google.com, pub-4324601895065941, DIRECT, f08c47fec0942fa0

Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

UHAMISHO WA KIROHO



JUMAPILI YA TAREHE 21 – 12 – 2014
MCHUNGAJI KIONGOZI JOSEPHAT GWAJIMA
SOMO: UHAMISHO WA KIROHO
 Basi vizazi vyote tangu Ibrahimu hata Daudi ni vizazi kumi na vinne; na tangu Daudi hata ule uhamisho wa Babeli ni vizazi kumi na vinne; na tangu ule uhamisho wa Babeli hata Kristo ni vizazi kumi na vinne.” Mathayo 1:17
“Yekonia alikuwa na umri wa miaka kumi na minane alipoanza kutawala; akatawala miezi mitatu katika Yerusalemu; na jina la mama yake aliitwa Nehushta binti Elnathani wa Yerusalemu. Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, mfano wa yote aliyoyafanya baba yake. Wakati ule watumishi wa
 
 Nebukadreza mfalme wa Babeli wakakwea kwenda Yerusalemu, na mji ukahusuriwa. Na Nebukadreza, mfalme wa Babeli, akaufikilia huo mji, hapo watumishi wake walipokuwa wakiuhusuru. Na Yekonia, mfalme wa Yuda, akatoka akamwendea mfalme wa Babeli, yeye na mama yake, na watumishi wake, na wakuu wa watu wake, na maakida wake; mfalme wa Babeli akamchukua mateka katika mwaka wa nane wa kutawala kwake. Akatoa huko hazina zote za nyumba ya Bwana, na hazina za nyumba ya mfalme, akavikata-kata vyombo vyote vya dhahabu ambavyo Sulemani, mfalme wa Israeli, alivifanya katika hekalu la Bwana, kama Bwana alivyosema. Akawachukua mateka watu wa Yerusalemu wote pia, na wakuu wote, na mashujaa wote, watu elfu kumi; na mafundi wote, na wafua chuma wote; hapana mtu aliyebaki, ila waliokuwa wanyonge wa watu wa nchi.” 2Wafalme 24:8 – 14
Mfalme wa Israel wakati ule alikuwa anaitwa Yekonia na alitawala miezi mitatu na kumtenda Mungu dhambi, naye Mungu akaruhusu mfalme wa Babeli aende kwa mfalme wa Israeli na kuitawala Israel. Kumbe katika utawala, mtawala haihitaji muda mrefu sana ili kuharibu mambo; vivyo hivyo kwenye wokovu, mtu haihiitaji kuwa kwenye wokovu muda mrefu ili amkosoe Mungu. Tunaona Mfalme Yekonia alitawala miezi mitatu tu na kisha kumtenda Mungu dhambi. Pia tunaona Mungu alipoziona dhambi za Yekonia akaliachia taifa adui la Babeli kulivamia taifa la Israel. Unapokuwa dhambini Mungu ataruhusu adui zako wakupige na hakika watakushinda. Hakuna ushindi katika dhambi. Na Mfalme Yekonia alilitambua vema jambo hili.
Kwa kutambua hilo, Yekonia akaamua kujisalimisha kwa mfalme Nebukadreza yeye pamoja na mama yake, baraza lake la mawaziri, maakida pamoja na watu wengine muhimu katika nchi wakiwemo matajiri wote. Pia, mfalme Nebukadreza alichukua vitu vya thamani kutoka katika hekalu la Bwana ikiwa ni pamoja na sanduku la agano. Akachukua majeshi, mafundi, wenye akili wote na wafua chuma ili wakaujenge ufalme wa Babeli.
Mfalme Yekonia alijisalimisha kwa kuwa alijua atashindwa vita kwa sababu ya hali yake mbaya kiroho, yaani dhambi. Imeandikwa,
“Mpenzi naomba ufanikiwe katika mambo yote na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo.” 3 Yohana 1:2
 
