google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

HAIKUWA HIVYO TANGU ZAMANI


IBADA YA JUMAPILI YA TAREHE 12/10/2014

MCHUNGAJI JOSEPHAT GWAJIMA

SOMO: HAIKUWA HIVYO TANGU ZAMANI

Utangulizi
Mchungaji kiongozi Josephat Gwajima

 Kanisa leo limefanywa kuwa mahali pa kukutania baada ya uchovu wa wiki nzima. Lakini haikuwa hivyo tangu zamani; kanisa lilianzishwa kama mahali pa kutatua matatizo yaliyoshindikana ndani ya wiki nzima.
“Kwa maana viumbe vyote pia vinatazamia kwa shauku nyingi kufunuliwa kwa wana wa Mungu.
Kwa maana viumbe vyote pia vilitiishwa chini ya ubatili; si kwa hiari yake, ila kwa sababu yake yeye aliyevitiisha katika tumaini;
Kwa kuwa viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.
Kwa maana twajua ya kuwa viumbe vyote  pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.” Warumi 8:19-22

Kumbe kuna viumbe ambavyo vimebebeshwa utumwa wa aina fulani ambavyo vinategemea kuwekwa huru.
Ulimwengu tunaouendea utakuwa ni ulimwengu ambao sio wa kushinda kwa sababu ndugu yako ni mbunge, waziri ama raisi, bali utakuwa ni ulimwengu wa kushinda mambo yote kwa imani. Tunakiendea kizazi ambacho mwenye haki ataishi kwa imani.

“Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” Mwanzo1:28
Haya ni mamlaka ambayo Mungu alimpa mwanadamu zamani sana kabla nyumba hazijajengwa, kabla  mavazi hayajaanza kutengenezwa. Kwanza ni kuzaa na kuongezeka iwe mwilini au rohoni. Pili ni kutiisha kila kitu kwenye nchi; mapori, majangwa, milima. Tatu, kutawala kila kitu angani, baharini na nchi kavu. Hivi ndivyo ilivyokuwa tangu mwanzo, asili yetu kama wana wa Mungu ni kutawala sio kutawaliwa. Lakini leo wana wa Mungu wamekuwa watu wakuogopaogopa; sivyo ilivyokuwa. Tuliumbwa kutiisha na kutawala angani, baharini na kwenye nchi.
Mungu ni Mungu wa kusema. Kabla hajatenda huwa anaongea kwanza. Ndio maana biblia nzima imejaa ahadi za Mungu, anasema atatubariki, atatuinua. Hivyo inatupasa  na sisi kuongea na kuikiri asili yetu. Tunatawala kwa mujibu wa sheria ya kitabu cha Mwanzo ibara ya kwanza kifungu cha ishirini na nane. Biblia ni sheria ya Bwana wa Majeshi na sheria hii haiwezi kubadilika kizazi hata kizazi.

Kwa asili ya mwanadamu alitakiwa atawale majini, angani na katika nchi. Shetani alipoona mwanadamu amepewa mamlaka hiyo akamfuata Adamu ili aibe mamlaka hiyo. Kwa kuwa sisi nasi tulikuwa katika viuno vya Adamu wakati anatenda dhambi iliyomgharimu mamlaka yake tumehesabiwa dhambi kutoka kwake..
“Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu;
Ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi;

Ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tama za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili nay a nia, tukawa kwa tabi yetu watoto wa hasira kama na hao wengine” Waefeso 2:1-3
Ndio maana leo shetani anaitwa mkuu wa anga. Kabla ya Adamu na Eva hawajatenda dhambi walikuwa wanatiisha anga, nchi na bahari. Walipokosea walipoteza mamlaka yao ambayo ilichukuliwa na shetani. Shetani aliichukua anga na kuitawala ndio maana akaitwa mfalme wa anga.
“Nao wakamshinda kwa damu ya mwanakondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hwakupenda maisha yao hata kufa.
Kwa hiyo shangilieni enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wan chi na bahari! Kwa maana yule ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache.” Ufunuo12:11-2
Adamu alikuwa anamiliki anga, bahari na nchi. Shetani alipofanikiwa kumtoa Adam, akafanikiwa kumiliki vyote alivyokuwa anamiliki. Ndio maana sasa kuzimu ina sehemu kuu tatu; angani, baharini na kwenye nchi.
Kama wana wa Mungu ambao tunatakiwa kuishi kwa imani ili kumpendeza Mungu;  kutamka, kusema na kukiri ahadi za Mungu kabla hazijawa bayana katika ulimwengu wa mwili ni sehemu ya maisha yetu. Tamka kwa bidii yaliyomo ndani ya moyo wako kwa maana uweza wa uzima na mauti u ndani ya kinywa chako. Hii ndiyo imani itupasayo kuishi kwayo. Imani ina viwango vinne;

