JUMAPILI
YA TAREHE 26_10_2014
MCHUNGAJI
JOSEH JONES
NA MCHUNGAJI KIONGOZI JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO:
NGUVU YA IMANI
Mchungaji kiongozi Josephati Gwajima akiwa na Mchungaji Joseph Jones |
Kama raia wa Tanzania
unahitaji upate fedha ya Tanzania ambayo ni shilingi ili uweze kuishi ndani ya
nchi hii. Utaihitaji kupanda daladala, kununua chakula na kugharamia maisha kwa ujumla. Lakini wewe kama
mtu aliyeokoka ni zaidi ya raia wa Tanzania, wewe ni raia wa mbinguni. Kama
ilivyo kwa nchi ya Tanzania, raia wa mbinguni pia wana fedha ambayo ni imani.
Biblia inasema mwenye haki wangu ataishi kwa imani. Hatuwezi kumpendeza Mungu
wala kuingia katika ufalme wa Mungu bila imani.
“Kwa maana mmeokolewa
kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa
cha Mungu;” Waefeso 2:8
“Basi imani ni kuwa
na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana. Lakini
pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima
aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”
Waebrania11:1
Kama unataka
kumpendeza Mungu lazima uishi kwa imani; ndani ya maisha ya imani kuna
uponyaji, wokovu, amani, nguvu. Pasipo imani huwezi kamwe kupokea baraka hizi.
Lakini imani huendana na uvumilivu.
“Kwa maana haki ya
Mungu inadhihirishwa ndani yake, toka imani hata imani; kama ilivyoandikwa,
Mwenye haki ataishi kwa imani.” Warumi1:17
Imani inakuja kwa
kusikia neno la Mungu, hiyo ndiyo njia pekee unayoweza kupokea imani. Unahitaji
kusoma neno la Mungu, kulitafakari na zaidi kulitenda ndipo upokee imani. Kama
ambavyo leo ungeenda kwenye ATM ya benki
mojawapo ya Tanzania kuchukua fedha; nenda kwenye ATM ya Mungu ambayo ni biblia
ukachukue imani. Neno la Mungu ni mbegu; Yesu alitoa mfano huu wa mpanzi:
“Akawaambia, Hamjui
mfano huu? Basi mifano yote mtaitambuaje? Mpanzi huyo hulipanda neno. Hawa ndio walio kando
ya njia lipandwapo neno; nao, wakiisha kusikia, mara huja Shetani, akaliondoa
lile neno lililopandwa mioyoni mwao. Kadhalika na hawa ndio wapandwao penye
miamba, ambao kwamba wakiisha kulisikia lile neno, mara hulipokea kwa furaha; ila hawana mizizi
ndani yao, bali hudumu muda mchache; kisha ikitokea dhiki au udhia kwa ajili ya
lile neno, mara hujikwaa. Na hawa ndio wale wapandwao penye
miiba; ni watu walisikiao lile neno, na shughuli za dunia, na udanganyifu wa
mali, na tamaa za mambo mengine zikiingia, hulisonga lile neno, likawa halizai.
Na hawa ndio
waliopandwa penye udongo ulio mzuri; ni watu walisikiao lile neno na kulipokea,
na kuzaa matunda, mmoja thelathini, mmoja sitini, na mmoja mia. Akawaambia, Mwaonaje?
Taa huja ili kuwekwa chini ya pishi, au mvunguni? Si kuwekwa juu ya kiango? Kwa
maana hakuna neno lililositirika, ila makusudi lije likadhihirika; wala hakuna
lililofichwa, ila makusudi lije likatokea wazi. Mtu akiwa na masikio ya kusikilia, na
asikie.” Marko4: 13
Neno la Mungu ni mbegu
ambayo siku zote hutenda kazi. Tunalipanda neno la Bwana ndani ya mioyo yetu. Baada
ya muda mbegu hii hukua ndani ya mioyo yetu na kuzaa matunda. Je, ni nani
aliyepanda viazi akavuna mahindi? Hayupo. Vivyo hivyo basi mtu akitaka kuishi
maishi ya imani lazima apande mbegu ya imani ambayo ni neno la Mungu.
Tunaposoma neno la
Mungu au kusikiliza mahubiri hiyo ni mbegu inakuwa inapandwa. Baada ya kusikia
mara kwa mara kwa muda fulani mti wa imani huanza kukua. Ili kuyaona matunda ya
mti wa imani inatupasa kuwa wavumilivu.