Hali yako ya kiroho ikiwa imefanikiwa, “ukiwa hauna dhambi” mambo mengine ya mwilini yatafanikiwa vivyo hivyo. Mfalme wa Babeli hapa ni alama ya shetani. Shetani huwa ana kawaida ya kuwachukua wale watu wenye akili, uwezo na nguvu popote aingiapo na kuondoka nao. Yawezekana ni katika nchi au hata familia. Hujawahi kusikia msibani watu wakisema, “ni heri angekufa fulani na si huyu.” Kuna msemo kuwa watu wazuri huwa hawadumu. Kwa nini? Shetani anajua kuwa watu wa namna hii ni hatari kwa ufalme wake ndio maana anajitahidi kuwafanya mateka mapema wawe misukule au wadhaifu kwa namna ambayo hawatakuwa tishio kwake tena.
Imeandikwa,
Kabla sijakuumba katika tumbo nalikujua, na kabla hujatoka tumboni, nalikutakasa; nimekuweka kuwa nabii wa mataifa.” Yeremia 1:5
Kabla hujazaliwa Mungu tayari alikuwa na mpango na maisha yako kwamba utakapokuja duniani, uje kuujenga ufalme wa Mungu. Hivyo akakuwekea uwezesho wa namna fulani ambayo leo tunauita nyota ya mtu. Yaweza kuwa ni nyota katika biashara, masomo, utawala au nyota ya kupendwa na kuubalika. Nyota yako ilipokuwa inashuka kuingia kwenye tumbo la mama yako, shetani pia aliiona. Ndio maana kuna watu matatizo yao yalianza tangu wakiwa tumboni. Shetani anajaribu kuharibu ule mpango wa Mungu juu ya mtu. Lakini Mungu wetu ni Mungu aokoaye, ni pale tunapokuwa tumejitenga naye kwa dhambi zetu ndipo tunapompa mwanya wa kutufanya mateka.
Imeandikwa,
“Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” Yohana4:24
Mungu ni roho na kilichozaliwa na roho ni roho na huushinda ulimwengu. Tunamwita Mungu Baba kwasababu ya Roho zetu. Sisi sio miili, bali ni roho zilizotoka juu mbinguni na kuvaa miili. Biblia inasema atokaye juu yu juu ya yote hata mauti. Kama kuna kitu cha kipuuzi na cha kijinga tena kisicho na thamani hapa duniani basi kitu hicho ni mwili wa mwanadamu. Miili mingine ya wanyama kama kuku, ng’ombe, mbuzi inapokufa inaweza kutunzwa na kutumika baadae kama chakula au manufaa mengine. Lakini mwili wa mwanadamu unapokufa hauna thamani ni wa kutupa tu. Wanadamu wamejiwekea utaratibu wa namna ya kuutupa mwili ambao wanauita mazishi. Lakini ukweli ni kwamba wanachokuwa wanafanya ni kuutupa mwili husika. Roho zetu ndizo zenye thamani maana hizo hazifi hata milele. Kama sio Yesu, mwili wako hauna thamani kabisa. Paulo alijua hili ndio maana akasema, “Kwa maana si mimi ninayeishi bali Kristo aliye ndani yangu, kufa ni faida na kuishi ni Kristo. Imeandikwa,
“Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani.” Yohana 5:24
 
Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli. Kama vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami vivyo hivyo naliwatuma hao ulimwenguni.” Yohana 17: 14
Mfalme Yekonia hakuwa mjinga bali mtu mwenye hekima. Alipokubali kujisalimisha kwa Mfalme Nebukadreza alikuwa akiwaza ni heri wapelekwe uhamishoni kuliko kuipoteza nchi kabisa. Japo nchi ilibaki na watu wadhaifu tu, alikuwa anajua katika viuno vyake kulikuwa na mtoto ambaye ndiye angewatoa uhamishoni hawa wana wa Israel waliopelekwa uhamishoni.
Na baada ya ule uhamisho wa Babeli, Yekonia akamzaa Shealtieli; Shealtieli akamzaa Zerubabeli; Zerubabeli akamzaa Abihudi; Abihudi akamzaa Eliakimu; Eliakimu akamzaa Azori; Azori akamzaa Sadoki; Sadoki akamzaa Akimu; Akimu akamzaa Eliudi; Eliudi akamzaa Eleazari; Eleazari akamzaa Matani; Matani akamzaa Yakobo; Yakobo akamzaa Yusufu mumewe Mariamu aliyemzaa YESU aitwaye Kristo.” Mathayo 1:12  
Leo kanisa limehamishwa kwenye ulimwengu wa kiroho kiasi cha kutoamini uweza na nguvu za Mungu. Tumehamishwa kwenye miji ya kiroho ya uharibifu, tupo mashimoni. Lakini tumebweteka na kuridhika kukaa huku uhamishoni. Tumelima mashamba na bustani, tumeoa na kuolewa huku uhamishoni na pia tumezaa tukiwa uhamishoni. Ni wakati wa kutambua kuwa pamoja na mashamba na bustani tulizotengeneza lakini tuko uhamishoni na yatupasa kurudi kwenye asili yetu.
“Bwana amekufanya kuhani badala ya Yehoyada, kuhani, ili mpate kuwa watumishi katika nyumba ya Bwana, kwa kila mtu aliye na wazimu, na kwa kila mtu ajifanyaye kuwa nabii, umtie katika mkatale na pingu. Mbona, basi, hukumkemea Yeremia wa Anathothi, ajifanyaye kuwa nabii kwenu,  ambaye ametuma watu kwetu katika Babeli, kusema, Uhamisho huu ni wa siku nyingi; jengeni nyumba, mkakae ndani yake; pandeni bustani, mkale matunda yake.” Ezekieli 29: 26
Kwenye ulimwengu wa rohoni kuna miji ya kiroho kabisa ambayo mtu ambaye ni roho anaweza kuchukuliwa na kupelekwa huko. Miji hiyo ina nyumba, magari na kila kitu kama ilivyo kwenye ulimwengu huu. Iko miji ya kiroho ya Mungu ambayo ina nuru kuu inayoangazwa na Yesu mwenyewe.
“Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo. Nami niendako mwaijua njia.” Yohana 14:1
Na ukuta wa mji ulikuwa na misingi kumi na miwili, na katika ile misingi majina kumi na mawili ya wale mitume kumi na wawili wa Mwana-Kondoo. 23 Na mji ule hauhitaji jua wala mwezi kuuangaza, kwa maana utukufu wa Mungu huutia nuru, na taa yake ni Mwana-Kondoo.” Ufunuo 21: 14
“Nami sikuona hekalu ndani yake; kwa maana Bwana Mungu Mwenyezi na Mwana-Kondoo, ndio hekalu lake. Na mji ule hauhitaji jua wala mwezi kuuangaza, kwa maana utukufu wa Mungu huutia nuru, na taa yake ni Mwana-Kondoo. Na mataifa watatembea katika nuru yake. Na wafalme wa nchi huleta utukufu wao ndani yake.” Ufunuo 21:22-24
Pia,kuna miji ya kiroho ya giza ambayo giza lake hutokana na giza la mtawala wake shetani. Miji hii inaitwa miji ya uharibifu. Inaitwa miji ya uharibifu kwa sababu ndani yake kunafanyika mambo ya uharibifu. Huko ndiko shetani huwaweka watu na mali za watu alizoiba.
“Katika siku hiyo itakuwako miji mitano katika nchi ya Misri itumiayo lugha ya Kanaani, na kumwapia Bwana wa majeshi; mji mmoja utaitwa Mji wa uharibifu.” Isaya 19:18
“Macho yangu yamechoka kwa machozi, Mtima wangu umetaabika; Ini langu linamiminwa juu ya nchi Kwa uharibifu wa binti ya watu wangu; Kwa sababu watoto wachanga na wanyonyao, Huzimia katika mitaa ya mji. Wao huwauliza mama zao, Zi wapi nafaka na divai? Hapo wazimiapo kama waliojeruhiwa Katika mitaa ya mji, Hapo walipomiminika nafsi zao Vifuani mwa mama zao.” Maombolezo2:11-12
Katika miji hii shetani na mawakala wake hufanya kazi za giza pamoja na kuchukua watu walio imara, wenye akili, wenye nguvu, wenye uelewa mkubwa wanaong’ara na kuwapeleka kwenye miji yake ya kiroho iliyoko kuzimu. Huko watu hawa humtumikia yeye kwa namna mbalimbali katika kuujenga utawala wake wa kuzimu.
Sio mpango wa Mungu watu wake wakae uhamishoni. Ndio maana hata kipindi kile, baada ya muda mrefu wa kukaa uhamishoni Babeli, Mungu alimuinua Mfalme Koreshi akawaruhusu wana wa Israeli kurudi kwenye nchi yao. Naye mfalme Koreshi aliandika waraka kwa wafalme wengine katika njia ambayo wana wa Israeli wangeitumia kupita ili wawaruhusu kupita. Mungu anainua mfalme Koreshi kwa kanisa katika wakati huu na waraka pia umekwishaandikwa na Bwana Yesu mwenyewe. Ni wakati sasa watu wa Mungu tuhame kutoka uhamishoni katika ulimwengu wa Roho na kurudi kwenye asili yetu chini ya kiongozi wetu Yesu Kristo. Ni kweli tumejenga, tumelima uhamishoni lakini hatuna budi kuacha yote na kuirudia ile asili yetu.
Maelfu wakiwa ndani ya bonde la kukata maneno

MAOMBI
Kwa mamlaka ya jina la Yesu Kristo, ninarudi kwenye mtazamo wangu wa asili niliowekewa na Mungu. Kwa jina la Yesu ninarudi kutoka uhamishoni, ninawafyeka wale wote mnaonizuia nisirudi kwa jina la Yesu. Ninatoka uhamishoni kwa jina la Yesu, ninahama kwenye uhamisho wa kiroho kwa jina la Yesu; wale wote mlionipandikizia fikra na mitazamo ya kishetani ninawateketeza kwa moto wa Mungu. Kwa jina la Yesu ninaangusha milima yote iliyo mbele yangu, wachawi wote mlionizuia uhamishoni ninawateketeza kwa moto wa Mungu, ninawaangusha kwa jina la Yesu. Kwa damu ya mwanakondoo, nawasha moto kwenye miji yenu, natoka narudi kwenye asili yangu ya rohoni kwa jina la Yesu Kristo. Ninafungua njia ya kupita kutoka kwenye utumwa kwa jina la Yesu Kristo, ninarudi nyumbani. Ninahama kwenye ulimwengu wa roho kutoka utumwani, narudi uzimani kwa jina la Yesu; ninahama kutoka mautini narudi uzimani kwa jina la Yesu, ninahama kutoka kwenye kushindwa narudi kwenye kushinda kwa jina la Yesu, nahama kutoka kwenye kufeli, kuhuzunika, kuogopa, ninarudi kwenye asili ya ujasiri, nguvu, uweza, uimara, utajiri, mafanikio kwa damu ya mwanakondoo. Kila anayenizuia ninamsambaratisha kwa jina la Yesu Kristo. Wote mnaonizuia nisihame kwenye vifungo vyenu ninawafyeka kwa jina la Yesu. Ninarudi kwenye asili yangu ya kumiliki kutiisha na kutawala kwa jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai. Amen!












Post a Comment

0 Comments