Ø Unachowaza
Awazavyo mtu moyoni mwake ndivyo alivyo. Ni muhimu kujua namna ya kuyatiisha mawazo yako ili yawe sawasawa na namna ambavyo Mungu anawaza kuhusu wewe.

Ø Unachosema
Chochote uwazacho baada ya muda fulani utakikiri kwa kuwa hii ndiyo asili yetu kutoka kwa Mungu; kusema kabla jambo halijatokea.

Ø Unachotenda
  Ukishawaza na kukiri ni lazima uanze kutenda kuelekea kwenye lile jambo ambalo unaloliamini.

Ø Tendo la Imani
Hili ni tendo ambalo unatenda ambalo huwa ni kinyume na hali halisi ya mambo katika ulimwengu wa mwili.
Pasipo Imani haiwezekani kumpendeza Mungu. Mungu ni Mungu wa makusudi, hivyo lazima ufahamu kusudi lako katika maisha. Maendeleo hayaji kwa kuota utakuwa unatembea ukaokota mamilioni ya fedha halafu ukafanikiwa, mafanikio yoyote huja kwa hatua za kuhifadhi kidogokidogo kile ulicho nacho. Pale ambapo kusudi lisipofahamika matumizi mabaya lazima yatokee.

Hivyo shetani alipomtoa Adamu kwenye utawala akakaa yeye kuwa mtawala wa anga, nchi, bahari na vyote vilivyomo. Kabla Adamu hajatenda dhambi, akiwa bado ni mtawala; sisi tulikuwa ndani ya viuno vyake hivyo tulionja utawala huo. Baada ya shetani kuuchukua utawala kutoka kwetu, ana uwezo wa kuvitiisha viumbe vyote baharini, angani na kwenye nchi. Anayo mamlaka ya kuamuru viumbe kama bacteria, virusi , protozoa kuingia ndani ya miili ya wanadamu na kusababisha magonjwa au hata mauti. Leo dunia ina kila aina ya magonjwa na nyuma ya kila ugonjwa kuna kiumbe. Lakini viumbe hivi vimetiishwa kwa ubatili na yule aibaye ambaye ameiba mamlaka yetu. Haikuwa hivyo tangu zamani.
Mwanzoni Adamu hakuwa na magonjwa kabisa kwasababu alikuwa anatawala anga na viumbe vyake vyote, nchi na viumbe vyake vyote bahari na viumbe vyake vyote. Hivyo viumbe vyote vilikuwa chini ya utiisho wake. Hii ndiyo asili ya mwanzo ya mwanadamu.
Kwa nini leo kila janga kubwa linatokea Afrika? Vita vya kikabila, siasa mbovu, umaskini uliopitiliza, magonjwa ya ajabu; ukimwi unaua sana Afrika, ebola, mafua ya ndege, mafua ya nguruwe, dengue. Ni nini kinatokea? Shetani hawapendi waafrika kwa sababu anajua kutokea kwao ndipo utakapotokea ule uamsho wa siku za mwisho utakaogeuza tawala zote kuwa tawala za mwanakondoo. Imani bado ipo Afrika.
Tangu mwanzo shetani amekuwa akiona dalili za Afrika kuwa jeshi la mwisho la Mungu ndio maana anainua vita juu yake. Wana wa Israeli waliishi Afrika kwa miaka mia nne na thelathini utumwani Misri, miujiza mingi ilitokea Afrika  kule Misri. Haitoshi  alipozaliwa Yesu, malaika alimtokea Yusufu akamwambia amchukue Mariamu mkewe na mtoto Yesu na kuwapeleka katika nchi ya Misri. Wakati wa kubeba msalaba, ilipofika hatua  Yesu hawezi kuubeba tena alitokea Simon mkrene (Krene ni Afrika mahali panapoitwa Libya leo.) akaubeba msalaba mpaka Kalvari. Hii ni kuonyesha kuwa injili ya siku za mwisho itabebwa na waafrika. Ndio maana biblia inasema kutakuwepo na madhabahu katika nchi ya Afrika ( Isaya 19:4) 4 Nami nitawatoa hao Wamisri na kuwatia katika mikono ya bwana mgumu; na mfalme mkali atawatawala; asema Bwana, Bwana wa majeshi.
Yesu alivyokuja duniani alikuja kuturudishia utawala wetu ulioibiwa na shetani. Basi kumbe leo shetani anatawala isivyo halali, sisi ndio watawala halali. Tunayo mamlaka ya kuvitiisha viumbe vyote viletavyo magonjwa  kukaa nje ya mipaka ya Tanzania kwa jina la Yesu na vikatii.
Ebola ni mpango wa kuzimu, ni hukumu ya kifo kwa waafrika ili kuipunguza nguvu yetu. Na sisi kama watawala leo tumegundua asili yetu na hila ya yule alaye. Hivyo inatupasa kuchukua hatua kama watawala kutiisha, kumiliki na kutawala.
 
