mpelelezi
yeyote aliyekuja kupeleleza mambo ya miradi yangu, kwa jina la Yesu siku ya leo
hautanitoroka, kwa jina la Yesu!
Wapelelezi wa nchi hupeleleza ili nchi ikae sawa. Je,
anayepeleleza mambo ya mtu, imani ya mtu, ndoa, nini lengo lake?
Imeandikwa katika Wagalatia 2:4-5
kuwa, “Bali kwa ajili ya ndugu za uongo walioingizwa kwa siri; ambao
waliingia kwa siri ili kuupeleleza uhuru wetu tulio nao katika Kristo Yesu, ili
watutie utumwani; ambao hata saa moja hatukujitia chini yao, ili kwamba kweli
ya Injili ikae pamoja nanyi.”. Kwa
neno hili, ni dhahiri ya kuwa wapelelezi wa mambo binafsi ya mtu wanalenga
kumtia mtu utumwani. Utumwa ni jambo lolote baya kwenye maisha ya mtu;
magonjwa, umasikini, hofu n.k.
Kila mtu ana hatima yake katika Kristo, na wote tuna
furaha katika Kristo. Adui hapendi tuwe na furaha katika Kristo; anakuja ili
aturudishe kwenye utumwa, kwenye vifungo, kwenye matatizo, kwenye msongo wa mawazo.
Tunampinga adui kwa maana Imeandikwa katika Warumi 8:15 kuwa, “Kwa
kuwa hamkupokea tena roho wa utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya
kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, Aba, yaani, Baba.”.
Bwana ametuagiza tufurahi katika Bwana kama
ilivyoandikwa katika Wafilipi 4:4 kuwa, “Furahini katika
Bwana sikuzote; tena nasema, Furahini.”. Sisi siyo watumwa katika jina la Yesu;
tunaikataa hofu.
Adui akikukosa kwenye kukupeleleza utaiona hasira
yake. Kwa jina la Yesu, ninakosekana kwenye mawindo wa adui zangu!
Hatima ya Yesu Ilichorwa na kusudi lake liliandikwa
kabla ya kuzaliwa kwake. Wakati wa kuzaliwa, wachawi kutoka Mashariki ya mbali
walifika kwa Herode kutaka kumuona mtoto Yesu wamsujudie. Herode anafadhaika na
kuwapeleleza mamajusi na kupata taarifa kuwa mtoto kazaliwa yapata miaka miwili.
Herode anawatuma mamajusi kupeleleza sana habari za mtoto Yesu, na wakimuona wampee
taarifa ili naye aende kumsujudia (huu ni mtego). Mamajusi hawakumpa taarifa
Herode; Herode hakumpata mtoto Yesu.
Adui hutuma wapelelezi kwenye maisha ya mtu ili
aharibu. Adui hushambulia kulingana na taarifa alizopata. Silaha kubwa ni
kulinda taarifa. Kuna wakati mtu anashambuliwa na kuharibiwa mambo yake kwa
sababu ya kuongea sana / kutoa siri zake hovyo kwa watu wasiofaa. Hata kwenye
kutoa ushuhuda mtu anahitaji maarifa, kwa maana ushuhuda hukaribisha vita. Zuia
kamdomo; adui anakushambulia kwa sababu ya mdomo wako. Zuia ulimi wako (1
Petro 3:10).
Herode alivyokosa taarifa za mtoto Yesu akapitisha
upanga kwa Watoto ili kumuua mtoto Yesu, ila hakufanikiwa (Yeremia 31:15,
Mathayo 2:18).
Warumi 13:2
Kisa hiki kinamzungumzia Manoa mwenye mke tasa,
asiyezaa. Neno “lakini” lilivyotumika linamaanisha, mbingu zinajua ni tasa,
mbingu zinajua ni masikini, mbingu zinajua umelogwa, mbingu zinajua huwezi,
lakini inabatilisha yote na kumaanisha, ni tasa lakini atachukua mimba. Lakini ni
ya mbinguni. Bila kujali sababu za kibaiolojia alizonazo mke wa Manoa, lakini
ya mbinguni kutoka kwa mjumbe wa Bwana inaleta tofauti kwa kufuta sababu zote.
Kisa hiki ndicho kilimleta duniani Samsoni. Kuzaliwa
Samsoni kutoka kwa mama tasa ni mpango wa Mungu kuwashinda Wafilisti. Visa vya
Samsoni kuwashambulia Wafilisti ilikuwa ni wanawake. Katika kuwapiga Wafilisti chanzo
kwa Samsoni ilikuwa kila mwanamke aliyempata (Waamuzi 14, 15,
16).
Badae wakuu wa Wafilisti wakaona Samsoni amewashinda
sana hivyo wakatafuta udhaifu wake ili kumkabili kupitia huo. Wafilisti
wakataka kujua asili ya nguvu za Samsoni na ili kujua hilo, wakagundua Samsoni
ana udhaifu wa wanawake hivyo wanaweza kujua kupitia mwanamke. Wafilisti wakamtuma
Delila kumpeleleza Samsoni. Adui hulenga desturi ya mtu kile akipendacho ili
akitumie kumfunga. Adui anakupeleleza ili akufunge uwe mtumwa akutese.
Kiasili wanadamu hatuko sawa; watu wote hatuko sawa.
Samsoni mwenye vishungi vya nywele na mnadhiri wa Bwana hakuwa sawa na wanadamu
wenzake. Tunavaa kama wao, tunakula kama wao ila hatuko kama wao.
Mpelelezi wa maisha yako kuna wakati anahusika moja
kwa moja kwenye kifungo chako na mateso yako. Delila alimpeleleza Samsoni ili
amfunge ateswe, nyuma ya Delila kuna jeshi la Wafilisti wanaomuotea Samsoni. Usimuone
mtu ukamdharau vile anavyoonekana; hujui nyuma yake kuna nini kilichopo dhidi
yako. Mfano, nyuma ya Yesu kuna majeshi kumi na mbili ya Malaika ambayo
angeweza kutoa amri yawashambulie watesi wake.
Delila alimpeleleza Samsoni, siyo siku moja tu;
ilikuwa mara kwa mara, na Samsoni alijitahidi kumficha ukweli. Ukiona mtu
anauliza jambo lile lile mara kwa mara na hakati tamaa, kaa mbali naye, na uwe
makini na machozi ya anayelia mbele yako.
Samsoni alipelelezwa akapelelezeka, akapofushwa na
akawa mtumwa wa Wafilisti. Samsoni akawa mtu wa kawaida. Adui humtesa mtu wa kawaida.
Hata hivyo badae nywele zilimuota Samsoni na kuwa siyo mtu wa kawaida tena. Tafsiri
ya nywele kuota ni kurudi kwenye njia ya Mungu / kwenye mapenzi ya Mungu.
Nywele zikiota ni wakati wa kulipiza kisasi. Bwana anatutumia
sisi kulipa kisasi kwa maana yeye hutenda kazi ndani yetu. Imeandikwa katika Warumi
8:28 kuwa, “…” Kwenye “mambo yote” kisasi kinapatikana, hivyo dhana ya
kuwa kisasi ni juu ya Mungu mwenyewe inakosa msingi. Kwenye “mambo yote”
utamuona Mungu kwa sura ya mtu. Mungu hufanya kazi na wale wampendao; ukimpenda
Mungu anafanya kazi na wewe. Kisasi cha Bwana kipo juu ya wote waletao utumwa
kwenye maisha ya watu.

0 Comments