“Kwa hiyo wekeeni
mbali uchafu wote na ubaya uzidio, na kupokea kwa upole neno lile lililopandwa
ndani, liwezalo kuziokoa roho zenu. Lakini iweni
watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. Kwa sababu mtu akiwa
ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia
uso wake katika kioo. Maana
hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo.” Yakobo1:21
Kukombolewa kwetu
kunatokana na lile neno tunalolipokea. Kazi yetu sisi ni kulisikia neno,
kulitafakari na kulitenda. Kazi ya Mungu ambaye ndiye mpanzi ni kulikuza hilo
neno ili lizae matunda..
“Lakini yanenaje?
Lile neno li karibu nawe, katika kinywa chako, na katika moyo wako; yaani, ni
lile neno la imani tulihubirilo. Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa
chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika
wafu, utaokoka. Kwa
maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata
wokovu.” Warumi10: 8
Imani ni kuamini kwa
mioyo yetu na kukiri kwa midomo yetu. Unapookoka watakuwepo watu watakaokueleza
habari mbalimbali za wokovu wakati kanisa nalo linajitahidi kukufundisha habari
za wokovu. Wote hawa wanajaribu kupanda mbegu ndani yako. Utakachokiamini ndani
ya moyo wako na kukiri kwa midomo yako hicho kitakuwa.
Imani yaweza
kuelezewa kwa mfano wa ujauzito. Ili mama awe mjamzito ni lazima iwepo mbegu
ambayo inapandwa ndani ya tumbo lake. Hawezi kuamka tu siku moja akajikuta ana
tumbo kubwa. Wakati wa ujauzito zipo adha mbalimbali ambazo mama huyu
atazipitia. Hata muda wa kujifungua unapowadia mama huyu hujua kuwa muda wake
umefika bila hata kuambiwa. Zile dakika chache kabla ya kujifungua kwake huwa
ni za mateso na maumivu makali sana lakini hufuatiwa na furaha isiyoelezeka
baada ya mama huyu kumuona mwanaye kwa mara ya kwanza. Ndivyo ilivyo imani;
lazima neno lipandwe, na hakika zitakuwepo adha nyingi utakazopitia wakati wa
ujauzito wako wa imani. Na kabla tu imani yako haijazaa matunda kutakuwa
uchungu ambao hufuatiwa na ule muujiza ambao ndilo tunda la imani yako. Beba
ujauzito wa imani leo kwa jina la Yesu.
Mtu anaweza kuwa
anajidanganya kuwa ana imani kwa kukiri maneno ya ukombozi. Lakini kama unatamka
maneno hewa bila kuwa na neno ulilopanda ndani ya moyo wao huwezi kuwa na imani
wala huwezi kuzaa matunda ya imani. Biblia inaiita imani ya namna hii imani
iliyokufa. Kama wewe ni mgonjwa na unang’ang’ana kusema nimepona, nimepona bila kuwa na neno la
kusimamia hakika imani yako imekufa.
Unatakiwa kusema , “Imeandikwa kwa kupigwa kwale mimi nimepona, nimepona
kansa kwa jina la Yesu.” Kama unataka ulinzi unasema, “Mabaya hayatanipata mimi
wala tauni haitakaribia hemani mwangu, hakuna uchawi juu ya Yakobo wala uganga
juu ya Israeli.” Imani ya namna hii hakika itazaa kwa wakati wake. Biblia
inasema ukiwa na imani ndani yako chochote utakachokisema utakipata sawa sawa na imani yako kama usemavyo.
Inawezekana unasema
mimi ninaamini lakini siwezi kukisema ninachokiamini kwa sababu kama kisipotokea
nitachekwa. Watu wengi huwa na mtazamo huu. Lakini kama huu ni muamala basi
bila kutamka kile ulichopanda ndani ya moyo wako muamala huu haujakamilika. Ni
lazima usikie neno ili lipandwe ndani yako halafu ukiri kile unachokiamini.
Baada ya kupanda
mbegu ya imani upo muda wa kusubiri ili mbegu hii iweze kumea, kukua na kisha
kuzaa matunda. Hakuna mkulima apandaye mahindi leo na kutegemea kuvuna kesho;
wala hakuna mama atungaye mimba leo akitegemea mtoto kesho. Ipo miezi tisa ya
kusubiri mimba kugeuka mtoto. Watu wengi hukata tamaa wanapokosa kuona matunda
ya imani yao mapema. Ili uweze kuzaa unahitaji kuwa mvumilivu kusubiri imani
yako izae.
0 Comments