 
Maelfu ya watu wakiomba ndani ya bonde la kukata maneno

MAOMBI.
Ninaamuru kama mtawala wa bakteria, virusi na viumbe vyote wa magonjwa hamna uwezo juu yangu kwa jina la Yesu. Hamna mamlaka juu ya Tanzania. Ninawatiisha viumbe wote wanaoonekana na wasioonekana wasababishao magonjwa kwa jina la Yesu, hamtaingia ndani ya Tanzania kwa jina la Yesu. Kwa mamlaka niliyonayo ninawafunga virusi wote wa mafua ya ndege, virusi wa mafua ya nguruwe, ebola  nje ya Tanzania kwa damu ya Yesu. Kemikali zote, bakteria, protozoa wote ninawatiisha kwa damu ya Yesu Kristo. Kwa mamlaka ya damu ya mwanakondoo, viumbe wote wa magonjwa ninaupiga ule uweza uliowekwa ndani yenu juu ya Tanzania, juu ya Afrika, juu ya maisha yangu, juu ya familia yangu; ninaamuru kuanzia sasa  hamtaingia ndani ya nchi ya Tanzania kwa jina la Yesu.Ninavimiliki na kuvitiisha viumbe vyote vinavyokaa kwenye anga, bahari, na nchi. Mimi ni mtawala wenu, hamna mamlaka ya kunitawala  haikuwa hivyo tangu zamani. Ninawaseta mrudi kuzimu mlikotoka kwa jina la Yesu. Ninaamuru kuanzia sasa hamtanidhuru kwa damu ya Yesu. Viumbe vyote vinavyoonekana na visivyoonekana hamna uwezo wa kunitawala kwa jina la Yesu Kristo. Ninabeba mamlaka kama mtawala, ninawateketeza na uwezo wenu wa kudhuru kwa damu ya mwanakondoo. Nimepewa amri juu ya pepo wachafu na viumbe vyote, ninaangamiza kila nguvu iliyo juu yenu ninyi viumbe wa kishetani na kichawi na waganga wa kienyeji, ninawakausha kwa damu ya Yesu Kristo. Niwaondolea ule uwezo wa kuidhuru Tanzania kwa mamlaka ya damu ya mwanakondoo. Ninaiachilia damu ya mwanakondoo kwenye mipaka yote ya Tanzania,  damu inenayo  mema, ninainyunyizia kwenye mipaka yote ya Taifa la Tanzania na juu ya watu wake wote. Iwalinde dhidi ya magonjwa yote kwa jina la Yesu. Kwa mamlaka ya Jina la Yesu kristo ninatawala viumbe vvyote  vilivyomo baharini,  angani na kwenye nchi kwa damu ya Yesu. Ninatawala uchumi wa nchi, utajiri wa nchi; ninautawala kwa jina la Yesu Kristo. Ninatawala kwa jina la Yesu Kristo, ninatawala na kuvitiisha viumbe vyote vya magonjwa kwa jina la Yesu Kristo. AMEN!
 







 

Post a Comment

0 Comments